JAJI AHIMIZA HAKI ZA WANAWAKE KUZINGATIWA



Wadau wa haki jinai mkoani Kagera wametakiwa kuzingatia haki za akinamama na watoto, ambao  ni waathirika wa vitendo vya kikatili ili waweze kupata haki zao za msingi.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba, Peragia Khadai wakati wa kikao cha siku moja cha  wadau hao kutoka wilaya zote za mkoa huo kwa lengo la kutekeleza miongozo, kanuni na maelekezo ya viongozi wao.
“Sio kwamba napendelea kundi hilo la akinamama ambao huathirika na vitendo vya kikatili, bali tuzingatie udhaifu wa kundi hili kwani wamekuwa wakipata taabu wanapofika  mahakamani,  hawana uzoefu katika kuweka mawakili wa kuwatetea hivyo tuwasaidie na kuwasikiliza wasije kuathirika mara ya pili ,” alisema.
Alisema takwimu zinaonesha katika Mkoa wa Kagera bado yapo mashauri mengi ya jinai, ambayo  ni ya muda mrefu kuanzia mwaka 2009.
Alisema baadhi ya watuhumiwa wapo mahabusu katika magereza ya mkoa muda mrefu,  kwa hiyo ni vema suala hili likapatiwa ufumbuzi ni kwa jinsi gani linaweza kumalizika.
Aliwataka wapelelezi wakiongozwa na Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai  wa Mkoa, Henry Mwaibambe kufanya kazi yao kwa weledi kwa kutumia vifungu vya sheria, kanuni na miongozo mbalimbali na kuzingatia masuala ya haki za binadamu katika hatua zote za upelelezi.
Kwa upande wake, Wakili wa Serikali, Sakina Sindah alisema wamekuwa wakijikuta na masuala mengi juu ya utekelezaji wa sheria mpya ya watoto, hasa wale wanaokabiliwa na tuhuma za jinai katika vituo  vya polisi.
Alisema kupitia wadau hao, wataweza kulitatua na kulipatia ufumbuzi.

No comments: