Wamiliki
wa mabasi ya abiria Dar es Salaam na wadau wengine watakutana jijini humo
kujifunza fursa na kufahamu namna ya kushiriki katika mradi wa mabasi yaendayo
haraka (BRT) unaotarajiwa kuanza baadaye mwaka huu.
Kwa
mujibu wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART), mkutano huo unatarajiwa
kufanyika kesho katika Ukumbi wa Karimjee na utatumika pia kuelezea mkutano
mwingine wa kimataifa utakaofanyika Juni 3 na 4 kujadili kuanza kwa awamu ya
kwanza ya mradi huo jijini Dar es Salaam.
Mtendaji
Mkuu wa DART, Asteria Mlambo aliwaambia waandishi wa habari jijini humo jana
kuwa, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki atakuwa mgeni rasmi katika
mkutano huo muhimu.
“Mkutano
huo unalenga kuwaelezea wamiliki wa mabasi ya abiria maarufu kama daladala na
wale wa UDA fursa za mradi wa mabasi yaendayo haraka na jinsi wanavyoweza kuwa
wadau, wataelezewa faida na fursa za mradi huo mpya na jinsi wanavyoweza
kushiriki,” alisema Mlambo.
Mkutano
huu pia unalenga kupata maoni ya wadau hao wa usafiri na kuyatumia kama mchango
katika mkutano wa kimataifa wa Juni. Aliwataka wamiliki hao wa mabasi ya abiria
kuhudhuria kwa wingi na kushiriki kikamilifu.
Aprili
mwaka huu, DART ilikamilisha zoezi la kusajili mabasi ya daladala yanayopita
katika barabara ya Morogoro na yake yanayokatiza katika njia hiyo.
Hatua
hiyo ilikuwa moja ya matayarisho ya kupisha mradi huo wa mabasi yaendayo haraka
na hivi sasa wakala huo uko kwenye mchakato wa kuwezesha upatikanaji wa watoa
huduma kwenye mfumo mpya wa mabasi yaendayo haraka awamu ya kwanza.
Awamu
hiyo inajumuisha barabara ya Morogoro, Kawawa na mtaa wa Msimbazi kwa njia kuu
na nyingine za kiungo. Kulingana na mpango wa uendeshaji wa mfumo wa DART,
barabara zinazohusika zitapaswa kutumiwa na mabasi ya mfumo huo pekee.
Jumla
ya njia 64 jijini Dar es Salaam zitakoma kutumika kutokana na kuanza kwa mradi
huo unaolenga kupunguza tatizo sugu la msongamano wa magari jijini humo.
No comments:
Post a Comment