Serikali inatarajia
kuweka katika mtaala wa elimu unaotumika sasa, somo la afya ya uzazi kwa vijana
katika shule za msingi na sekondari nchini kupunguza mimba za utotoni na
maambukizi ya Ukimwi.
Hayo yalisemwa jana, Dar
es Salaam na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Jenista Mhagama katika
ufunguzi wa mkutano wa siku tatu kuhusu afya ya uzazi kwa vijana
uliozishirikisha nchi 16.
Mhagama alisema serikali
imeweka mikakati ya kuanzisha elimu hiyo ya afya ya uzazi na jinsia kwa vijana
katika shule za msingi kutokana na ukubwa wa tatizo la mimba za utotoni na
maambukizi ya Ukimwi.
“Serikali inawahakikishia
wanasayansi kuwa elimu hiyo itawapa matokeo chanya kwamba hakutakuwa na
maambukizi wala mimba za utotoni kwa vijana hao,’’ alisema Mhagama katika
hotuba yake ilisomwa kwa niaba yake na Mkurugenzi Msaidizi wa masuala mtambuka
katika wizara hiyo, Letisia Sayi.
Mhagama alisema elimu ya
afya ya uzazi kwa vijana itasaidia kubadili tabia, kujikinga kwa kutumia
kondomu na wanaoishi na maambukizi kulinda afya zao.
Naye, Mtaalamu wa kitaifa
wa masuala ya Ukimwi na elimu ya afya wa Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni
(UNESCO), Martin Herman alisema takwimu za wizara hiyo zinaonesha wanafunzi
6000 kila mwaka wanaacha shule kwa sababu ya mimba za utotoni.
Herman alisema mpango huo
wa kutoa elimu ya afya utaanza Julai mwaka huu baada ya mapitio ya mtaala
huo na inatarajiwa ifikapo mwaka 2015 wanafunzi watajua afya ya uzazi na kupata
walimu waliobobea katika masomo hayo.
Nchi zilizoshiriki
mkutano huo ni pamoja na Afrika Kusini, Kenya, Sweden, Uganda, Malawi,
Zimbabwe, Zambia, Burundi, Namibia, Rwanda, Botswana, Lesotho, Swaziland,
Angola, Ethiopia na wenyeji Tanzania.
No comments:
Post a Comment