Meya wa Jiji la
Dar es Salaam, Dk Didas Massaburi amesema abiria watakaokutwa wakiwa wamepanda
pikipiki (bodaboda) katika maeneo ambayo pikipiki hizo hazina leseni ya kufanya
biashara, watakamatwa na kufikishwa mahakamani pamoja na dereva.
Alisema pia
wafanyabiashara ndogo, watakaokutwa wakifanya biashara katika maeneo
yasiyoruhusiwa kisheria, ikiwemo maeneo ambayo yamefanyiwa usafi na Halmashauri
ya Jiji la Dar es Salaam hivi karibuni, watakamatwa na kufikishwa mahakamani.
Alisema hayo
mjini Tanga jana, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, ambao walitaka
kufahamu msimamo wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT), kuhusu
kunyanyaswa kwa waendesha bodaboda katika maeneo mbalimbali nchini.
Dk Massaburi
mbaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa ALAT, alisema Jumuiya hiyo imekuwa bega kwa
bega na kuwaunga mkono waendesha bodaboda nchini, pale wanapofanya biashara zao
kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa.
Alisema zaidi ya
kuwaunga mkono serikali za mitaa, zimekuwa pia zikiwawezesha vijana kwa kuwapa mikopo na kuwapa nyenzo
mbalimbali, zikiwemo bodaboda zenyewe
ili kukabiliana na maisha, hatua inayoonesha kuwa si kweli kwamba
serikali haiwapi umuhimu waendesha bodaboda.
Akizungumzia
agizo la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam la kuwazuia waendesha bodaboda na
wafanyabiashara ndogo, kufanya biashara katika maeneo yasiyoruhusiwa kisheria,
ikiwemo kuingia katikati ya Jiji, Dk Massaburi alisisitiza kuwa agizo hilo liko
pale pale, kwa vile lipo kisheria.
Alisema ili
kuonesha kuwa Halmashauri ya Jiji inatilia mkazo agizo hilo, kuanzia sasa
abiria atakayekutwa akiwa amepanda pikipiki katika eneo ambalo haina leseni ya
kufanya biashara hiyo, atakamatwa sambamba na dereva na kufikishwa mahakamani
mara moja.
Alisema hatua
kama hizo pia zitachukuliwa kwa wafanyabiashara watakaokutwa wakifanya biashara
katika maeneo yasiyoruhusiwa kisheria yakiwemo yale yaliyovunjwa na Jiji hivi karibuni katika
operesheni ya kusafisha Jiji la Dar es Salaam.
Alisema kampeni
hiyo haina maana kwamba Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam haina mpango wa
kuwaendeleza wafanyabiashara ndogo kama inavyopotoshwa, kwani ipo mipango
kabambe ya kuboresha biashara ndogo katika Jiji hilo kwa kujenga maeneo maalumu na ya kisasa ya kufanyia biashara hizo.
“Upo mpango wa
uboreshaji wa maeneo ya biashara katika Jiji la Dar es Salaam unaofadhiliwa na
Benki ya Dunia ambapo karibu dola milioni 100 zimetengwa kwa mradi huu.
“Huu ni
uthibitisho wa Jiji kuelewa umuhimu wa kuwa na maeneo maalumu ya kufanyia
biashara, na si kuruhusu biashara holela zinazoashiria ukiukwaji mkubwa wa sheria. Tutasimama kidete kusimamia sheria
zilizotungwa na Bunge,” alisema Dk Massaburi.
Kauli hiyo ya Dk
Massaburi imekuja wakati Umoja wa Wabunge wa Jiji la Dar es Salaam chini ya
Mbunge wa Temeke, Abbas Mtemvu kusema kuwa unajiandaa kutoa shinikizo la kuzuia
kuendelea kwa kampeni hiyo ya usafi jijini Dar es Salaam kwa madai kuwa
inawaonea na kuwakandamiza wananchi wa kipato cha chini wakiwemo waendesha bodaboda.
Wabunge hao
wamekuwa wakimrushia lawama za moja kwa moja Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,
Saidi Meck Sadiki na Meya Massaburi kuwa
ndio vinara wa unyanyasaji huo, lakini viongozi hao wamekuwa wakipuuza
madai hayo kwa maelezo kuwa wanasimamia
sheria zilizotungwa na wabunge wenyewe.
No comments:
Post a Comment