Mtandao
wa wabunge katika mashirika ya fedha ya kimataifa wametembelea wanavijiji
wanaonufaika na mradi wa utoaji fedha kwa kaya masikini unaotekelezwa na
Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) wilayani Bagamoyo na kujiridhisha na
utekelezaji.
Wabunge
kutoka nchi mbalimbali duniani wanaunda mtandao pamoja na Benki ya Dunia
pamoja na Shirika la Fedha Duniani (IMF) , walitembelea juzi Kijiji cha Kerege
na Mlingotini, mkoani Pwani ambako walipata ushuhuda wa walengwa
wanavyonufaika.
Katika
kijiji cha Mlingotini, wabunge walitembelea kikundi cha wanawake cha
Mshikamano chenye wanachama 12 kinachoendesha miradi ya ufugaji kuku, mbuzi na
uuzaji samaki chini ya mradi huo unaofadhiliwa na Benki ya Dunia kupitia
Tasaf.
Akizungumza
mbele ya ujumbe huo, Mweka Hazina wa kikundi , Stahabu Mrisho alisema Tasaf
iliwapatia Sh milioni 13 ambazo walitumia kujenga jengo la biashara, kununua
majokofu na pia kwa mtaji.
“Kwa
kweli tumenufaika sana na Tasaf. Tumekuwa tukigawana mapato kila mwaka lakini
pia akiba na hisa zimetusaidia kuanzisha miradi ya magenge na mama ntilie…Tasaf
imetujengea utu na heshima mbele ya jamii,” alisema Stahabu.
Katika
Kijiji cha Kerege, ujumbe huo wa wabunge ulimtembelea mwanakijiji, Jema Lemabi
ambaye katika ushuhuda wake, alisema alikuwa na maisha magumu akitegemea kupika
na kuuza pombe.
Kwa
mujibu wa Jema, baada ya Tasaf kumwingiza kwenye mpango wa kupewa fedha,
alifanya miradi midogo midogo ikiwemo ufugaji wa bata, kuku na kanga na kumudu
kujenga nyumba imara iliyoezekwa kwa bati.
Jema
ambaye kwa mujibu wake, alikuwa akiishi nyumba ya makuti, anao bata 49, kuku
watatu na kanga wawili. Bei ya bata ni Sh 15,000 na kwamba soko lake kubwa ni
Bagamoyo Mjini.
Mpango
huo wa utoaji fedha kwa kaya masikini, umeanza rasmi mwaka huu kutekelezwa
nchini kote baada ya majaribio yaliyoanza 2008 mkoani Dodoma na Pwani. Walengwa
wake ni watoto na wazee katika kaya masikini zilizo katika mazingira
hatarishi.
Kwa
mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Tasaf, Ladislaus Mwamanga, Mpango huo wa
Uhawilishaji Fedha kwa Kaya Masikini chini ya ufadhili wa Benki ya Dunia,
unalenga Watanzania zaidi ya milioni 7.5 katika kaya zipatazo milioni 1.2
wanaoishi katika lindi la umasikini.
Mtandao
wa wabunge wa IMF na Benki ya Dunia unaundwa na wabunge 300 kutoka zaidi ya nchi
140 zinazoendelea na zilizoendelea ambako mashirika hayo ya kimataifa yanafanya
kazi.
Ulianzishwa
mwaka 2000. Ziara za wabunge husika nchini ni kujionea shughuli zinazotekelezwa
na Benki ya Dunia katika miradi mingine ya maendeleo.
No comments:
Post a Comment