Serikali imetaka vyombo vya habari, kutumia ushawishi
wake kwa jamii, kuripoti shughuli za utalii na kuvitangaza vivutio mbalimbali
vya utalii vilivyopo nchini kuhamasisha utalii wa ndani na nje.
Hayo yalielezwa jana na Katibu Mkuu wa Wizara
ya Maliasili na Utalii, Maimuna Tarishi wakati akifungua warsha ya wahariri wa
vyombo vya habari, inayofanyika jijini hapa.
“Ni wakati muafaka sasa kwa vyombo vya habari
kuamua kwa makusudi na kwa kuongeza uhamasishaji kwa jamii kwa kuvitangaza ili
jamii iweze kuvitembelea,” alisema.
Alisema vivutio vya utalii, vipo katika
maeneo yote nchini na kwamba utalii unapaswa kuwa endelevu na usiyumbe, utalii
wa ndani unahitajika hivyo kasi ya
uelewa, inahitajika kwa vyombo vya habari kujulisha umma.
Tarishi alisema utalii ni moja ya sekta, ambazo huchangia kwa kiasi kikubwa katika
uchumi wa Tanzania, ambapo kwa mwaka jana inakadiriwa uliingiza dola za
Marekani bilioni 1.8.
Aidha, alisema tafiti zinaonesha sekta ya
utalii, ilitoa ajira 1,196,000 za moja
kwa moja na zisizo za moja kwa moja.
Alisema katika mwaka huo, Tanzania ilipokea
watalii wa nje wapatao 1,135,884. Alitaka vyombo vya habari kutumika katika
kutangaza vyema vivutio na hifadhi ili ziweze kutembelewa na wageni wengi
zaidi.
Awali, Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Hifadhi
za Taifa (TANAPA), Ibrahimu Musa alisema eneo la utalii wa ndani ni changamoto
kubwa kwa shirika, licha ya sekta ya utalii kutoa mchango mkubwa kwenye uchumi
wa nchi.
Alisema mkutano huo, ambao unafanyika kwa
mara ya pili na kuwahusisha wahariri wa
habari, una kaulimbiu inayosema ‘Wajibu
wa Vyombo vya Habari katika Kukuza Utalii’.
Warsha hiyo imeandaliwa na Tanapa, yenye
dhamana ya kusimamia maeneo yote, yaliyotengwa kisheria kama hifadhi.
No comments:
Post a Comment