Mradi mkubwa wa
kupima viwanja katika ufukwe mjini Lindi unadaiwa kugubikwa na utata,
hali ambayo Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
imeingilia kati na kutaka mchakato huo usitishwe kwa muda.
Mwenyekiti wa
kamati hiyo, Dk Hamisi Kigwangala alisema jana bungeni mradi huo unaoendeshwa
na Taasisi ya Utility Trust of Tanzania (UTT), wananchi wamenyang’anywa maeneo
yao ya asili bila ridhaa yao, kuyapima na kuyauza kwa ujanja ujanja.
Dk Kigwangala
alikuwa akiwasilisha taarifa ya kamati kuhusu utekelezaji wa majukumu ya ofisi
ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa mwaka wa fedha 2014/15
pamoja na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha ujao.
Kwa mujibu wa
Kigwangala, mwananchi mwenye ekari 20 za ufukweni amejikuta akipewa fidia kwa
ekari nne na nyingine kuandikishwa majina ya watu wasiojulikana.
“Mheshimiwa
spika, kamati imesikitishwa na hili na imeazimia kuitaka Serikali kuwasilisha
ndani ya wiki moja taarifa ya namna ilivyolishughulikia jambo hili na hatua
ilizochukua dhidi ya udhalimu huu mkubwa kwa wananchi,” alisema.
Aliendelea
kusema, “sambamba na hilo, kamati imeiagiza serikali isitishe zoezi hili kwa
muda mpaka ukweli wa namna jambo hili lilivyotekelezwa utakapopatikana.”
Hata hivyo,
Kigwangala alisema kamati imefurahishwa hatua za awali na za haraka
zilizochukuliwa na serikali kutii agizo la kamati.
Kamati hiyo ya
bunge kupitia kwa mwenyekiti wake, ilisisitiza, “tusikubali kuvunja misingi
imara ya taifa letu kwa kuukubali ubepari na ubeberu kuingia nchini, na hadi
kwa wananchi wetu huko vijijini bila kuweka mifumo ya kulinda maslahi yao na
kuyasimamia ilhali tunaujua uwezo wao kielimu, kiuchumi na kisheria kuwa ni
mdogo.”
No comments:
Post a Comment