Wakimbizi wenye asili ya Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Burundi wapatao 32,000 walioko nchini,
wanatarajiwa kuhamishiwa Marekani.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,
Mathias Chikawe alitoa taarifa hiyo jana bungeni mjini hapa, kwamba huo ni
mpango maalumu unaotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano.
Alisema unatekelezwa katika mwaka wa
fedha 2014/2015 kwa kushirikiana na Serikali ya Marekani baada ya serikali
kusaini mkataba na mashirika ya Shirika la Umoja wa Mataifa Linaloshughulikia
Wakimbizi (UNHCR) na Shirika la
Kimataifa la Uhamiaji (IOM).
“Katika mwaka 2014/2015, Serikali kwa
kushirikiana na Serikali ya Marekani itaanza kutekeleza Mpango Maalumu wa
kuwahamishia nchini Marekani wakimbizi wenye asili ya DRC na Burundi wapatao
32,000…,” alisema.
Aidha, alisema katika mwaka 2013/2014
serikali kupitia wizara hiyo, ilitoa uraia kwa wakimbizi wa Kisomali 1,514
wenye asili ya kibantu waliokuwa wakiishi katika makazi ya Chogo wilayani
Handeni mkoani Tanga.
Kwa kuzingatia uamuzi huo, makazi hayo
yamefungwa rasmi Februari mwaka huu na wakimbizi wapatao 150 ambao wamebaki
katika eneo hilo wataendelea kuishi hapo kwa mujibu wa sheria ya wakimbizi ya
mwaka 1998.
Waziri alisema hadi Machi 31 mwaka huu,
idadi ya wakimbizi ambao wanahifadhiwa nchini ilikuwa 97,783 ikilinganishwa na
wakimbizi 101,183 waliokuwepo nchini Machi 31 mwaka jana.
Wakati huo huo, waziri alisema katika
mwaka 2014/15, serikali itaendelea na jitihada za kupata ufumbuzi wa kudumu wa
tatizo la wakimbizi kwa kuwarejesha nyumbani ambao hali ya amani na usalama
itakuwa imerejea kwenye nchi zao za asili.
Aidha taratibu zinakamilishwa kuhusu
hatma ya wakimbizi wa Burundi wapatao 162,156 wa mwaka 1972.
No comments:
Post a Comment