Wamiliki wa daladala katika Jiji la Dar
es Salaam wameonesha hofu ya kutupwa nje ya Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka
(DART) wakati wakielekea katika mchakato wa kuingia katika ushindani wa zabuni
itakayotangazwa kimataifa.
Hata hivyo, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dar
es Salaam, Raymond Mushi amewataka kujiamini na kujipanga, akisisitiza hakuna
kisichowezekana.
Hofu ya wamiliki hao ilibainika wakati
wa mkutano wa majadiliano ya wamiliki wa daladala, wakavyoweza kutambua fursa
za uwekezaji kwenye mfumo wa DART, uliofanyika jana jijini Dar es Salaam na
kuhudhuriwa na wadau mbalimbali usafirishaji.
Wamiliki hao wanahofu kushindwa katika zabuni ya kuendesha mradi
huo kwa kile wanachoeleza kutokuwa na mtaji mkubwa na uzoefu vitu ambavyo ni
kigezo kikubwa katika zabuni ya mradi huo.
Walihoji inakuwaje zabuni inatangazwa
wakati wao wapo na wamefanya kazi miaka
mingi ya kutoa huduma katika Jiji la Dar es Salaam wakati mazingira ambayo si
rafiki ikiwa ni pamoja na kuwa na miundombinu mibovu na kutaka zabuni
isitangazwe kimataifa.
Wakichangia kwa nyakati tofauti
wamiliki hao waliitaka Serikali kuwasaidia kwa hali na mali ili waweze
kushiriki katika mradi huo ikiwa ni pamoja na kuwafanya kuwa waendeshaji wakuu.
Mwenyekiti wa Wamiliki wa Daladala Mkoa
wa Dar es Salaam (DARCOBOA), Sabri Mabrouk alisema tayari wamiliki hao
wameanzisha kampuni inayoitwa Mzizima Daladala Express, lakini wana hofu iwapo
watapata nafasi ya kushiriki uendeshaji wa mradi huo.
Mabrouk alisema mashaka yao ni kuwa
wanahisi kutengwa katika mradi huo kutokana na hatua ya kuambiwa daladala zao
zitaondolewa na kwenda kwenye barabara za pembezoni wakati miaka yote wamekuwa
wakitumia barabara hizo katika mazingira ambayo si rafiki.
“Hatuna tatizo na mradi lakini siasa
nyingi imekuwa ikitumika hapa, tunaambiwa daladala zetu ziende katika barabara
za pembezoni wakati barabara hizo ni mbovu…miaka yote tumetumia barabara hizi
leo miundombinu inaboreshwa ndio tunaambiwa tuhame,” alisema.
Ruth Majura alisema wamiliki wa
daladala, wameanzisha kampuni, lakini changamoto inayowakabili ni ukosefu wa
fedha kwa ajili ya kuandaa mpango wa kibiashara utakaowawezesha kuingia katika
ushindani wa zabuni ya mradi huo.
Kwa upande wake, Gwamaka Nsekela
alisema wamiliki wa daladala wana nafasi finyu ya kuingia katika tenda hiyo ya
kimataifa na kuhoji iwapo kweli serikali ilikuwa na nia wamiliki hao wazawa
kushiriki katika mradi huo mkubwa.
Katibu mstaafu wa Chama cha Wamiliki wa
Daladala Mkoa wa Dar es Salaam (DARCOBOA), Mujengi Gwao akichangia katika
mkutano huo, alisema wakati Serikali inaanza mradi huo, iliahidi kuwabeba
wazawa na kuitaka Serikali iwasaidie wamiliki wa daladala kwa hali na mali ili
waweze kushiriki kikamilifu katika mradi huo.
Mtendaji Mkuu wa DART, Asteria Mlambo akijibu
hoja za wadau hao alisema zabuni hiyo haijaletwa ili kuwaondoa wamiliki wa
daladala, bali ni utaratibu uliowekwa kuhakikisha anapatikana mtu atakayeweza
kuendesha mradi huo kwa ufanisi.
Aliwataka wamiliki hao kuimarisha,
kuijengea nguvu na uwezo kampuni yao ili waweze kuingia katika ushindani wa
zabuni na kuongeza kuwa kwa mujibu wa Sheria na Taratibu Serikali haiwezi kutoa
upendeleo wowote kwa wazawa hao.
Mshauri Mwezeshaji wa DART, Felix Mlaki
aliwataka wamiliki hao kufanya juhudi kutafuta mtaji wa kutosha katika kampuni
yao kwa kile alichoeleza kuwa kigezo kimojawapo katika zabuni hiyo ni mtaji na
uzoefu na kwamba Juni 3 na Juni 4, mwaka huu kutakuwa na mkutano wa wadau wa
ndani na nje kujadili namna ya kushiriki katika zabuni.
Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,
Raymon Mushi aliyekuwa mgeni rasmi katika mkutano huo alisema hakuna
lisilowezekana na kuwataka wamiliki hao kujipanga, kuimarisha kampuni yao ili
iweze kuingia kwenye ushindani.
No comments:
Post a Comment