Katibu
Mkuu wa Jimbo la Kanisa Katoliki Same, Padre Bruno Chelagwa amehadharisha
vijana kujiepusha na vishawishi vya kutaka utajiri wa harakaharaka kwa
kujitumbukiza kwenye biashara ya dawa za kulevya.
Padre
Chelagwa alitoa tahadhari hiyo, alipokuwa mgeni rasmi kwenye mahafali ya tatu
ya kidato cha sita katika shule ya Sekondari ya Wasichana ya Sayansi Kandoto
Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro mwishoni mwa wiki.
‘’Msidanganywe
kukimbilia utajiri wa harakaharaka kwa kujitumbukiza kwenye madawa ya kulevya.
Someni zaidi mpate ujuzi na kazi itakayowawezesha kuishi maisha mazuri,’’
alisisitiza.
Alifafanua
kwamba elimu peke yake, haitoshi katika maisha, bali pia wanatakiwa kuzingatia
utu na ubinadamu na kuongeza kuwa elimu bila utu ni kazi bure.
Ofisa
Elimu wa Wilaya ya Same, Happiness Laiza aliwataka wahitimu hao, kuwa makini
wanapojiunga na vyuo vya elimu ya juu kwa kujichunga na kujiongoza wenyewe.
‘’Mnapokwenda
vyuo vikuu hakuna kengele ya kukuamsha, sare za shule wala geti bali ni wewe
mwenyewe kujiongoza tafauti na mlivyokuwa katika ngazi ya sekondari,’’ alisema.
Aliwaasa
pia kuwa makini na gonjwa hatari la Ukimwi kwa kuepuka vitendo vya ngono zembe
katika maisha yao ya elimu ya juu, wanayotegemea kujiunga siku za usoni.
Ofisa
Elimu huyo pia alikabidhi shule hiyo tuzo, waliyotunukiwa na Wizara ya Elimu na
Mafunzo ya Ufundi katika Wiki ya Elimu ilifanyika mjini Dodoma hivi karibuni
kwa kupata matokeo mazuri ya kidato cha nne kwa mwaka 2013 kwa kushika nafasi
ya 22 kitaifa.
Kwa
upande wake, Mkuu wa Shule hiyo , Padre Peter Mziray, awali katika hotuba
yake kwenye mahafali hayo, aliwakumbusha wahitimu kuwa makini katika masomo yao
ya elimu ya juu kwa kutobweteka kwamba wametoka kwenye shule nzuri.
‘’
Ni rahisi kwa mtu mzima wa afya kuwa mlemavu wa viungo lakini siyo rahisi kwa
mlemavu wa viungo kuwa na afya njema,’’ alionya.
Katika
hotuba yao, wahitimu nao pamoja na kushukuru uongozi wa shule hiyo kwa
kuwapatia malezi na elimu bora, walitoa changamoto kwa shule hiyo kuongeza
idadi ya walimu na vitabu kwenye maktaba ya shule.
Shule
ya Sekondari ya Wasichana ya Sayansi Kandoto, ina jumla ya wanafunzi 586 wa
kidato cha kwanza hadi cha sita. Ni wanafunzi 11 wa michepuo ya masomo ya PCB
na PCM ndiyo waliohitimu masomo yao ya kidato cha sita mwaka huu shuleni hapo.
No comments:
Post a Comment