BAJETI YA WIZARA YA UJENZI



HOTUBA YA WAZIRI WA UJENZI, MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE MAGUFULI (MB), AKIWASILISHA BUNGENI MPANGO WA MAENDELEO NA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA WA FEDHA 2014/15

A.        UTANGULIZI

1. Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali kupokea na kujadili Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2013/14. Aidha, lijadili na kupitisha Mpango na Bajeti ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2014/15.

2. Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunilinda na kunipa nguvu na kuniwezesha kusimama hapa mbele ya Bunge lako Tukufu kuwasilisha bajeti hii ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2014/15. Ni Mungu pekee aliyetulinda kipindi tulipopata ajali ya helikopta mnamo tarehe 13 Aprili, 2014 nikiwa pamoja na Viongozi wengine wa Serikali.  Ninawashukuru sana kwa sala zenu.

3. Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa wetu, kwa kuwa mstari wa mbele katika kutafuta fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo.   Aidha, nawapongeza Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilali, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, Waziri Mkuu kwa namna ambavyo wamemsaidia Mheshimiwa Rais kusimamia na kuongoza shughuli zote za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

4. Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua nafasi hii kutoa rambirambi na salamu za pole kwako wewe Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa wabunge, familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu Dkt. William Mgimwa na Marehemu Saidi Bwanamdogo, waliokuwa Wabunge wa Jimbo la Kalenga na Jimbo la Chalinze. Naungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa pole na kumwomba Mwenyezi Mungu aendelee kutoa faraja kwa familia na ndugu. Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema peponi, Amina.

5. Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kuwapongeza Mheshimiwa Godfrey Mgimwa (Mb.) na Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete (Mb.), kwa kuchaguliwa kuwa Wabunge.

6. Mheshimiwa Spika, nawapongeza wajumbe wote wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu chini ya uongozi wa Mwenyekiti Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba (Mb.) na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Profesa Juma Athumani Kapuya (Mb.) kwa ushauri wao wenye tija kwenye sekta ya Ujenzi. Wizara ya Ujenzi inazingatia ushauri unaotolewa na Kamati hii pamoja na Wabunge wote katika utekelezaji wa majukumu yake. Aidha, nampongeza Mhe. Felix Mkosamali (Mb) kwa kuteuliwa kuwa Waziri Kivuli wa Wizara ya Ujenzi toka Kambi ya Upinzani.

7.  Mheshimiwa Spika, ufafanuzi kuhusu Dira, Dhima, Majukumu, Malengo na Mikakati ya Wizara Ujenzi umeainishwa katika Kitabu cha Hotuba ya Bajeti ukurasa wa 4 - 7. 




B:       TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA MWAKA WA FEDHA 2013/14

8. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14, Wizara ilipanga kukusanya Shilingi 45,047,550.00. Hadi kufikia Aprili, 2014 Shilingi 40,385,200.00 zilikuwa zimekusanywa (sawa na asilimia 89.65). Aidha, Wizara ilitengewa kiasi cha Shilingi 381,205,760,000.00 kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida. Hadi kufikia Aprili 2014, Shilingi 372,088,829,186.73 zilitolewa na HAZINA kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida (sawa na  asilimia 97.61). Kati ya fedha hizo zilizotolewa, Shilingi 18,196,824,680.00 ni kwa ajili ya Mishahara ya Watumishi wa Wizara na Taasisi zake, Shilingi 352,114,418,206.73 ni fedha za Mfuko wa Barabara na Shilingi 1,777,586,300.00 ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo ya Wizara na Taasisi zake.

9. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14, Wizara iliidhinishiwa na Bunge Shilingi 845,125,979,000.00 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kati ya fedha hizo, Shilingi 448,174,599,000.00 ni fedha za ndani na Shilingi 397,051,380,000.00 ni fedha za nje. Fedha zilizotolewa hadi Aprili, 2014 ni Shilingi 604,405,943,800.00 ambazo zinajumuisha Shilingi 347,328,096,167.00 fedha za ndani na Shilingi 257,077,847,633.00 fedha za nje. Kiasi cha fedha zilizotolewa ni sawa na asilimia 71.52 ya fedha iliyoidhinishwa na Bunge kwa mwaka wa fedha 2013/14.

10.        Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Aprili, 2014, kwa upande wa barabara kuu, jumla ya kilomita 600.17 kati ya kilomita 495 zilizopangwa kujengwa kwa kiwango cha lami zilikamilika na kilomita 193.5 kati ya kilomita 190.00 zilizopangwa zilikarabatiwa kwa kiwango cha lami.  Kwa upande wa barabara za mikoa kilomita 59.25 kati ya kilomita 66.1 zilijenga kwa kiwango cha lami na kilomita 424.5 kati ya kilomita 867.6 zilifanyiwa ukarabati kwa kiwango cha changarawe.

11.        Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Madaraja manne (4) ya Kikwete katika Mto Malagarasi, Nangoo, Nanganga na Ruhekei ulikuwa umekamilika.  Aidha, ujenzi wa madaraja makubwa 6 (Kigamboni, Mbutu, Maligisu, Kavuu, Kilombero na Sibiti) unaendelea vizuri na usanifu wa daraja la Ruhuhu unaendelea.

12.        Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mwezi Aprili, 2014 jumla ya km 7,412 kati ya km 11,276.87 na madaraja 836 kati ya 1,272 ya barabara kuu yalifanyiwa matengenezo ya kawaida na ya muda maalum (routine and periodic maintenance) na kwa upande wa barabara za mikoa km 14,192 kati ya 24,489.09 na madaraja 707 kati ya 1,305 yalifanyiwa matengenezo.  Ufafanuzi zaidi kuhusu Miradi ya Ujenzi na Ukarabati wa Barabara na Madaraja umefafanuliwa zaidi katika Kitabu cha Hotuba ya Bajeti Ukurasa 10 - 71.

13.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara imeendelea kutekeleza miradi ya barabara za kupunguza msongamano wa magari katika jiji la Dar es Salaam zenye urefu wa kilometa 109.35 na kuwezesha kukamilika kwa Barabara ya Ubungo Bus Terminal – Mabibo – Kigogo Round About (km 6.4) na barabara ya Jet Corner – Vituka – Devis Corner (km 10.30). Aidha, Barabara ya Kigogo Round About – Bonde la Msimbazi – Twiga/Msimbazi Jct (km 2.7); Mkandarasi anaendelea na kazi ya kujenga kwa kiwango cha lami ambapo maendeleo ya mradi kwa ujumla yamefikia asilimia 75.
14.       Mheshimiwa Spika, barabara ya Tabata Dampo – Kigogo (km 1.65) na Ubungo Maziwa - External (km 2.25)  kazi za ujenzi kwa kiwango cha lami zinaendelea.

15.       Mheshimiwa Spika, Mradi wa Ujenzi wa Miundombinu ya Mabasi Yaendayo Haraka unahusisha ujenzi wa barabara kutoka Kimara hadi Kivukoni (km 15.8), Magomeni hadi Morocco (km 3.4) na Fire hadi Kariakoo km (1.7) pamoja na vituo vya mabasi 27, vituo vikubwa (depots) vya mwisho vitatu katika maeneo ya Kimara, Ubungo na Morocco na madaraja ya waenda kwa miguu matatu. Hadi kufikia Aprili, 2014, kazi zilizofanyika ni asilimia 65.

Aidha, Karakana (Depot) ya Jangwani; imefikia asilimia 70 na Ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi (Terminal) cha Kivukoni umefika asilimia 95. Pia Ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi (Terminal) cha Kariakoo kazi zimeanza (mobilization).

16.       Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa Vituo vya Mlisho (Feeder Stations) katika maeneo ya Urafiki, Shekilango, Magomeni Mapipa, Kinondoni, Mwinyijuma na Fire, hadi Aprili, 2014, maendeleo ya mradi kwa jumla ni asilimia 45.

17.       Mheshimiwa Spika, Barabara ya Mbezi (Morogoro Road) – Malamba Mawili – Kinyerezi - Banana (km 14); mkataba wa mradi huu umesainiwa na maandalizi ya ujenzi kwa kiwango cha lami yanaendelea.  

Barabara ya Tegeta  Kibaoni - Wazo Hill – Goba - Mbezi Mwisho (km 20); mkataba umesainiwa na maandalizi ya ujenzi kwa kiwango cha lami yanaendelea.

Barabara ya Tangi Bovu-Goba (km 9); nayo mkataba umesainiwa na maandalizi ya ujenzi kwa kiwango cha lami yanaendelea.

Barabara ya Kimara Baruti-Msewe (km 2.6); Barabara hii inasaidia kupunguza msongamano wa magari hasa katika barabara ya Morogoro kuingia na kutoka katikati ya jiji. Mkataba umesainiwa na maandalizi ya ujenzi kwa kiwango cha lami yanaendelea.

18.       Mheshimiwa Spika, Barabara ya Kimara – Kilungule - External Mandela Road (km 9); mkataba wa awamu ya kwanza wa makutano ya barabara ya External na Mandela hadi Maji Chumvi (km 3.0) umesainiwa na maandalizi ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami yanaendelea.

Barabara ya Kibamba – Kisopwa (km 12.0); Mkataba wa ujenzi kwa kiwango cha lami umesainiwa.  Aidha, barabara ya Mwenge – Tegeta, Bagamoyo – Msata, Daraja la Kigamboni, Tazara flyover na Barabara ya Rangi Tatu – Gerezani zipo kwenye hatua mbalimbali za ujenzi. Wizara pia imenunua kivuko kitakachofanya kazi kati ya Dar es Salaam – Bagamoyo ambacho kitawasili nchini Juni, 2014. Pia hatua mbalimbali zinachukuliwa na Wizara yangu katika kupunguza misongamano katika miji ya Mwanza, Dodoma, Arusha, Iringa, Morogoro na Mbeya.

19.        Mheshimiwa Spika, miradi mingine iliyotekelezwa katika mwaka 2013/14 ni vivuko, nyumba na majengo ya Serikali ambayo utekelezaji wake umefafanuliwa katika Kitabu changu cha Hotuba ya Bajeti ukurasa 71 – 75 na utekelezaji wa miradi ya usalama barabarani na mazingira, masuala mtambuka pamoja na Utekelezaji wa Bodi na Taasisi zilizo chini ya Wizara umeonyeshwa katika ukurasa 75 -103.
20.        Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha kuanzia Januari – Aprili, 2014 nchi yetu ilikumbwa  na janga la mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa zilizonyesha katika mikoa yote.  Mafuriko hayo yalisababisha uharibifu wa miundombinu ya usafiri zikiwemo barabara na madaraja.  Mikoa 14 iliyokumbwa na mafuriko hayo ni pamoja na Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Mbeya, Ruvuma, Lindi, Mara, Tanga, Rukwa, Mtwara, Katavi, Dodoma, Iringa na Arusha.  Wizara kwa kupitia Wakala wa Barabara ilifanya juhudi za kukarabati na kuimarisha maeneo yaliyokumbwa na mafuriko hayo na hivi sasa yanapitika na wananchi wanapata huduma za usafiri kama kawaida.  Aidha, maeneo mengine yanaendelea kuboreshwa. Napenda kuwahakikishia Wananchi kuwa barabara zote zitakarabatiwa ili zirudi katika hali yake ya kawaida.

21.        Mheshimiwa Spika, Aidha katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara imeendelea na jitihada za kukabiliana na magari yanayozidisha uzito barabarani.  Athari za uzidishaji wa mizigo ni pamoja na uharibifu wa barabara ambazo zimejengwa kwa gharama kubwa.  Tatizo hili limeathiri kwa kiwango kikubwa barabara hapa nchini ikizingatiwa takribani asilimia 99.3 ya mizigo inayosafirishwa inatumia barabara.  Wizara imeendelea kuwaelimisha wasafirishaji pamoja na kufanya jitihada za kudhibiti mianya ya rushwa kwenye mizani.  Mizani ya kisasa inayopima uzito wa magari yakiwa kwenye mwendo  (Weigh-In-Motion) inaendelea kujengwa katika maeneo ya Vigwaza (Pwani), Mikese (Morogoro) na Nzuki (Singida).  Aidha, Watumishi wenye elimu za Shahada na Stashahada wameajiriwa kwenye mizani na kuboreshewa maslahi yao.  Watumishi 461 walifukuzwa kazi kwenye mizani kwa kukiuka maadili ya kazi kuanzia Agosti, 2012 hadi Aprili, 2014. Nawasihi Watumiaji wa Barabara hasa Wasafirishaji wazingatie Sheria Na. 30 ya Mwaka 1973 ili barabara zetu zidumu.  
C: MAKADIRIO YA  MPANGO NA BAJETI KWA MWAKA WA FEDHA 2014/15

22.        Mheshimiwa Spika, Wizara inatarajia kukusanya Shilingi 41,123,000.00. Bajeti ya Matumizi ya Kawaida ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2014/15, ni Shilingi 557,483,565,000.00. Kati ya fedha hizo, Shilingi 24,338,319,000.00 ni kwa ajili ya Mishahara ya Watumishi, Shilingi 6,944,846,000.00 ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo ya Wizara na Taasisi, na Shilingi 526,200,400,000.00 ni fedha za Mfuko wa Barabara.

23.        Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ujenzi imetengewa jumla ya Shilingi 662,234,027,000.00. kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Kati ya fedha hizo, Shilingi  450,000,000,000.00 ni fedha za ndani na Shilingi 212,234,027,000.00 ni fedha za nje. Mgawanyo wa fedha za maendeleo pamoja na miradi iliyotengewa fedha ni kama inavyooneshwa katika Kiambatisho Na.1.

MIRADI YA VIVUKO NA NYUMBA ZA SERIKALI

24.        Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa Maegesho ya Vivuko umetengewa Shilingi Milioni 5,990.00  kwa ajili ya  kazi za ujenzi wa maegesho ya kivuko cha Dar es Salaam – Bagamoyo pamoja na upanuzi wa sehemu ya Maegesho ya Kigamboni, Iramba – Majita,  Bukondo na Zumacheli, na maandalizi ya kuanzisha usafiri wa majini katika  mwambao wa ziwa Victoria ili kupunguza msongamano katika Jiji la Mwanza.

25.        Mheshimiwa Spika, Ununuzi wa Vivuko Vipya umetengewa Shilingi milioni 4,512.32 kwa ajili ya ununuzi wa kivuko kitakachofanya kazi kati ya Magogoni – Kigamboni, ununuzi wa mashine za kisasa za kukatia tiketi (ticket vending machines) kwa ajili ya vivuko vya Kisorya, Ilagala na Pangani na ununuzi wa vifaa vya karakana za TEMESA katika mikoa ya Manyara, Singida, Lindi, Mwanza, Kagera na Ruvuma.

26.        Mheshimiwa Spika, Ukarabati Wa Vivuko umetengewa Shilingi milioni 2,102.21 kwa ajili ya kukarabati vivuko vya MV Magogoni, MV Mwanza,  ‘Tug boat’ MV Kiu- Morogoro  na MV Pangani II- Tanga.

27.        Mheshimiwa Spika, Ujenzi na Ukarabati wa Nyumba na Majengo ya Serikali  umetengewa Shilingi milioni 2,689.46 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa nyumba ya makazi ya Mkuu wa Wilaya ya Urambo na ujenzi wa nyumba za Majaji  katika Mikoa ya Shinyanga (1), Kagera (1), Mtwara (1), Kilimanjaro (1) na Dar es Salaam (1), na ujenzi wa jengo la Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya  Bariadi (awamu ya nne). Aidha, kuendelea na ujenzi wa uzio na kuweka mfumo wa ulinzi katika nyumba za viongozi wa Serikali zilizopo Mikocheni, Kijitonyama na Msasani Peninsular, kufanyia matengenezo na ukarabati wa nyumba za viongozi wa Serikali.

28.        Mheshimiwa Spika, shughuli nyingine ni ukarabati wa Karakana za TEMESA katika Mikoa ya Mwanza, Arusha, Dar es Salaam, Dodoma na karakana za Vikosi vya Ujenzi.

MIRADI YA BARABARA NA MADARAJA

29.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Dar es Salaam – Chalinze – Morogoro (Km 200) sehemu ya Dar es Salaam – Chalinze (Km 100) zimetengwa Shilingi milioni 750.00. Shilingi milioni 250 kwa ajili ya kuendelea na maandalizi ya ujenzi kwa njia sita wa Awamu ya Kwanza ya mradi huo kiwango cha “Expressway” kwa ubia baina ya Serikali na Sekta Binafsi (Public Private Partnership – PPP). Aidha, Kiasi cha Shilingi milioni 500.00 zimetengwa kwa ajili ya kukarabati na kuimarisha (Backlog Maintenance) sehemu ya Mlandizi – Chalinze (km 44.24).

30.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Wazo Hill – Bagamoyo – Msata zimetengwa Shilingi Milioni 10,885.24. Shilingi milioni 10,441.10 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa barabara ya Bagamoyo – Msata (km 64). Shilingi milioni 444.14 kwa ajili ya kukamilisha usanifu wa kina kwa barabara ya Bagamoyo – Sadani – Tanga (km 178).

31.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Usagara – Geita – Kyamyorwa (km 422)   sehemu ya Uyovu – Biharamulo (km 112) zimetengwa shilingi milioni 9,800.00. Shilingi milioni 8,000.00 kwa ajili ya kuendelea na  ujenzi wa sehemu ya Uyovu – Biharamulo (km 112), kiasi cha Shilingi  milioni 800.00 kwa ajili ya ukarabati wa barabara ya Kyamyorwa –Buzirayombo (km120) na kiasi cha Shilingi milioni 1,000.00 kwa ajili ya malipo ya mwisho ya mkandarasi kwa sehemu ya Geita - Usagara (lot 1 na 2) (km 90).

32.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Kigoma – Kidahwe – Uvinza – Kaliua – Tabora (Km 430) zimetengwa shilingi milioni 36,596.34 ambapo Shilingi milioni 12,139.53 kwa ajili ya kuendelea na maungio ya barabara za Daraja la Kikwete katika Mto Malagalasi na Shilingi milioni 3,581.95 kwa ajili ya kulipa sehemu ya malipo ya mwisho ya mkandarasi wa barabara ya Kidahwe-Uvinza (km 76.6). 





33.        Mheshimiwa Spika, Shilingi milioni 6,837.80 kwa ajili ya kulipa sehemu ya malipo ya mwisho ya mkandarasi wa barabara ya Tabora - Ndono (km 42), Shilingi milioni 7,189.04 kuendelea na ujenzi sehemu ya Ndono -Urambo (km 52) na kiasi cha Shilingi milioni 4,848.02 kwa ajili ya sehemu ya Kaliua – Kazilambwa (km 56). Kwa upande wa barabara ya Uvinza – Malagarasi (km 51), Urambo – Kaliua (km 33) na Kazilambwa – Chagu (km 40) kiasi cha Shilingi milioni 2,000 zimetengwa.

34.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Marangu – Tarakea – Kamwanga/ Bomang’ombe – Sanya Juu (km 173), Arusha Moshi – Holili (km 140), Same – Himo – Marangu na Mombo – Lushoto (km 132), KIA – Mererani (km 26), Kwa Sadala – Masama – Machame Jct (km 15.5) na Kiboroloni – Kiharara – Tsudini – Kidia (km 10.80) zimetengwa jumla shilingi milioni 13,133.63.  

35.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Nangurukuru – Mbwemkulu (km 95) jumla ya Shilingi milioni 2,000.00 zimetengwa.

36.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Dodoma – Manyoni (km 127) jumla ya Shilingi milioni 1,309.28 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa barabara ya mchepuo kuingia Manyoni mjini (km 4.8) na kulipa sehemu ya malipo ya mwisho ya Mkandarasi.

37.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Mbwemkuru – Mingoyo (km 95) imetengewa kiasi cha Shilingi milioni 535.00.


38.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Nelson Mandela (km15.6) imetengewa Shilingi milioni 1,500.00 kwa ajili ya kulipa malipo ya mwisho ya mkandarasi. Aidha, kiasi cha Shilingi milioni 150.00 kimetengwa kwa ajili ya maandalizi ya upanuzi wa barabara ya Nelson Mandela sehemu ya Dar Port – TAZARA (km 6.0) kuwa njia sita.

39.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Dumila – Kilosa (km 78) imetengewa Shilingi milioni 8,000.00 kwa ajili ya kulipa madai ya Mkandarasi na kuendelea na ujenzi wa sehemu ya Rudewa-Kilosa (km 24).

40.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Sumbawanga – Matai -Kasanga Port (km. 112)  imetengewa kiasi cha Shilingi  milioni 10,241.37 kwa ajili ya kuendelea na kazi za ujenzi.

41.        Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa Madaraja ya Kirumi (Mara), Nangoo, Sibiti, Maligisu (Mwanza), Kilombero, Kavuu, Mbutu, Ruhekei, Ruhuhu (Ruvuma), Momba, Simiyu, Wami, Lukuledi II na  ununuzi wa Emergency Mabey Bridge Parts zimetengwa Shilingi milioni  25,500.00.

42.        Mheshimiwa Spika, barabara ya New Bagamoyo (Kawawa Jct – Tegeta km 17.1) zimetengwa Shilingi Milioni 14,500.00 wakati barabara ya Kyaka – Bugene (km 59.1) jumla ya Shilingi milioni 6,037.53 zimetengwa.

43.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Isaka – Lusahunga (km 242), Lusahunga – Rusumo na Nyakasanza – Kobero (km 150) zimetengwa Shilingi milioni 20,520.480. Aidha, barabara ya Manyoni - Itigi – Tabora (km 264) zimetengwa Shilingi milioni 21,499.57. Shilingi milioni 10,000.00 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi kwa sehemu ya Tabora – Nyahua na Shilingi milioni 10,299.57  kwa sehemu ya Manyoni – Itigi – Chaya. Kwa upande wa barabara ya Nyahua - Chaya (km 90) zimetengwa Shilingi milioni 1,200.00 ili kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami.

44.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Korogwe – Handeni (km 65) Shilingi milioni 6,356.73 zimetengwa na Barabara ya Handeni – Mkata (km 54) zimetengwa Shilingi Milioni 4,484.75 kwa ajili ya kulipa sehemu ya madai ya mkandarasi. 

45.        Mheshimiwa Spika, barabara za Mikoa zimetengewa Shilingi Milioni 31,915.27. Orodha ya miradi ya barabara za mikoa kwa kutumia fedha za Bajeti ya Maendeleo imeonyeshwa katika Kiambatisho Na. 2 kwenye kitabu changu cha Hotuba ya Bajeti.

46.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Mwandiga – Manyovu (km 60) imetengewa Shilingi milioni 500.00 na Daraja la Umoja limetengewa Shilingi milioni 500.00 kwa ajili ya kulipa sehemu ya malipo ya mwisho ya  mkandarasi. 

47.        Mheshimiwa Spika, barabara za Kuondoa Msongamano Dar es salaam (km 109.35) zimetengwa shilingi milioni 28,945.00. Kiasi cha Shilingi milioni 605.00 kwa ajili ya kukamilisha kazi zilizobakia kwa barabara ya Kawawa Roundabout - Msimbazi Valley – Jangwani/Twiga Jct. Shilingi milioni 1,290.00 kwa ajili ya kulipa sehemu ya madai ya mkandarasi wa barabara ya Jet Corner – Vituka - Devis Corner, Shilingi milioni 2,500.00 kwa ajili ya kuanza ujenzi barabara ya Ubungo – Maziwa – External na Tabata Dampo – Kigogo, Shilingi milioni 5,000.00 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara ya Kimara – Kilungule – External, Shilingi milioni 6,000.00 kwa ajili ya barabara ya Mbezi – Malambamawili – Kinyerezi – Banana, Shilingi milioni 5,000.00 kwa ajili ya barabara ya Tegeta – Kibaoni – Wazo Hill – Goba – Mbezi (Morogoro Road). Shilingi milioni 3,000.00 ni kwa ajili ya barabara ya Tangi Bovu – Goba,  Shilingi milioni 1,500.00 kwa ajili ya barabara ya Kimara Baruti – Msewe – Changanyikeni, Shilingi milioni 1,500.00 kwa ajili ya barabara ya Kibamba – Kisopwa, Shilingi milioni 1,000.00 kwa ajili ya barabara Banana – Kitunda – Kivule – Msongola (km 14.7) na Shilingi milioni 1,500.00 kwa ajili ya barabara ya Ardhi – Makongo. Aidha,  kiasi cha Shilingi milioni 50.00 zitatumika kufuatilia na kusimamia ujenzi wa miundombinu ya Mabasi Yaendayo Haraka (Bus Rapid Transit Infrastructure).   

48.        Mheshimiwa Spika, ujenzi wa flyovers Dar es Salaam na Barabara za maingilio zimetengewa Shilingi milioni 19,150.00 ambapo Shilingi milioni 16,000.00 ni kwa ajili ya kuanza ujenzi wa ‘Flyover’  ya TAZARA na  Shilingi milioni 3,000.00  kwa ajili ya maboresho ya makutano ya Chang'ombe, Ubungo, Uhasibu, KAMATA, Magomeni, Mwenge, Tabata/Mandela na Morocco. Kiasi cha Shilingi milioni 150.00 zitatumika kwa ajili ya maandalizi ya upanuzi wa barabara TAZARA – JNIA (km 6.0) kuwa njia sita.

49.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Ndundu - Somanga (km 60) imetengewa  Shilingi milioni  5,287.74 wakati barabara ya Kidatu – Ifakara – Lupilo – Malinyi – Londo – Lumecha/Songea (km 396) imetengewa Shilingi milioni 1,600.00 kwa ajili ya kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.




50.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Tabora – Ipole – Koga – Mpanda (km 351.40) imetengewa Shilingi milioni 7,260.00. Shilingi milioni 2,560.00 ni kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami  sehemu ya Mpanda – Koga – Ipole (km 261.40) na Shilingi milioni 4,700.00 kwa sehemu ya Tabora - Sikonge  - Ipole (km 90.00).

51.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Makutano – Natta – Mugumu/ Loliondo – Mto wa Mbu (km 452) zimetengwa Shilingi milioni 9,617.63 ambapo jumla ya Shilingi milioni  5,617.63 ni kwa ajili ya kuendelea na ujenzi kwa kiwango cha lami kwa sehemu ya Makutano -Sanzate (km 50) na Shilingi milioni  4,000.00   kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami sehemu ya Mto wa Mbu – Loliondo (km 213).

52.        Mheshimiwa Spika, barabara ya  Ibanda – Itungi/Kiwira Port (km 26) zimetengwa Shilingi milioni 1,000.00 kwa ajili ya kuendelea na ukarabati wa barabara ya Ibanda – Itungi/Kiwira Port sehemu ya Kajunjumele – Kiwira Port (km 5.6). 
53.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Nzega – Tabora (km 115) zimetengwa Shilingi milioni 13,169.34 ambapo Shilingi milioni 6,696.04 ni kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa sehemu ya Nzega – Puge na Shilingi milioni 6,473.30 kwa ajili ya sehemu ya Puge – Tabora.

54.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Sumbawanga – Mpanda – Uvinza (km 440.4) zimetengwa Shilingi milioni 28,858.72 ambapo Shilingi milioni 8,850.94 ni kwa ajili ya kuendelea na kazi ya ujenzi wa sehemu ya Sumbawanga-Kanazi, Shilingi milioni 8,850.94 kwa sehemu ya Kanazi-Kizi-Kibaoni na Shilingi milioni 6,617.63 kwa sehemu ya Kizi-Sitalike-Mpanda. Shilingi milioni 4,539.21 ni kwa ajili ya kuanza ujenzi wa sehemu ya Mpanda-Mishamo (km 100).

55.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Nyanguge – Musoma (km 183) na Mchepuo wa Usagara – Kisesa (km 17) zimetengwa Shilingi milioni 19,235.26 ambapo Shilingi milioni 2,500.00 zitatumika kuendelea na kazi ya ukarabati wa barabara ya Nyanguge – Simiyu/Mara Border (km 85.5), kiasi cha Shilingi 7,235.26 kwa ajili ya ukarabati wa sehemu ya Simiyu /Mara Border – Musoma (km 80). Kiasi cha Shilingi milioni 4,000.00 kwa sehemu ya barabara ya Kisesa – Usagara Bypass. Aidha, kiasi cha Shilingi milioni 4,500.00 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Nansio - Kisorya – Bunda - Nyamuswa sehemu ya Kisorya - Bunda (km 50) na Shilingi milioni 1,000.00 kwa ajili ya kuanza ujenzi sehemu  ya Nyamuswa - Bunda.


56.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Magole – Mziha (Magole – Turiani km 48.8) jumla ya Shilingi milioni 6,156.84 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi.

57.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Mwigumbi – Maswa – Bariadi – Lamadi (km 171.8) (Bariadi – Lamadi km 71.8) zimetengwa Shilingi Milioni 10,965.65. Shilingi milioni 6,465.65 kwa ajili ya barabara ya Bariadi – Lamadi (km 71.8) na  kiasi cha Shilingi milioni 4,500.00 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa  barabara ya Mwigumbi - Maswa - Bariadi (km 100). Zabuni zimetangazwa kwa sehemu ya Mwigumbi – Maswa.

58.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Tabora – Ipole – Rungwa (Ipole – Rungwa km 95) imetengewa Shilingi milioni 50.00. kwa ajili ya kukamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.

59.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Kidahwe – Kasulu – Kibondo - Nyakanazi (km 310) jumla ya Shilingi milioni 10,000.00 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa kilomita 100 za barabara ya Kidahwe – Kasulu – Kibondo – Nyakanazi (km 310) kwa kiwango cha lami. Mikataba ya ujenzi kwa sehemu ya Kidahwe – Kasulu (km 50) na Nyakanazi – Kibondo (km 50) imekwishasainiwa na makandarasi wako kwenye maeneo ya kazi (sites) kwa ajili ya ujenzi.

60.        Mheshimiwa Spika, barabara ya kuingia uwanja wa ndege wa Mafia (Mafia Airport Access Road km 14) jumla ya Shilingi milioni 2,471.17 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi kwa kiwango cha lami.

61.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Chuo Kikuu cha Dodoma (km 12) jumla ya Shilingi milioni 3,000.00 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi kwa kiwango cha lami.

62.        Mheshimiwa Spika, daraja la Kigamboni na barabara za maingilio ya kwenye daraja zimetengwa Shilingi milioni 7,451.56 ambapo Shilingi milioni 4,951.56 ni kwa ajili ya kuendelea na kazi ya ujenzi wa daraja, na Shilingi milioni 2,500.00 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara ya maingilio ya  Mjimwema – Vijibweni (km 10).

63.        Mheshimiwa Spika, ujenzi wa njia za magari mazito na maegesho ya dharura kwa ajili ya kuimarisha barabara katika ukanda wa kati Shilingi milioni 200.00 zimetengwa.

64.        Mheshimiwa Spika, barabara ya PUGU sehemu ya JNIA – Pugu (km 8.0) jumla ya Shilingi milioni 150.00 zimetengwa kwa ajili ya kuanza usanifu ili kuipanua kuwa njia sita.   
65.        Mheshimiwa Spika, kuipanua barabara ya Kimara – Kibaha  ikijumuisha madaraja ya Kibamba, Kiluvya na Mpiji jumla ya Shilingi milioni 250.00 zimetengwa kwa ajili ya kuanza usanifu.

66.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Kisarawe – Mlandizi (km 52) jumla ya Shilingi milioni 400.00 zimetengwa kwa ajili ya kuanza usanifu wa kujenga kwa kwa kiwango cha lami. Aidha, upanuzi wa barabara ya Bandari (km 1.2), ujenzi wa barabara ya Dockyard (km 0.7) na Mivinjeni (km 1.0) jumla ya Shilingi milioni 50.00 zimetengwa kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi.

67.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Pugu – Kifuru – Mbezi Mwisho – Mpiji Magoe – Bunju (km 34) kuwa njia tatu Shilingi milioni 1000.00 zimetengwa ambapo jumla ya Shilingi milioni 500.00 ni kwa ajili ya kuanza usanifu wa sehemu ya Pugu – Kifuru – Mbezi Mwisho (km 12.7) na Shilingi milioni 500.00 ni kwa ajili ya kuanza usanifu wa sehemu ya Mbezi Mwisho – Magoe Mpiji – Bunju (km 21.3).

68.        Mheshimiwa Spika, kujenga mizani mipya karibu na bandari ya Dar es Salaam Shilingi milioni 100.00 zimetengwa kwa ajili ya maandalizi ya usanifu. Aidha, barabara ya Tunduma – Sumbawanga (km 224.81) Shilingi milioni 1,057.88 zimetengwa ambapo Shilingi milioni 57.88 ni kwa ajili ya kuhamisha miundombinu katika eneo la Tunduma – Sumbawanga na kiasi cha Shilingi milioni 1,000.00 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa sehemu ya Tunduma mjini (km 1.6).



69.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Kagoma – Lusahunga (km 154) Shilingi milioni 9,600.00 zimetengwa kulipa sehemu ya madai ya mkandarasi wakati barabara ya Arusha – Namanga (km 105) imetengewa Shilingi milioni 4,517.12.

70.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Singida – Babati – Minjingu – Arusha (km 321.5) imetengewa shilingi milioni 10,444.83 kwa ajili ya kuendelea na  ukarabati wa barabara ya Minjingu hadi Arusha yenye urefu wa kilomita 98 na barabara ya Dar es salaam – Mbagala (Kilwa Road) – Gerezani (sehemu ya Kamata – Bendera Tatu km 1.5) imetengewa Shilingi milioni 8,000.00 kwa ajili ya  kukamilisha ulipaji fidia na kuanza ujenzi wa sehemu ya  KAMATA – Bendera Tatu (km 1.5). 

71.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Msimba – Ruaha/Ikokoto Mafinga (km 517.40) zimetengwa Shilingi milioni 43,284.28 ambapo Shilingi milioni 4,016.513  ni kwa ajili ya kulipa sehemu ya madai ya mkandarasi barabara ya Iringa – Mafinga (Km 68.9); Shilingi milioni 34,844.527  kwa ajili ya ukarabati wa barabara ya Mafinga-Igawa yenye urefu wa kilometa 137.9. Aidha, Shilingi milioni 500 kwa ajili ya kufanya maandalizi ya ujenzi wa  barabara ya Igawa-Madibira-Mafinga, Shilingi milioni 2,823.24 kwa ajili ya ujenzi wa Njombe-Ndulamo-Makete, na Shilingi milioni 1,000.00 kwa ajili ya ujenzi wa Njombe-Lupembe-Madeke. 






72.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Korogwe - Mkumbara –Same (km 172) imetengewa shilingi milioni 15,200.00.

73.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Mbeya - Makongolosi (km 115) shilingi milioni 13,340.12 ambapo Shilingi milioni 6,528.78 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi kwa sehemu ya Mbeya-Lwanjilo; Shilingi milioni 5,008.00 kwa sehemu ya Lwanjilo-Chunya na Shilingi milioni 1,495.50 kwa sehemu ya Chunya – Makongolosi. Aidha, Shilingi milioni 307.84  kumalizia deni la Mhandisi Mshauri aliyefanya kazi ya usanifu wa kina wa sehemu ya Makongolosi – Rungwa – Itigi – Mkiwa. 

74.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Chalinze – Segera – Tanga (km 248) zimetengwa shilingi milioni 3,500.00 ambapo Shilingi milioni 2,500.00  kwa ajili ya kulipa sehemu ya madai ya mkandarasi wa sehemu ya Kitumbi-Segera-Tanga. Aidha, Shilingi milioni 1,000.00 ni kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa barabara ya Msoga – Msolwa (Chalinze Bypass).

75.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Itoni – Ludewa – Manda (km 211) jumla ya Shilingi milioni 4,400.00 zimetengwa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa sehemu ya kilometa 50 za barabara ya Itoni – Ludewa – Manda.

76.        Mheshimiwa Spika, Daraja la Ruvu Chini kwenye barabara ya Bagamoyo – Msata Shilingi milioni 700.00 zimetengwa.
 




77.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Dodoma – Mtera – Iringa (km 260) imetengewa Shilingi milioni 21,739.31 na barabara ya Dodoma – Kondoa – Babati (km 261) zimetengwa Shilingi milioni 28,392.41.

78.        Mheshimiwa Spika, barabara ya Masasi- Songea – Mbamba Bay (km 659.7) zimetengwa Shilingi milioni 68,383.08 ambapo Shilingi milioni 10,533.88 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi Mangaka-Nakapanya; Shilingi milioni 10,532.57 kwa Nakapanya – Tunduru;  Shilingi milioni 10,532.93 kwa sehemu ya Mangaka-Mtambaswala; na Shilingi milioni 10,567.32 kwa Tunduru-Matemanga; Shilingi milioni 10,679.20 kwa Matemanga-Kilimasera; Shilingi milioni 10,679.18 kwa Kilimasera – Namtumbo. Aidha, fedha kwa ajili ya gharama za usimamizi na ufuatiliaji wa mradi katika kipindi cha uangalizi ni Shilingi milioni 17.00 kwa barabara ya Songea – Namtumbo na Shilingi milioni 17.00 kwa barabara ya  Peramiho – Mbinga. Shilingi milioni 2,324.00 ni kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami sehemu ya Mbinga-Mbamba Bay, na Shilingi milioni 2,500.00 kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi wa  barabara ya Masasi - Newala – Mtwara.

79.        Mheshimiwa Spika, Ujenzi Makao Makuu ya Wakala wa Barabara pamoja ujenzi wa Ofisi za mikoa ya Dar es Salaam, Katavi, Geita, Simiyu, Njombe na Lindi, jumla ya Shilingi milioni 2,934.35 zimetengwa kwa ajili ya kuanza kazi ya ujenzi.

80.        Mheshimiwa Spika, barabara ya kuingia kwenye Chuo cha Uongozi pamoja na barabara zilizoko ndani ya Chuo hicho jumla ya Shilingi milioni 1,500.00 zimetengwa kwa ajili ya kuanza maandalizi.

81.        Mheshimiwa Spika, mradi wa Usalama Barabarani zimetengwa Shilingi milioni 4,899.00; Usalama, Mazingira na Marekebisho ya Mfumo - Shilingi milioni 720.00; Menejimenti na Utunzaji wa Mazingira  – Shilingi milioni 502.34 ambapo mchanganuo wa miradi yote hii na kazi zitakazofanyika zimeainishwa katika Kitabu cha Hotuba yangu Ukurasa 155 - 158.

FEDHA ZA MFUKO WA BARABARA KWA MWAKA WA FEDHA 2014/15

82.               Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2014/15, Mfuko wa Barabara unatarajiwa kukusanya jumla ya Shilingi 751,700,000,000.00. Mchanganuo wa fedha za Mfuko wa Barabara zilizotengwa kwa ajili ya Wizara ya Ujenzi umeonyeshwa katika Kiambatanisho Na. 3.

83.               Mheshimiwa Spika, maelezo ya miradi ya barabara na shughuli zingine zinazotekelezwa kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara kwa mwaka wa fedha 2014/15 yameainishwa kwenye Kitabu cha Hotuba ya Bajeti ukurasa 159 - 175. Aidha, fedha  za matengenezo ya barabara kuu na barabara za mikoa kwa mwaka wa fedha 2014/15 kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara ni jumla ya Shilingi 469,494,900,00.00. Mchanganuo wa mpango huo wa matengenezo umefafanuliwa katika ukurasa 175 - 179 na katika Viambatisho Na. 5A hadi 5E katika Kitabu cha Hotuba ya Bajeti.





MPANGO WA UTEKELEZAJI KAZI KATIKA TAASISI ZILIZO CHINI YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2014/15
 
84.               Mheshimiwa Spika, shughuli zitakazofanywa na Wakala wa Barabara (TANROADS), Wakala wa Majengo ya Serikali (TBA), Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) na Bodi ya Mfuko wa Barabara  zimefafanuliwa katika Kitabu cha Hotuba ya Bajeti Ukurasa 179 - 183.

85.               Mheshimiwa Spika, Bodi ya Usajili wa Wahandisi imepanga kusajili Wahandisi 800, Mafundi Sanifu 200 na Kampuni za Ushauri wa Kihandisi 25. Bodi pia itasimamia mpango wa mafunzo kwa vitendo kwa wahandisi wahitimu 692 ambapo wahandisi wahitimu 442 ni wanaoendelea na 250 watakuwa wapya. Vile vile bodi itaendelea kuwaapisha wahandisi wataalamu na wahandisi washauri wote waliosajiliwa na wanaoendelea kusajiliwa ili kuhakikisha kuwa wahandisi wanatekeleza majukumu yao kwa weledi na kuzingatia sheria. Hivyo Waheshimiwa Wabunge wenye fani ya uhandisi mnaombwa mjitokeze kwa ajili ya viapo hivyo muhimu katika fani ya uhandisi.

86.               Mheshimiwa Spika,  Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi inatarajia kusajili  Wabunifu Majengo 25, Wakadiriaji Majenzi  35, Kampuni 24 za Wabunifu Majengo na 10 za Wakadiriaji Majenzi. Aidha, Bodi itaendelea kukagua shughuli za wataalamu hao kwenye miradi iliyopo nchini inayostahili kukaguliwa kwa mujibu wa sheria. 

87.               Mheshimiwa Spika, Bodi ya Usajili wa Makandarasi imepanga kusajili jumla ya Makandarasi 834 wa fani mbalimbali  pamoja na kukagua miradi ya ujenzi 2,500.   Aidha, Bodi itaendesha kozi tano za mafunzo kwa makandarasi katika mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Mara, Rukwa na Dodoma. Bodi pia itaendeleza Mfuko Maalum wa Kutoa Dhamana ya Kusaidia Makandarasi Wadogo na wa Kati (Contractors Assistance Fund), jitihada za kuhamasisha makandarasi wazalendo kujiunga ili kuomba zabuni kwa mfumo wa ubia na mkutano wa mafunzo ya utekelezaji wa miradi kwa ubia kwa makandarasi wa Kanda ya Kusini utafanyika mjini Iringa.

88.               Mheshimiwa Spika, shughuli za Taasisi nyingine chini ya Wizara yangu kama vile Baraza la Taifa la Ujenzi, Vikosi vya Ujenzi, Chuo cha Ujenzi  Morogoro, Chuo cha Matumizi ya Teknolojia Stahiki ya Nguvukazi (Appropriate Technology Training Institute – ATTI) cha Mbeya, Kituo cha Usambazaji wa Teknolojia Katika Sekta ya Uchukuzi (Tanzania Transportation Technology Transfer Centre) na Masuala Mtambuka ya Maendeleo ya Rasilimali Watu, Habari, Elimu na Mawasiliano, Ushirikishwaji wa Wanawake Katika Kazi za Barabara Nchini, Mikakati ya Kupambana na UKIMWI, Kudhibiti Rushwa na Mapitio ya Sera ya Ujenzi zimeainishwa katika Kitabu cha Hotuba ya Bajeti ukurasa 186 - 192

SHUKURANI 

89.        Mheshimiwa Spika,  kwa niaba ya Wizara ya Ujenzi, napenda kuwashukuru kwa dhati wale wote walioshirikiana nasi katika kipindi cha mwaka wa fedha 2013/14 katika kutimiza malengo yetu. Shukrani za pekee ziwaendee Washirika wa Maendeleo walioendelea kushirikiana nasi katika kutekeleza programu na mipango yetu katika kuendeleza Sekta ya Ujenzi. Washirika hao ni pamoja na Abu Dhabi, Denmark (DANIDA), Japan (JICA), Korea, Marekani (MCC), Uingereza (DFID), Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB), Benki ya Dunia (WB), Benki ya Kiarabu ya Maendeleo ya Afrika (BADEA), Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya Nchi za Ulaya (EU), Shirika la Maendeleo la Marekani (USAID), Kuwait Fund, SIDA na OPEC Fund.

90.        Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowashukuru viongozi wenzangu katika Wizara nikianzia na Mhe. Eng. Gerson H. Lwenge (Mb.), Naibu Waziri; Eng. Mussa I. Iyombe, Katibu Mkuu  na Eng. Joseph M. Nyamhanga, Naibu Katibu Mkuu na Wakurugenzi. Aidha, ninawashukuru Wenyeviti wa Bodi na Watendaji Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara, Wakuu wa Vitengo pamoja na wafanyakazi wote wa Wizara ya Ujenzi na Taasisi zake, kwa kujituma na kujitolea kwa juhudi na maarifa katika kutekeleza malengo  na majukumu ya Wizara yetu.

91.        Mheshimiwa Spika, tunawashukuru wadau wote wa sekta ya ujenzi, na hasa sekta binafsi, ambao wametupa ushirikiano wa kutosha katika kuendeleza sekta hii. Aidha, nachukua fursa hii kuvipongeza vyombo mbalimbali vya habari kwa ushirikiano wao na jinsi ambavyo vimekuwa vikifuatilia na kutoa taarifa za shughuli zinazohusiana na malengo, sera, sheria na kanuni mbalimbali zinazosimamiwa na Wizara ya Ujenzi. Shukrani zangu za dhati pia nazitoa kwa Mpigachapa Mkuu wa Serikali na Wafanyakazi wote wa Ofisi ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali kwa kuchapa hotuba hii.

92.        Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee nawashukuru wapiga kura wangu wa Jimbo la Uchaguzi la Chato kwa ushirikiano wanaonipatia na uvumilivu wao kipindi chote ninapotekeleza majukumu ya Kitaifa.

93.        Mheshimiwa Spika, hotuba yangu hii inapatikana katika tovuti ya Wizara ya Ujenzi - (www.mow.go.tz).

MAOMBI YA FEDHA KATIKA MWAKA WA FEDHA 2014/15

94.        Mheshimiwa Spika,  ili Wizara iweze kutekeleza majukumu yake ya kuendeleza sekta ya ujenzi, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu liidhinishe jumla ya Shilingi 1,219,717,592,000.00 kwa  ajili ya matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2014/15. Kati ya fedha hizo, Shilingi 557,483,565,000.00 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida ambazo zinajumuisha Shilingi 24,338,319,000.00 za mishahara ya Watumishi (PE), Shilingi 6,944,846,000.00 za matumizi mengineyo (OC) na Shilingi 526,200,400,000.00 za Mfuko wa Barabara.

Bajeti ya  Miradi ya Maendeleo  ni Shilingi 662,234,027,000.00.  Kati ya fedha hizo, Shilingi 450,000,000,000.00 ni fedha za ndani na Shilingi 212,234,027,000.00 ni fedha za nje.
95.        Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.


No comments: