Serikali
imeuonya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), kuwa makini na mpango inaotaka
kuuanza katika mwaka ujao wa fedha wa kutoa mikopo ya dawa kwa watoa huduma
wote waliosajiliwa.
Naibu
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Kebwe Stephen aliyasema hayo Jumanne wiki
hii wakati alipotembelea makao makuu ya mfuko huo Kurasini Dar es Salaam na
kuzungumza na Menejimenti.
Katika
taarifa yake kwa Waziri, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Hamis Mdee alisema
katika kukabiliana na uhaba wa dawa, wanatarajia kuanza kutoa mikopo ya dawa
kama ilivyo kwa vifaa tiba kwa majaribio, kabla ya kueneza utaratibu huo kwa
watoa huduma wote waliosajiliwa.
Lakini
Naibu Waziri akautaka Mfuko huo kufanya uangalifu mkubwa katika eneo hilo kwa
sababu dawa zimekuwa na gharama kubwa, lakini pia kumekuwapo na watumishi wasio
waaminifu wanaoiba dawa.
“Hili
la kukopesha dawa ni lazima mliangalie kwa uangalifu mkubwa. Dawa ni eneo lenye
gharama kubwa. Kwa mfano, mwaka jana, zimetengwa Shilingi bilioni 80 kwa ajili
ya dawa, na sasa zaidi ya asilimia 70 imeshatumika kununulia dawa hizo,”
alisema Naibu Waziri.
Dk
Kebwe alisema kuwa hali hiyo imefanya upatikanaji wa dawa uwe kwa asilimia 80,
lakini akabainisha kuwa hofu yake hiyo ya kuanza kutoa mikopo ya dawa inatokana
na ukweli kuwa kuna watumishi wasio waaminifu ambao wamekuwa wakiiba fedha
hizo.
“Kuna
wizi au udokozi katika eneo hili la dawa. Kwa mfano, kule Magu kuna mfamasia
tumemfunga miaka mitano jela kwa wizi wa vitendanishi vya malaria. Tumemfunga
huyu kuwa mfano kwa watumishi wengine, na watakaopatikana, sheria itachukua
mkondo wake,” alieleza Naibu Waziri.
Alisema
hofu nyingine ni kwamba je dawa hizo zitawafikia walengwa, kwani licha ya dawa
kuwekwa alama na Serikali kupitia Bohari Kuu ya Dawa (MSD), bado kumekuwapo na
wizi, kwa watumishi wasio waaminifu wanaoshirikiana na watoa huduma za afya
nchini.
Awali,
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, alisema mbali ya kuanza kutoa mikopo ya dawa
kama njia ya kukabiliana na uhaba wa dawa, pia wataongeza ufuatiliaji wa
matumizi ya fedha za uchangiaji na kutoa taarifa ya utekelezaji wa agizo la
asilimia 67 ya fedha za uchangiaji zitumike kununulia dawa.
Kwa
upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NHIF, Balozi Ali Mchumo aliitaka
Serikali kuharakisha uundwaji wa bodi maalumu itakayosimamia bei za huduma za
afya kama ilivyo kwa simu na maji, akisema itasaidia kupunguza gharama kubwa
kwa watoa huduma na bei zisizodhibitiwa.
No comments:
Post a Comment