Mamlaka ya
Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imesema imewekeza zaidi ya dola milioni 500
na kupata mikopo yenye riba nafuu kutoka Benki ya Dunia na nchi mbalimbali za
Ulaya katika kuendeleza miundombinu na manunuzi ya vifaa mbalimbali.
Kaimu Meneja
Mawasiliano wa TPA, Janeth Ruzangi alisema hayo Dar es Salaam na
kuyataja maeneo ya uendelezwaji kuwa ni pamoja na magati na maeneo ya kuhifadhi
mizigo, vifaa vya kupakia na kupakua, vifaa vya majini na majengo.
Alisema chini ya
uendelezaji miundombinu pia bandari imeongeza vifaa vya kuhudumia mizigo,
sambamba na mabadiliko ya mfumo mzima wa mabadiliko ya ubebaji mizigo, usalama
wa Bandari, pamoja na vifaa vya doria kuimarishwa.
Vilevile alisema
matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yameongezeka katika
shughuli za bandari na hivyo kuongeza tija na ufanisi.
Alisema Bandari
ya Dar es Salaam ni kubwa kuliko zote
ikiwa na urefu wa kilomita 2.6 na upana wa mita 500 na ina uwezo wa kuhudumia
tani milioni 10.1.
“Bandari ina
magati 11, gati Na. 1 - 7 linahudumia shehena mchanganyiko na linaendeshwa na
Mamlaka na Gati Na. 8 - 11 yanahudumia shehena ya kontena na yana uwezo wa
kuhudumia kontena 330,000 kwa mwaka,” alisema.
Alivitaja
vitengo vingine ni pamoja na kituo cha kuhudumia mafuta, kituo cha nafaka na karakana ndogo ya kukarabati meli, Mashedi
10 ya mizigo, Kitengo cha kuhudumia meli za mwambao na Kitengo cha Nafaka chenye uwezo wa kuhifadhi
tani 30,000.
Alisema kabla ya
Uhuru, lango lilikuwa na uwezo wa kuingiza meli zenye urefu wa mita 145 hadi
175 na kina cha maji cha mita saba.
Upanuzi wa lango
ulifanyika mwaka 1998 ambapo kina kilichimbwa hadi kufikia mita 10.5 na upana
wa mita 140 kwa gharama ya Dola za Marekani 240 milioni.
Hata hivyo
alisema hivi sasa lango linaruhusu meli zenye ukubwa usiozidi mita 234.
Kutokana na
utekelezaji wa mradi wa kupanua na uwekaji wa taa katika lango kuu, pamoja na
uchimbaji ndani ya Bandari mwaka 1998, meli zinaweza kuingia usiku na mchana,
ukubwa wa meli umeongezeka hadi kufikia urefu wa mita 234/240 na kina cha maji
kimeongezeka hadi kufikia mita 10.5.
No comments:
Post a Comment