BILIONEA DANGOTE KUSHUSHA NEEMA TANZANIA



Kampuni ya Dangote Group inayomilikiwa na bilionea kutoka Nigeria, imetangaza neema itakayotokana na uwekezaji wa kiwanda cha saruji unaofanyika mkoani  Mtwara, miongoni mwake ikiwa ni kupungua kwa bei ya saruji uzalishaji utakapoanza. 
Rais wa kampuni hiyo, Aliko Dangote, alisema kiwanda cha Saruji cha Dangote kitakapoanza, miezi sita ijayo,  licha ya bidhaa hiyo kuuzwa kwa bei ya chini, kutakuwa na ongezeko la ajira na nafasi za mafunzo, watachangia huduma za kijamii na uchumi kwa ujumla. 
Akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari jana jijini Dar es Salaam, mfanyabiashara huyo alisema watatafuta njia ya kukabili gharama zinazochangia bei ya saruji miongoni mwake, ikiwa ni kutatua tatizo la usafirishaji wa bidhaa hiyo. 
Kiwanda hicho kinajengwa kwa thamani ya dola za Marekani milioni 500 (takribani Sh trilioni 8.3). 
“Pindi kiwanda kitakapoanza kufanya kazi mwaka ujao, tutaangalia namna ya kupunguza tatizo la bei ya saruji, siku zote kuna nafasi ya kufanya hivyo katika uzalishaji,” alisema. 
Bei ya saruji hutegemea maeneo huku usafiri ukitajwa kuwa chanzo cha ongezeko hususani kwa mikoa ya pembezoni. Wakati jijini Dar es Salaam, bei yake ni kati ya Sh 13,000 na 15,000, baadhi ya mikoa, bei inazidi Sh 20,000. 
Kwa mujibu wa Dangote, awali kiwanda chake kililenga kuzalisha tani milioni 1.5 kwa mwaka lakini sasa baada ya kukamilika,  kitazalisha tani milioni tatu kwa mwaka.
Alisema kampuni imepanga kuingiza malori 250 kwa kuanzia, yatakayotumika kusambaza bidhaa hiyo  nchini. 
 “Usafirishaji ni ghali sana kwa nchi za Afrika Mashariki, lakini sisi tumejipanga kuingiza malori yatakayosaidia kusambaza ingawa tutatumia na njia nyingine pia.”
Wakati huo huo , kuhusu upatikanaji wa wafanyakazi wenye ujuzi kwa ajili ya kufanya kazi kwenye kiwanda, alisema wamepanga kuchukua wahandisi kutoka Tanzania na kwenda kupata mafuzo ya nadharia na vitendo katika chuo cha Dangote Academy kilichoko Abuja nchini Nigeria.
 “Kuna baadhi ya wahandisi wa kitanzania ambao wamefanyiwa usaili kwa ajili ya kujiunga na chuo chetu na watapata nafasi ya kujifunza kwa nadharia na vitendo kwa kufanyakazi kwenye kiwanda chetu, ili wakirudi watumike katika uzalishaji na kuwafundisha wengine.
Alisema, “Kwa suala la ajira, theluthi mbili ya wafanyakazi watakuwa ni Watanzania na pia kutakuwapo na wafanyakazi wageni ambao hata hivyo hawatakaa milele, watakuwa na kazi ya kusaidia ujuzi na kiwanda kitakapotengamaa wataondoka.”
Alipoulizwa yeye kama mmoja wa matajiri wa Afrika, nini anachotamani kifanyike kila anapoamka, Dangote alisema nia yake ni kuiona Afrika inapiga hatua ya juu ya maendeleo.
Akizungumza mchango wa huduma za kijamii, Dangote alisema: “ Ingawa wajibu wa kutoa huduma kwa wananchi ni serikali, lakini sisi tunatarajia kuchangia katika huduma ya afya, maji, shule, nafasi za elimu na kuwajengea soko wananchi wa Mtwara.

No comments: