Mtoto wa miaka
minne (jina limehifadhiwa), amedhulumiwa haki yake ya utu na kuteswa kwa zaidi
ya miaka mitatu, kwa kufungiwa ndani ya boksi kama mnyama, ili asimuambukize
mama mlezi virusi vinavyosababisha Ukimwi.
Unyama huo wa
kusikitisha, umefanyika muda wote huo kwa mtoto huyo Morogoro mjini katika mtaa
wa Azimio bila kuripotiwa popote, huku wakazi na majirani wa nyumba hiyo
wakisikia akikohoa na kulia usiku, na baba yake mzazi akiendelea na maisha kwa
kumuogopa mkewe.
Wakizungumza na mwandishi
jana, majirani hao walidai Mariam
alihamia katika nyumba hiyo mwaka 2010, lakini hawakuwahi kumuona akiwa na
mtoto.
Hata hivyo
majirani hao walikiri kwamba walikuwa wakisikia mtoto akikohoa na kulia hasa
nyakati za usiku, lakini walikuwa na wasiwasi kuwa huenda mtuhumiwa alikuwa
mshirikina anayefuga watu waliouawa kishirikina au kwa jina lingine misukule.
Hatimaye juzi
mateso ya mtoto huyo yalipungua, baada ya msamaria mmoja kupata taarifa sahihi,
kwamba ndani ya nyumba hiyo kuna kiumbe asiye na hatia aliye katika mateso na
kutoa taarifa kwa Ofisa Mtendaji wa Kata ya Kiwanja cha Ndege, Dia Zongo.
Zongo akiwa
katika kazi za kawaida katika mtaa huo, alipata taarifa kutoka kwa majirani
kuwa kuna mwanamke, Mariam Said, amemficha mtoto ndani ya boksi na hamfanyii
usafi wala kumtoa nje.
Baada ya kupata
taarifa hizo, Zongo alimtafuta mwenyeji wake, Mwenyekiti wa mtaa huo, Tatu
Mgagalana na kuongozana naye hadi kwenye
nyumba hiyo ambapo walimkuta mtuhumiwa, Mariam na kuanza kumhoji kuhusu tuhuma
hizo.
Kwa mujibu wa
Zongo, wakati mtuhumiwa akijibu maswali aliyoulizwa huku akibabaika, ghafla
mtoto huyo alipiga chafya na kuanza kukohoa hali iliyowapa wasiwasi na kuamua
kuingia chumbani kwa Mariam kwa nguvu, hatua iliyomuokoa mtoto huyo kutoka
katika mateso ya zaidi ya miaka mitatu.
Ofisa huyo na
mwenyeji wake walimkuta mtoto huyo ametapakaa uchafu uliotokana na kinyesi na
mkojo, kwa kuwa boksi hilo lilikuwa chumba chake cha kulala, meza yake ya
chakula na maji na choo kwa ajili ya haja ndogo na kubwa.
Hali ya mtoto
huyo ilisababisha mashuhuda waliokuwa wamezunguka nyumba hiyo, kuanza
kumshambulia Mariam kwa fimbo na mawe, na kumlazimu Zongo na mwenyeji wake
kufanya kazi ya ziada kumnusuru mtuhumiwa kwa kutoa taarifa Polisi, huku
wakijaribu kuzuia asidhurike.
Baada ya muda
askari Polisi walifika na kumchukua mtuhumiwa na alipofika kituoni, inadaiwa alikiri
kuanza kumlea mtoto huyo tangu akiwa na miezi tisa baada ya mama yake, kufariki
dunia mwaka 2010.
Mtuhumiwa huyo
alidai Polisi kuwa kwa mara ya mwisho, alimuogesha mtoto huyo Julai mwaka jana,
na alikuwa akimwekea chakula na maji ndani ya boksi hilo.
Mume wa
mtuhumiwa huyo, Mtonga Ramadhani ambaye ni mfanyabiashara wa Soko la Mawenzi
katika Manispaa ya Morogoro naye alikamatwa na katika mahojiano, alidai hakuona
sababu ya kutoa taarifa za kufichwa kwa mtoto huyo kwa sababu hamhusu na wajibu
wake ilikuwa kutafuta chakula tu.
Kwa sasa mtuhumiwa huyo yupo Kituo Kikuu cha Polisi
mjini
Morogoro
na mtoto amepelekwa katika Ofisi
ya Idara ya Ustawi wa Jamii.
Baba mzazi wa
mtoto huyo, Rashid Mvungi ambaye ni mtumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya
Morogoro, alidai baada ya mzazi mwenzake kufariki dunia, alishindwa kumchukua
mtoto wake kwa sababu tayari alishakuwa na mke.
Alidai kwa kuwa
alikuwa ameoa, alikubaliana na upande wa pili wa familia ya marehemu, kuwa
mwanawe huyo alelewe na mama yake mkubwa, Mariam.
Akizungumzia
ulemavu wa mtoto huyo, Ofisa Ustawi wa Jamii, Oswin Ngungamtitu alisema
ulemavu huo huenda umetokana na kuishi kwenye boksi tangu akiwa na miezi tisa
hadi sasa bila kutolewa nje, kufanyiwa usafi wala kupewa chanjo mbalimbali
ikiwemo ya polio.
Ngungamtitu
alisema ulemavu huo pia huenda umetokana na kukosa lishe yakiwemo maziwa ya
mama, hewa safi na upendo na
kwamba mtoto huyo atakuwa na magonjwa mbalimbali ikiwemo minyoo, nimonia,
utapiamlo na malaria.
Kutokana na hali
hiyo, Ngungamtitu alisema ofisi yake imempeleka katika Hospitali ya Rufaa ya
Mkoa wa Morogoro, ili akafanyiwe uchunguzi na kupewa chanjo ya kutibu magonjwa
yatakayobainika.
Baada ya hapo
kwa mujibu wa Ofisa huyo, mtoto huyo atapelekwa kwenye kituo cha kulelea
watoto yatima na ikibidi atakabidhiwa kwa baba yake mzazi.
Kwa mujibu wa
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Leonard Paulo, mwanamke huyo pamoja na
mumewe wanashikiliwa Polisi kwa kosa la kumfanyia ukatili mtoto kinyume cha
Sheria ya Mtoto ya 2009.
No comments:
Post a Comment