TAARIFA ZAOKOA MALI ZA UMMA ZA SHILINGI BILIONI 39.9


Tuhuma 3,099 za rushwa zikiwemo mpya 679 zilichunguzwa ambapo uchunguzi wa tuhuma 666 ulikamilika katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014.
Aidha kiasi cha Sh bilioni 39.9 kiliokolewa baada ya kutolewa taarifa zinazohusiana na wizi wa mali ya umma.
Hayo yalisemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Umma, Celina  Kombani jana wakati akiwasilisha bungeni makadirio ya matumizi ya fedha kwa mwaka 2014/ 2015.
Alisema kati ya tuhuma hizo ambazo uchunguzi umekamilika majalada 234 yaliombewa kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) ambapo majalada 174 yalipata kibali cha kuwafikisha watuhumiwa mahakamani.
Pia majalada 139 ya uchunguzi maalumu wa vocha za pembejeo yalifanyiwa uchunguzi ambapo 19 yaliombewa kibali cha mashtaka na kati ya hayo majalada manne yalipata kibali cha kuwafikisha watuhumiwa mahakamani.
Aidha alisema majalada yanayohusu maliasili ya nchi yalifanyiwa uchunguzi ambapo majalada 10 yaliombewa kibali cha Mkurugenzi wa mashtaka na kati ya hayo, majalada manne yalipata kibali cha mashtaka.
Alisema majalada manne yaliyohusu tuhuma kubwa za rushwa  yalifikishwa kwa mkurugenzi wa mashtaka kuombewa kibali cha mashtaka.
“Kupitia vyanzo tofauti vya taarifa zinazohusiana na wizi wa mali za umma kiasi cha Sh 39,910,523,898 kiliokolewa,” alisema.
Waziri Kombani alisema katika kipindi cha kuanzia Julai 2013 hadi Machi 2014, Wizara yake  ilitoa vibali vya ajira mpya kwa watumishi wa umma 50,155 kati ya nafasi 61,915 zilizoidhinishwa katika bajeti ya Serikali ya mwaka 2013/2014 sawa na asilimia 81.
Alisema madai ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi wa umma yameendelea kulipwa hadi kufikia Machi 2014 jumla ya madai ya watumishi 56,622 yenye thamani ya Sh 55,993,095,061.95 yalipokelewa.
Pia madai ya watumishi 45,048 yenye thamani ya Sh  41,760,794,348.95 yalihakikiwa na kuingizwa kwenye mfumo tayari  kwa malipo kati yao watumishi 41,952 wamelipwa malimbikizo ya mishahara yenye thamani ya Sh 36,236,611,127.75.
Malipo ya malimbikizo ya watumishi 3,096 yenye thamani ya Sh 5,524,183,221 yapo kwenye mfumo yakisubiri kulipwa. Madai ya malimbikizo ya watumishi 11,574 yenye thamani ya Sh 14,234,300,713 yapo kwenye hatua ya uhakiki kabla ya kuingizwa kwenye mfumo wa malipo.
Waziri Kombani alisema utafiti kuhusu uelewa wa viongozi juu ya maadili ya uongozi na sheria ya maadili ya viongozi wa umma ulifanyika na kuhusisha viongozi 540 kati ya hao viongozi 514 sawa na asilimia 95.2 walisema wanaifahamu sheria hiyo na viongozi 26 sawa na asilimia 4.8 walisema hawaifahamu.

No comments: