Majambazi wamemuua kwa kumpiga risasi Mhasibu
wa Kanisa Katoliki, Usharika wa Makoka, jijini Dar es Salaam, Sista
Prisencia Kapuli na kisha kumpora fedha zinazokadiriwa kuwa zaidi ya Sh milioni
10 alizokuwa nazo.
Tukio hilo ni la jana saa 9 alasiri katika
eneo la Ubungo Riverside wakati Prisencia, mtawa mwenzake pamoja na dereva wao,
Mark Mwarabu, walipokwenda katika eneo hilo kununua mahitaji ya
kanisa.
Taarifa za mashuhuda wa tukio hilo
zilizothibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura,
zilisema walikuwa wakitoka benki. Hata hivyo Kamanda hakutaja kiasi
kilichoporwa isipokuwa inadaiwa mtawa aliyenusurika ndiye alisikika
akisema.
Inadaiwa baada ya gari lililowabeba watumishi hao
wa kanisa kufika eneo hilo, Prisencia alishuka akiwa na mkoba kwenda duka la
mchele na ghafla majambazi hao waliokuwa kwenye pikipiki mbili aina ya Boxer,
walimvamia na kuanza kumnyang’anya mkoba wake uliokuwa na fedha hizo.
“Wakati wakiendelea kuvutana ndipo mmoja wa
majambazi hao aliyekuwa akivuta mkoba huo akampiga bastola shingoni.
Hatua hiyo ilifanya auachie mkoba na kudondoka,” alisema shuhuda na
kwamba walimpiga risasi dereva kwenye kidole. Kamanda Wambura alisema
uchunguzi wa tukio hilo unaendelea.
No comments:
Post a Comment