MBOWE ATAKA WANAOUNDA UKAWA WAJIIMARISHE



Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) vikiwa na matumaini ya kuunganisha nguvu katika uchaguzi mkuu ujao, vimeambiwa kila kimoja kijiimarishe kivyake katika mapambano ya kisiasa. 
Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Freeman Mbowe, amesema vyama hivyo, visitegemee nguvu ya umoja huo badala yake, vijiimarishe kuleta ushindani katika harakati zao za kisiasa wanazoendelea kuzifanya. 
Mbowe ambaye chama chake ni miongoni mwa vinavyounda Ukawa, alisema hayo jana katika mkutano mkuu wa sita wa Chama cha Wananchi (CUF) ambacho pia ni mwana Ukawa. 
Kingine ni NCCR Mageuzi ambavyo kwa pamoja vilifikia maafikiano ya kutoishia kwenye ushirikiano katika masuala ya katiba mpya, bali pia masuala mengine kisiasa ikiwemo kuunda kambi rasmi ya upinzani bungeni. 
 “Ni vizuri sasa wakati tupo katika harakati hizi kupitia Ukawa, kila chama kwa nafasi yake, kikajiimarisha ili tunapokuwa ndani ya Ukawa kila kimoja kikawa na nguvu zake hatua itakayosaidia harakati zetu,” alisema Mbowe. 
Hata hivyo Mbowe alisisitiza kwamba  ushirikiano wa vyama hivyo kupitia  Ukawa,  unaweza kuwa wa umuhimu  ingawa unabezwa na baadhi ya vyama.
Aliendelea kusisitiza, umoja huo siyo mapito bali utaendelea hata suala la Katiba litakapoisha. “Umoja huu siyo mwisho wake katika Katiba, lazima utaendelea kutuongoza mbele katika mipango mingine na hata uchaguzi mkuu ujao hivyo wanaotubeza wajue hizo ndiyo salamu zetu,” alisema Mbowe.
Katika mkutano mkuu huo ambao Chama Cha Mapinduzi (CCM) pia kilialikwa na kuwakilishwa na Makamu Mwenyekiti wake, Bara, Philip Mangula, alisema umoja waliounda ni mzuri. 
Aliwaambia, “mkiwa vyama vingi dhaifu na mkajiweka katika umoja wa pamoja ni vizuri  kuliko mmoja mmoja kwa kuwa kutasaidia kuleta upinzani. ”
Alisema hata Baba wa Taifa , Mwalimu Julius Nyerere kipo kipindi alitamani CCM igawanyike katika makundi mawili ili kuchagiza kukuza ushindani. Alisema ujio wa vyama vingie umesaidia kuleta upinzani huo katika kipindi hiki.
Aidha Mangula alitaka vyama vyote kujenga tabia ya kuvumiliana kukuza demokrasia ya kweli . Alisema kwa kufanya hivyo kutasaidia kuondoa vurugu za kisiasa za mara kwa mara zinazojitokeza nchini. 
 Mangula alipongeza CUF kwa mkutano huo pamoja na mwaliko kwa chama chake. Pia alieleza kufurahishwa na demokrasia ndani ya chama hicho hususani, kutokana na uwezo wake wa kukutanisha wajumbe wake katika mkutano huo.
Alisema kufanya mkutano kama huo, ndiyo demokrasi ya kweli. Alieleza kushangazwa na hatua ya Msajili wa Vyama vya Siasa  kuendelea kufumbia macho baadhi ya vyama ambavyo licha ya kupewa usajili wa kudumu, havijawahi kuitisha mkutano hata mmoja.
Wakati huo huo Profesa Lipumba alitaka wajumbe wa mkutano huo kuhakikisha wanakamilisha kikamilifu mchakato wa uchaguzi wa kuwapata viongozi mbalimbali wa chama hicho  kuepuka kuleta makundi yatakayogharimu chama hicho siku zijazo. 
Alisema wajumbe wanapaswa kutambua kuwa uchaguzi usio na vijembe, utasaidia kukuza demokrasia ya kweli ndani ya chama hicho wakati wakijiandaa kuelekea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

No comments: