Upelelezi wa kesi ya
mauaji ya watu 27 yaliyotokea baada ya jengo la ghorofa 16 kuporomoka,
inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Gabriel Fuime na
wenzake 11, haujakamilika.
Wakili wa Serikali,
Bernald Kongolo alidai hayo jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakati
kesi hiyo ilipotajwa.
Hakimu Mkazi wa Mahakama
hiyo, Devotha Kisoka aliahirisha kesi hiyo hadi Juni 9 mwaka huu itakapotajwa
tena kuangalia kama upelelezi umekamilika. Wakati huo washitakiwa wote
wanaendelea kubaki rumande kwa kuwa mashitaka yao hayana dhamana.
Mbali na Fuime
washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Mfanyabiashara Laza Radha, Diwani
katika Manispaa ya Kinondoni, Ibrahim Mohamed (59), watendaji katika Manispaa ya
Ilala akiwemo Mhandisi Mkuu, Charles Ogare (48), Mhandisi Majengo, Godluck
Sylivester (35) na Mkurugenzi Mkuu wa Ukaguzi wa Majengo, Willibrod Mugyabuso
(42).
Wengine ni Mhandisi,
Mohamed Abdulkarim (61), Mhandisi Mshauri, Zonazea Oushoshaodaga Hema (59),
Msajili Msaidizi AQRB, Albert Mnuo na Ofisa Mkuu Mtekelezaji OQRB, Joseph Ringo
(60), Mkadiriaji Ujenzi, Vedasto Ruhale (59) na Msanifu Majengo, Michael
Hema.
Inadaiwa kuwa Machi 29
mwaka jana, katika mtaa wa India Gandhi Ilala, Dar es Salaam kwa makusudi
washitakiwa waliwaua watu 27.
Hivi karibuni Fuime
aliiomba Mahakama imfutie mashitaka ya mauaji, lakini Hakimu Kisoka alisema
hawezi kutoa uamuzi kwa kuwa jalada la kesi lipo Mahakama Kuu.
Awali, washitakiwa hao
isipokuwa Fuime walikabiliwa na mashitaka ya kuua watu 24 bila kukusudia.
Baadaye walibadilishiwa mashitaka na kuwa ya kuua kwa kukusudia na kuunganishwa
na mkurugenzi huyo.
No comments:
Post a Comment