Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu
imesisitiza kuwa ili mradi wa treni ya kusafirisha abiria jijini Dar es Salaam,
ufanyike kwa kasi na kwa ufanisi, Serikali iharakishe kununua angalau treni
mbili za kisasa.
Aidha, imeishauri kuongeza kasi katika
kutafuta kampuni tanzu mahsusi kwa usafiri huo, ambayo itatoa fursa kwa sekta
binafsi kushiriki kutoa huduma jijini.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Peter Serukamba
alisema hayo jana bungeni wakati akitoa taarifa ya Kamati hiyo kuhusu
utekelezaji wa Bajeti ya Wizara ya Uchukuzi ya mwaka 2013/14 na maoni kuhusu
bajeti ya 2014/15.
“Kamati inasisitiza kuwa ili mradi uweze
kufanya kazi kwa ufanisi na kuondokana na hasara, Serikali iharakishe kununua
angalau treni mbili za kisasa na maalumu kwa safari fupi ambazo gharama yake ni
takribani shilingi bilioni nane kila moja.
“Vile
vile Kamati inashauri Serikali kuongeza kasi katika kutafuta kampuni tanzu
mahsusi kwa usafiri wa treni ya abiria, ambayo itatoa fursa kwa sekta binafsi
kushiriki katika kutoa huduma ya usafiri wa treni katika Jiji la Dar es Salaam
na miji mingine nchini,” alisema Serukamba.
Kuhusu usafiri wa reli kwa ujumla, Kamati
hiyo iliishauri Serikali kuchukua hatua mahsusi za kukarabati na kuimarisha
mtandao wa reli nchini, hata kwa kutafuta fedha nje ya utaratibu wa kawaida wa
bajeti.
Ilishauri Serikali kutoa fedha za miradi ya
reli zipatazo Sh bilioni 9.8, zilizobaki katika mwaka wa fedha 2013/14 ili
mabehewa yanayotengenezwa nje ya nchi, yaweza kuwasili na kuboresha huduma za
usafiri wa reli nchini.
Akizungumzia viwanja vya ndege, Serukamba
alisema kumekuwa na changamoto na migogoro mingi ya ardhi baina ya wananchi
wanaoishi kando ya viwanja vya ndege.
“Kamati inaishauri Wizara ya Uchukuzi kwa
kushirikiana na Wizara ya Ardhi pamoja na mamlaka zingine zinazohusika na ardhi
kuhakikisha inaweka mipaka katika maeneo ya viwanja vyote vya ndege na kuvipa
Hati Miliki,” alisema Serukamba na kuongeza:
“Vile vile kwa maeneo ambayo yametwaliwa na
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege kama vile Omukajunguti-Bukoba, malipo ya fidia kwa
wananchi yafanyike haraka.”
Kuhusu Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL),
Serukamba alihoji kama Serikali inatambua umuhimu wa kampuni hiyo na kama bado
inaihitaji, na kama inaihitaji, kwa nini haitoi mtaji wa kutosha.
“Kamati inaishauri Serikali iamue kuwekeza
mtaji wa kutosha ili iweze kulipa madeni yote ya ATCL hatimaye kufufua upya
kampuni hii,” alisema mbunge huyo wa Kigoma Mjini (CCM).
Kwa upande wake, Msemaji wa Kambi Rasmi ya
Upinzani Bungeni, Moses Machali alisisitiza Serikali kuweka mkazo katika sekta
zote zinazozalisha mali na huduma muhimu kama vile usafiri wa anga, barabara,
maji, elimu na afya.
“Wanasiasa wenzangu tujenge nchi yetu, tuamue
sasa kwamba tuanze na kuhamisha mafungu ya fedha za matumizi yasiyo ya lazima
na kuzipeleka kwenye reli na bandari mwaka huu na tuanze na hizo za Uchukuzi
zenyewe,” alisema mbunge huyo wa Kasulu Mjini (NCCR-Mgeuzi).
No comments:
Post a Comment