WAHITIMU 24,000 KIDATO CHA NNE HAWANA MATOKEO



Watahiniwa 24,204 wa Kidato cha Nne mwaka 2013, hadi sasa hawajawasilisha malipo ya ada zao kwa Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA), ili kupatiwa matokeo yao, Bunge limefahamishwa.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa alisema hayo bungeni akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Kuruthum Mchuchuli (CUF).
Mchuchuli alitaka kufahamu ni wanafunzi wangapi wa Kidato cha Nne ambao hawajapata matokeo yao kwa sababu ya kutolipa ada za mitihani.
Dk Kawambwa alisema matokeo ya Kidato cha Nne 2013 yalitangazwa Februari 21, 2014 ambapo matokeo ya watahiniwa 31,518 kati ya 404,083 waliofanya mtihani huo yalizuiwa kwa sababu za kutolipa ada.
“Idadi hiyo ni sawa na asilimia 7.79 ya watahiniwa waliofanya mtihani. Matokeo ya mtahiniwa yaliyozuiwa hufunguliwa mara moja baada ya mtahiniwa husika kulipa ada yake ya mtihani.
“Hadi tarehe 8, Mei 2014, jumla ya watahiniwa 7,314 wameshawasilisha ada zao na kufunguliwa matokeo yao na hivyo idadi ya watahiniwa ambao bado hawajawasilisha malipo yao ya ada ni 24,204,” alisema Waziri Dk Kawambwa.
Aliwahimiza wazazi na walezi wa watahiniwa ambao matokeo yao yamezuiliwa kwa kutolipa ada ya mtihani, kulipa ada hizo mapema ili matokeo hayo yafunguliwe na kutoa fursa ya wanafunzi hao kuendelea na kozi mbalimbali kulingana na matokeo hayo.

No comments: