Wabunge
wameendelea kupigia debe maslahi mazuri sanjari na mazingira bora ya kufanyia
kazi kwa kutaka pamoja na masuala mengine, serikali iangalie uwezekano wa
kumpatia kila mbunge ofisi ya kufanyia kazi awapo Dodoma.
Ushauri huo
umetolewa jana mjini hapa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria
na Utawala kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa
fedha 2013/14 pamoja na maoni ya kamati kuhusu makadirio na matumizi kwa mwaka
wa fedha 2014/15.
Mjumbe wa kamati
hiyo, Fakharia Shomar katika taarifa ya kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa
Sengerema, William Ngeleja, alisema kamati inapongeza Ofisi ya Spika pamoja na
Tume ya Utumishi wa Bunge kwa kuendelea kutoa ushauri na mapendekezo kwa Rais
ya kuboresha maslahi ya wabunge na watumishi wa bunge.
Alisema ili
kuhakikisha bunge linatekeleza majukumu yake ipasavyo, wabunge wote wapatiwe
ofisi za kufanyia kazi wanapokuwepo Dodoma ili kuwawezesha kutekeleza majukumu
yao kwa umakini na ufanisi.
Wakati ofisi ya
Bunge imeingia mkataba na kampuni ya bima ya Jubilee kutoa matibabu kwa wabunge
na familia zao, kamati imeshauri kampuni hiyo ielekezwe itoe elimu kwao kuhusu
utaratibu wa utoaji huduma, aina ya matibabu na hospitali zinazohusika na mkataba
huo na zinakopatikana.
Kwa mujibu wa
taarifa hiyo ya kamati, ofisi ya Bunge imeingia mkataba na Mfuko wa Hifadhi ya
Jamii (NSSF) kujenga ofisi 178 za wabunge katika majimbo ambayo hayana ofisi.
Wabunge kupitia
kamati hiyo, pia wameshauri ofisi ya bunge ihakikishe inaingia mikataba na
benki zinazotoa mikopo yenye bima kuepusha usumbufu unaoweza kujitokeza
kutokana na deni la mkopo huo kwa familia za wabunge endapo watapoteza maisha
kwa namna moja au nyingine.
Kamati imekuja
na ushauri huo wakati kwenye bajeti ya 2014/15 ikiwa, kati ya Sh
224,932,198,000 zilizotengwa kwa ajili ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake,
zaidi ya nusu ni za mfuko wa bunge.
Taasisi nyingine
ni Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa iliyotengewa Sh 20,732,781,000 na
Tume ya Taifa ya Uchaguzi ni Sh 4,371,895,000.
Mfuko wa Bunge
umeomba jumla ya Sh 123,941,455,000 ambazo kati yake, Sh 15,520,327,000
zinaombwa kwa ajili ya mishahara ya wabunge na watumishi, Sh 108,421,128,000
zitatumika kuendesha mikutano ya Bunge na Kamati pamoja na shughuli zingine za
kiutawala.
No comments:
Post a Comment