Vyama vya msingi vya wakulima wa zao
la tumbaku wilayani Kahama mkoani Shinyanga, vimetakiwa kushirikiana na taasisi
za kifedha zikiwemo benki ili waweze kupata mikopo kwa haraka, itakayokuza
mitaji yao ya biashara kurejesha kwa wakati uliopangwa.
Meneja Uhusiano wa Benki ya
CRDB Kanda ya Ziwa Kitengo ya asasi ndogondogo za kifedha, Raymond Urassa
alitoa mwito huo wakati akitoa msaada wa mifuko100 ya saruji, yenye
thamani ya Sh milioni mbili kwa Chama cha Msingi cha Tumbaku cha Kangeme Kaya
ya Ulowa.
Msaada huo una lengo ya kujenga wadi
ya wazazi na wajawazito katika kata hiyo.
Urassa alisema benki ya CRDB kwa
sasa imeanza kushirikiana na vyama vya msingi, hasa vile vya wakulima wa
tumbaku, lengo likiwa ni kurudisha kiasi
kidogo cha sehemu ya faida wanayopata
kwa ajili ya shughuli za kijamii kwa wananchi.
Alisema kuwa ili vyama vya msingi
viweze kuendelea, lazima wakulima washirikiane na kuonesha umoja wao, hasa
wakati wa kurudisha madeni ya pembejeo wanazokopa katika taasisi mbalimbali za
fedha, hususani katika benki.
Pia, Meneja huyo aliwataka wakulima
kuhakikisha wanakuwa mstari wa mbele kudhibiti wale ambao wamekuwa wakitorosha
pembejeo ili kukimbia madeni, waliokopeshwa na vyama vya msingi katika eneo
husika.
Mgeni rasmi katika makabidhiano
hayo, kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Ushetu, John Duttu alisema
kuwa msaada huo umekuja wakati muafaka.
Alisema kutokana na msaada huo,
wananchi wa eneo hilo hawana budi kujenga kwa nguvu zao hadi kufikia lenta na
Halmashauri ya Wilaya itamalizia kwa kuezeka jengo hilo.
Kwa upande
wake, Diwani wa Kata ya Ulowa, Paschal Mayengo alisema msaada uliotolewa na
benki ya CRDB utakuza uhusiano mzuri na wakazi wa kata hiyo na kukamilika kwa
wadi hiyo, kutanufaisha wakazi 25,000 wa eneo hilo.
No comments:
Post a Comment