Bodi
ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu imekusanya zaidi ya Sh bilioni 49.7 ya
mikopo kutoka kwa wanufaika wa mikopo hiyo hadi kufikia Aprili 30, mwaka huu.
Kiasi
hicho cha fedha kilichokusanywa na Bodi ni sawa na asilimia 55 ya mikopo
iliyopaswa kuwa imerejeshwa ya zaidi ya Sh bilioni 90.
Hayo
yalibainishwa mwishoni mwa wiki na Kaimu Mkurugenzi wa Bodi hiyo, Asange Bangu
wakati wa ufunguzi wa ofisi ya Bodi hiyo Kanda ya Ziwa.
Alisema
hadi kufikia Aprili 30, mwaka huu idadi ya wanufaika wa mikopo waliotafutwa na
kujulikana mahali walipo walikuwa 97,823 sawa na asilimia 68 ya wanufaika
wote wa mikopo 143,281 ambao mikopo yao imeiva.
Bangu
alisema idadi ya wanafunzi wa elimu ya juu imezidi kuongezeka mwaka hadi mwaka
ambapo mwaka 2005/06 wanafunzi walionufaika na mikopo walikuwa 42,729
waliokopeshwa kiasi cha Sh 56,111,371,485.
Alisema
katika mwaka wa fedha 2013/2014, Bodi imekwishatoa mikopo kwa wanafunzi 95,241
ambao wamekopeshwa kiasi cha Sh 333,507,422,641, fedha ambazo zinajumuisha
ruzuku kutoka serikalini na za urejeshwaji wa mikopo.
Alisema
uanzishwaji wa ofisi za Kanda ni muendelezo wa utekelezaji wa Mpango Mkakati wa
Bodi uliolenga kusogeza huduma karibu na wadau wake na pia kuongeza kasi ya
ukusanyaji wa marejesho ya mikopo iliyoiva.
Akizindua
ofisi ya Bodi, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Baraka Konisaga alisema wastani wa
wanafunzi wanaotakiwa kwenda elimu ya juu kwa Tanzania ni asilimia 3.9
wakati kwa nchi zilizo chini ya Jangwa la Saharani ni asilimia 5.
Konisaga
alisema hali ya kuwa na kiwango cha chini kimechangiwa na ufinyu wa rasilimali
fedha kwa wananchi jambo ambalo liliifanya Serikali kuanzisha utaratibu wa
utoaji wa mikopo ili kuwawezesha wanafunzi wengi zaidi kupata elimu.
“Ili
kujenga Mfuko endelevu utakaowawezesha wanafunzi wengi kunufaika, ni budi
kuhakikisha mikopo inayotolewa inarejeshwa kwa wakati,” alisema Konisaga.
Alisema
mara kadhaa limekuwa likizungumzwa suala la utoaji wa mikopo, lakini
urejeshwaji wake haliguswi hivyo ni wajibu wa kila mzalendo aliyepata mkopo
kuurejesha kwa ajili ya manufaa ya vizazi vijazo.
No comments:
Post a Comment