Watu saba wamekamatwa na
Polisi mkoani Tabora wakituhumiwa kuhusika katika mauaji ya askari Polisi
wawili na unyang’anyi wa kutumia silaha, yaliyofanyika mwezi
uliopita.
Matukio hayo ya
unyang’anyi na mauaji yalifanyika Aprili 28, mwaka huu katika
Tarafa ya Usoke Wilaya ya Urambo.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa
wa Tabora, Suzan Kaganda alisema askari waliouawa, walikuwa katika harakati za
kutekeleza majukumu yao katika eneo hilo la Usoke. Askari hao ni F.5179
Konstebo Jumanne na G.3388 Konstebo Shaaban.
Kuhusu waliokamatwa,
wakituhumiwa kwa mauaji ya askari hao, kamanda aliwataja ni Silvester Mussa
maarufu kama Kingwendu (31), mkazi wa Mkuyuni Tambukareli, Mwanza.
Watuhumiwa wengine ni
Sadiki Rushikamwa ambaye anajulikana pia kama Sadiki Milambo au White (28),
mkazi wa Mihogoni Tabora na Abel Benedicto maarufu kama Mwendo wa saa (23),
ambaye ni mkazi wa Muungano Wilaya ya Urambo.
Wengine waliokamatwa ni
Francis Kashinje maarufu Masanja (38) mkazi wa Nansio, Ukerewe, Haji Athanas
(50) mkazi wa Usoke, Mussa Khatibu Ally (49) ambaye ni
mfanyabiashara wa nafaka na mkazi wa Mwanza Road. Mtuhumiwa mwingine ni
Ramadhan Mkunya, mkazi wa Tabora.
Kwa mujibu wa Kamanda,
baada ya mahojiano na polisi, watuhumiwa walikiri kushiriki matukio mbalimbali
ya unyang’anyi wa kutumia silaha pamoja na mauaji ya askari Polisi wawili.
Alisema baada ya upekuzi,
walikutwa na silaha aina ya Pistol Glock 17, yenye namba za usajili TZ
Car 91968, ikiwa na magazini yenye risasi tano.
No comments:
Post a Comment