PINDA AALIKA WAWEKEZAJI KATIKA MADINI NA NISHATI



Waziri Mkuu, Mizengo Pinda amewataka wafanyabiashara na wawekezaji wa Tanzania na China kutumia fursa zilizopo katika nchi hizo kuwekeza katika sekta mbalimbali ili kuinua uchumi wao na mataifa haya mawili.
Pamoja na hayo, Pinda alitumia fursa hiyo, kuinadi Tanzania kuwa ni moja kati ya nchi za Afrika yenye mazingira mazuri ya uwekezaji hasa katika sekta za kilimo, nishati, madini na utalii.
Alikuwa akizungumza katika ufunguzi wa Kongamano la pili la biashara baina ya China na Tanzania ambalo pia lilihudhuriwa na Makamu wa Rais wa China, Li Yuanchao, aliyeko nchini kwa ziara ya kikazi ya takribani wiki moja.
"Napenda niwajulishe kuwa uamuzi wenu wa kufanya biashara na Tanzania ni muafaka kwa kuwa nchi hii, mbali na kubarikiwa rasilimali nyingi, lakini pia ina utulivu wa kisiasa, inasifika kwa amani na ina nguvu kazi nyingi," alisisitiza.
Katika hatua nyingine,  Makamu huyo wa Rais wa China akiongozana na Pinda, aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo la Mfuko wa Mwalimu Nyerere (MNF), jijini Dar es Salaam linalojengwa na Kampuni ya China Railway Group Limited. 
Rais wa kampuni hiyo, Dai Hegen ameahidi kwamba jengo litakuwa mradi wa daraja la juu katika menejimenti, ubora, ufanisi, teknolojia na uzoefu. Kampuni ya China Railway Jianchang Engineering Co. (T) Limited, ambayo ni kampuni tanzu ya China Railway Group Limited ndiyo itakayojenga jengo hilo.
Kwa mujibu wa Rais huyo, Jengo la MNF litajengwa katika kiwanja chenye ukubwa meta za mraba 61,000 na litakuwa na hoteli ya nyota tano, ofisi za kiwango cha daraja la kwanza, na eneo la maegesho.
Katika kongamano hilo, pia China na Tanzania zilisaini mkataba wenye thamani ya dola za Marekani milioni 200 kwa ajili ya kuisaidia Mamlaka ya Majisafi na Majitaka (Dawasco) katika ujenzi wa bwawa la Kidato, mtambo wa maji na miundombinu yake mkoani Morogoro.

No comments: