Spika wa Bunge, Anne Makinda amesema Bunge la
Tanzania liko katika mchakato wa kuandaa Sheria na Kanuni itakayosimamia idara
mpya, inayotarajiwa kuundwa itakayosimamia na kuongoza shughuli zote za Kamati
ya Bunge ya Bajeti.
Makinda alisema hatua hiyo, inatokana na
Bunge hilo kutambua changamoto iliyopo ndani ya kamati hiyo, ambayo ni pamoja
na ukosefu wa idara hiyo nyeti ya kuisimamia.
Alikuwa akifungua semina ya siku tano ya 25
ya Chama cha Mabunge ya Jumuiya ya Madola (CPA), inayofanyika jijini Dar es
Salaam, ambapo Tanzania ni mara yake ya kwanza kuwa mwenyeji wa semina hiyo.
“Katika dunia ya leo ya utandawazi, mabunge
mengi duniani yako katika mchakato wa mageuzi katika utendaji wake ili
kuhakikisha shughuli na uwajibikaji wake unawafikia ipasavyo na kwa uwazi
wananchi, na Bunge la Tanzania ni moja ya mabunge hayo yanayopitia mageuzi
hayo,” alisema Makinda.
Alisema katika Bunge la 10, Bunge hilo,
lilipitia mageuzi kadhaa kwa ajili ya kuliimarisha ikiwemo kuanzishwa kwa
kamati hiyo ya bajeti ambayo imetimiza takribani mwaka mmoja sasa tangu
kuanzishwa kwake.
Alisema katika kipindi hicho, kamati hiyo
imeweza kuimarisha ushiriki wa Bunge la Tanzania katika mchakato mzima wa
uandaaji wa bajeti ambapo kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, Bunge
hilo, limeweza kubadili baadhi ya vifungu vya fedha na kupendekeza maeneo yenye
umuhimu kwa wananchi kupewa kipaumbele.
Akizungumzia mada itakayowasilishwa na
kujadiliwa katika semina hiyo inayohusu mbunge anawajibika kwa nani, chama,
Bunge au taifa lake? Makinda alisema mada hiyo ni muhimu kwa kuwa itatoa dira
na mafunzo kwa wabunge ikiwa ni pamoja na kutoa mwanga juu ya hatua
zitakazochukuliwa kwa mbunge asiyetambua wajibu wake.
“Mada hii itatoa mwanga na kuwapa uelewa
wabunge wa kujitambua, kwa kuwa hili ni tatizo hata hapa nchini, kuna kesi
mbalimbali zinaendelea katika mahakama za nchi wanachama wa CPA ikiwemo sisi
Tanzania tuna kesi mbili za wabunge juu ya tatizo hili,” alisema Makinda.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa CPA Tawi la
Tanzania, Mussa Zungu, alisema semina hiyo pamoja na mambo mengi inatoa
changamoto kwa wabunge kufuata kanuni ndani ya Bunge na kutambua wajibu wao.
Akitolea mfano, suala la baadhi ya wabunge
waliounda chama cha Umoja wa Katiba ya Watanzania (UKAWA), alisema wabunge hao
wanatakiwa kutumia busara na kurejea bungeni baada ya kuzunguka kwa wananchi,
kwa kuwa ndani ya Bunge ndipo hoja zao zitakapofanyiwa kazi.
Katibu Mkuu wa CPA, Dk William Shija,
alimkabidhi Spika Makinda
kitabu kinachoitwa ‘Following the Money’
ambacho kinazungumzia kanuni za Bunge katika kusimamia na kufuatilia matumizi
ya Serikali.
Semina hiyo imejumuisha wabunge 60 kutoka
nchi 18 wanachama wa CPA, wakiwemo wageni maarufu kama vile Spika wa Bunge la
Uganda, Rebecca Kadaga, Naibu Spika wa Bunge la Malasyia Ronald Kiandee, Spika
wa Jimbo la Australia Mashariki Barry House na Mnadhimu Mkuu wa Serikali ya
Ghana, Dk Benjamin Bewa-Nyogo Kunbour.
No comments:
Post a Comment