Shule
ya Msingi ya Tusiime ya Dar es Salaam imeng’ara katika tuzo zilizotolewa na
Mkoa wa Dar es Salaam kwa kunyakua tuzo 12.
Tuzo
hizo zimetokana na kuwa na wanafunzi kumi bora kwa upande wa wasichana na kumi
bora kwa upande wa wavulana kwenye matokeo ya darasa la saba mwaka jana.
Hafla
hiyo ya kuzipongeza shule bora na wanafunzi bora ilifanyika juzi jijini Dar es
Salaam ambapo mgeni rasmi alikuwa Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Raymond
Mushi.
Akizungumza
kabla ya kukabidhi tuzo hizo, Mushi alisema shule na wanafunzi waliofanya
vizuri wanastahili kupongezwa ili iwe chachu kwa wanafunzi wengine.
Alisema
Mkoa wa Dar es Salaam umejitahidi kufikia ufaulu wa asilimia 75 ingawa
haukufikia lengo la matokeo makubwa sasa hivyo aliwaomba wadau wa elimu
kuongeza bidii ili kufikia malengo tarajiwa.
Alisema
ufaulu kwa sekondari katika mitihani ya kidato cha nne umeshuka hadi asilimia
59 hivyo aliwaomba wadau watazame changamoto hiyo na wawe na uhakika na
matarajio wanayotarajia.
Mwanafunzi
bora kimkoa ni Hussein Hemed Hussein kutoka Tusiime aliyepata alama 244 kati ya
250 zilizohitajika na ndiye alikuwa mwanafunzi bora kitaifa katika matokeo ya
darasa la saba mwaka jana.
Akizungumza
mara baada ya shule yake kutwaa tuzo hizo, Mkurugenzi wa Shule za Tusiime,
Albert Katagira, alisema usimamizi mzuri na ufuatiliaji wa taaluma shuleni
kwake ndiyo siri ya matokeo mazuri ya shule yake kila mwaka.
Alisema
shule yake ina kitengo cha ufuatiliaji ambacho kimekuwa kikifuatilia kwa karibu
mwenendo wa taaluma kwa walimu wanavyofundisha na maendeleo ya wanafunzi
kitaaluma siku hadi siku, hali ambayo imekuwa ikileta chachu kwa wanafunzi
kusoma kwa bidii.
Shule
zingine zilizoingia kumi bora Dar es Salaam ni Montfort, St Joseph Millennium,
Fountain of Joy, Hazina, Nyiwa, Heritage, Holy Cross, New Ambassador na Azanak.
No comments:
Post a Comment