Mbunge wa Konde, Khatibu Said Haji (CUF)
amesema wanawake wameadhibiwa na Mungu katika maandiko matakatifu na kuhoji
hawaoni kuwa harakati zao za kudai haki sawa, ikiwemo uwakilishi wa asilimia 50
kwa 50 katika nafasi za uamuzi kuwa ni kuingilia adhabu hiyo halali.
Alisema hayo bungeni jana, kwenye swali
la nyongeza baada ya Mbunge wa Viti Maalumu, Leticia Nyerere, kuomba Serikali
ipeleke muswada wa sheria bungeni, utakaowalazimisha waajiri kuajiri
wafanyakazi kwa kuzingatia asilimia 50 wanaume na asilimia 50 wanawake.
Huku Naibu Spika, Job Ndugai,
‘akichomekea’ kuwa hoja hiyo haiungwi mkono ndio maana hakuna makofi mengi ya
wabunge, Leticia alisema kwa kuwa wako wanawake wenye uwezo, elimu na makini
kuliko wanaume ni vyema sheria hiyo ifikishwe bungeni, ili kuwalazimisha
waajiri kuifuata.
Akijibu hoja ya Khatibu, Waziri wa
Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba, alisema kama Mbunge wa
Konde anazungumzia sheria ya dini, yeye ameisoma lakini haki za wanawake
zilizopo katika sheria hiyo ya dini, zimekuwa zikidhulumiwa.
Alitoa mfano wa haki ya mwanamke
aliyeolewa kufuliwa nguo na mumewe ambayo iko katika sheria ya dini, ambayo
alisema mfano unaoonesha namna haki hizo za wanawake zilizopo katika sheria ya
dini, zinavyodhulumiwa.
Baada ya kutoa jibu hilo, alisimama
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaaa
(Tamisemi), Hawa Ghasia aliyesema kitabu kitakatifu cha Kurani, kimeweka wazi
kuwa mwanamume ndiye mlinzi wa mwanamke na kufafanua kuwa katika hali ya
kawaida, mlinzi ni mtu muhimu lakini anayelindwa ni kiongozi.
Hata hivyo Waziri Simba katika majibu,
alisema Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za makusudi kutimiza lengo
la uwiano sawa kati ya wanawake na wanaume.
Akizungumza nje ya ukumbi wa Bunge, Mbunge
Haji alifafanua adhabu aliyosema wanawake wamepewa na Mungu akinukuu kitabu cha
Mwanzo katika Biblia kwamba mwanamke alipewa adhabu mbili; moja ya kuzaa kwa
uchungu na ya pili ya kuwa chini ya mamlaka ya mwanamume.
No comments:
Post a Comment