Serikali
imeamua kuanzisha bodi ya kitaalamu ya walimu Tanzania
katika mwaka ujao wa fedha, itakayosimamia masuala ya walimu, ikiwemo usajili,
uendelezaji wa walimu na maadili ya kazi ya ualimu.
Waziri
wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa, alisema hayo mwishoni mwa
wiki wakati akiwasilisha makadirio ya bajeti ya Wizara yake kwa mwaka
2014/2015.
Alisema
Wizara itaendelea kujadiliana na wadau wengine ikiwemo Ofisi ya Rais,
Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na
Serikali za Mitaa (Tamisemi) kuhusu suala namna bora ya kumhudumia mwalimu
katika mazingira ya sasa ya ugatuaji wa huduma mbalimbali kwenda
Tamisemi.
Wakati
huo huo, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii katika taarifa yake
imetaka posho ya mazingira magumu, itolewe kwa walimu.
Kamati
hiyo imetaka Serikali kukamilisha mapema iwezekanavyo mchakato wa kutoa posho
ya mazingira magumu kwa walimu, wanaofanya kazi hasa vijijini na kusisitiza
umuhimu wa mafunzo kwa walimu kazini.
Suala
lingine ambalo kamati hiyo chini ya uenyekiti wa Margaret Sitta
inapendekeza ni Serikali kuangalia upya mfumo wa kuhudumia walimu kwa kuanzisha
Tume ya Utumishi wa Walimu ili kukabili adha zinazowakabili watumishi
hao.
Wizara
imeomba kuidhinishiwa Sh bilioni 799, ambazo kati yake Sh bilioni 344.2 ni kwa
ajili ya matumizi ya kawaida na Sh bilioni 454.8 ni kwa ajili ya matumizi
ya maendeleo kwa mwaka 2014/2015.
Bajeti
ya wizara hiyo imeongezeka kutoka Sh bilioni 689.7 mwaka 2013/2014 hadi Sh
bilioni 799 mwaka 2014/2015. Pia bajeti ya matumizi ya maendeleo, imeongezeka
kutoka Sh bilioni 72 mwaka huu wa fedha hadi Sh bilioni 454 kwa mwaka
ujao wa fedha.
Wakati
huo huo leo ni zamu ya Wizara ya Viwanda na Biashara kuwasilisha bajeti yake
bungeni. Pia Wizara ya Ujenzi itasoma bajeti yake leo, kabla ya kujadiliwa
keshokutwa.
No comments:
Post a Comment