MWAKYEMBE AAHIDI RELI KUANZA 'KUKIMBIA' MWAKA HUU



Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, amesema bajeti ya wizara hiyo ya mwaka 2014/15 iliyopitishwa juzi bungeni, itaifanya reli ianze kukimbia.
Amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2012/13, hali ya reli nchini ilikuwa katika chumba  mahututi na katika mwaka 2013/14, unaomalizika mwezi ujao, reli ilianza kutembea.
Dk Mwakyembe alisema hayo wakati akifanya majumuisho ya bajeti yake ambayo Bunge, baada ya mjadala mkali, ilipitishwa bajeti ya Sh bilioni 527.93.
“Mwaka 2012/13 hali ya reli ilikuwa katika chumba cha mahututi kwa sababu kulikuwa hakuna hela, mwaka 2013/14 reli ilianza kutembea, lakini kwa fedha za sasa reli itaanza kukimbia,” aliahidi Dk Mwakyembe.
Katika kudhihirisha hali nzuri, Dk Mwakyembe alisema kufikia Januari mwakani kutakuwa na vichwa vya reli vipya 51, badala ya vinane vya sasa ikiwa ni idadi kubwa ambayo haijawahi kutokea nchini.
Alisema kwa kuwa na vichwa hivyo, uwezo wa reli kubeba mizigo utaongezeka kutoka chini ya tani 200,000 za sasa kufikia tani milioni 1.5 kwa mwaka.
Kuhusu Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL), alisema tayari Wizara imepeleka katika Baraza la Mawaziri waraka unaokusudia kuifanya Serikali ibebe deni la Sh bilioni 133 la kampuni hiyo ili kusafisha mizania na kuifanya kampuni hiyo ipate uwekezaji.
Aidha, Serikali iliahidi kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Mwanza baada ya wabunge kueleza kuwa hawaridhishwi na utoaji wa fedha, zilizotengwa katika bajeti kwa ujenzi wa uwanja huo. 
Aisisitiza ushiriki wa sekta binafsi katika miradi mbalimbali ya sekta ya uchukuzi, huku akieleza kuwa ufanisi katika Bandari ya Dar es Salaam umeongezeka katika kipindi kifupi. 
Katika hatua nyingine, mjadala mkali ulizuka kuhusu sakata la Kampuni ya Usafiri Dar es  Salaam (UDA), kiasi cha Dk Mwakyembe kusema suala hilo limeingia katika bajeti yake wakati kampuni hiyo haiko katika majukumu ya wizara yake.

No comments: