Wabunge
wamesema hali ya elimu nchini ni mbaya, na kumshauri Rais Jakaya Kikwete kuunda
Tume ya Kudumu ya Elimu, ili kuangalia ubora na kudhibiti sekta hiyo muhimu.
Katika
michango yao kwenye mjadala wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi
uliotarajiwa kuhitimishwa jana jioni, wabunge wamesema suala la elimu halina
siasa, na nchi isipochukua hatua sasa, itakuwa hatari kwa vijazi vijavyo.
Mbunge
wa Kuteuliwa, James Mbatia (NCCR-Mageuzi), alieleza matatizo kadhaa katika
mitihani ya Darasa la Saba pamoja na ule wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) na kudai
kuwa “kuna madudu makubwa.”
Mbatia
aliyekuwa ameshika nakala za mitihani hiyo na baadaye kuiwasilisha kwa Naibu
Spika, Job Ndugai, alidai baadhi ya mitihani hiyo ni migumu na imewashinda
maprofesa wa vyuo vikuu.
“Mimi
niliwapatia mitihani hii maprofesa wa vyuo vikuu, imewashinda. Niliwapa huu wa
hisabati, akanirudishia akisema mtihani wenyewe haufanyiki.
“Sasa
kama yupo mtu humu atamudu kuufanya na kupata alama mia moja, nampa milioni
kumi,” alisema Mbatia, huku Naibu Spika akieleza kuwa Waziri Profesa Sospeter
Muhongo yuko tayari kuufanya.
“Profesa
Muhongo ni profesa wa miamba, kama ataweza huu hapa aje achukue,” alitamba
Mbatia.
Mbatia
alisema elimu ya Tanzania ni dhaifu na nchi, imeshindwa katika elimu na kuwa
suala hilo si la chama cha siasa.
Akitoa
majawabu ya hoja zake, Mbatia alimshauri Rais kuunda Tume ya Kudumu ya Elimu
ambayo pamoja na mambo mengine, alisema itaangalia ubora na kudhibiti elimu
nchini.
Msomi
huyo alitaka pia Tume hiyo ifanye kazi ya kuandaa mitaala, kuhariri vitabu
akisema Tanzania haina wahariri wa vitabu kama ilivyo kwa vyombo vya habari
vyenye wahariri wa aina mbalimbali.
Alizitaja
kazi nyingine kuwa ni kufanya utafiti wa kisayansi, kuamua lugha ya kufundishia
na kuangalia kwa ujumla tatizo la kushuka kwa elimu.
Alisema
elimu siyo bidhaa ya kuuzwa sokoni, bali iwe huduma na kukerwa na kodi nyingi
katika elimu na gharama za ada kwa shule binafsi.
“Ni
lazima tuukubali ukweli na kukabiliana nao. Elimu yetu imeshuka. Watoto wa
walalahoi watapata tabu, kama hatukuisimamia hili, tutapata tabu katika miaka
20 au mia ijayo hasa wakati huu wa sayansi na
teknolojia,”
alisema Mbatia.
Mbunge
wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba (CCM), aliyesema kuwa elimu iko katika chumba
cha wagonjwa wenye uangalizi maalumu (ICU).
Kama
Mbatia, Serukamba alishauri kuanzishwa kwa Tume ya kujichunguza kuhusu
kuporomoka kwa elimu nchini, akisema “tukubali waseme, tujisahihishe.”
Alisema
suala hilo si la mtu mmoja, na kuacha siasa na kuongeza kuwa kama kuna jambo
“tunacheza nalo, basi ni elimu, tunaua kizazi kijacho.”
Alisema
si vyema kutatua tatizo la elimu kwa kuangalia leo tu, bali uwepo mkakati wa
dhati wa muda mrefu, na kutolea mfano Marekani ilivyopitia mfumo wake wa elimu
mwaka 1981.
Kwa
upande wake, Mbunge wa Bukoba Vijijini, Jason Rweikiza (CCM), ambaye anamiliki
shule kadhaa nchini, alisema kuna tatizo la shule binafsi kulundikiwa kodi
nyingi, na ndio manaa zinatoza ada kubwa.
“Kuna sijui kodi ya mapato, PAYE, majengo,
SDL, yaani ni michango, michango, kodi. Kwa staili hii, ada inapanda, baadaye
shule inakufa,” alisema Rweikiza.
Aidha,
kama walivyopendekeza wabunge wengine waliochangia jana, mbunge huyo alitaka
ukaguzi utiliwe mkazo, akitoa mfano kuwa shule zake hazijakaguliwa tangu mwaka
2005.
Mbunge
wa Ngara, Deogratius Ntukamazina (CCM), alisema kwa sasa hakuna Wizara ya Elimu
baada ya kuondolewa kwa shule na msingi na sekondari.
Badala
yake, akashauri wizara hiyo ibaki kuwa kitovu cha mawazo bora ya elimu kama
ilivyo Tume ya Mipango kuhusu masuala ya mipango.
Said
Arfi wa Mpanda Mjini (Chadema), licha ya kuzungumzia ukaguzi, alisema bajeti ya
elimu imezidi kutegemea wahisani ambao hawatekelezi ahadi zao.
Nyambari
Nyangwine wa Tarime (CCM), ambaye ni mtunzi wa vitabu, alipendekeza kuanzishwa
kwa Shirika la Uchapaji, kwani vitabu ni moja ya maeneo yanayochangia mporomoko
wa elimu nchini.
Mbunge
wa Viti Maalumu, Magdalena Sakaya (CUF), alisema mazingira mabovu, ukaguzi
kuachwa, shule kukosa maabara na kushuka kwa morali ya walimu, kumechangia
kushuka kwa elimu nchini.
Mbunge
wa Kilolo, Profesa Peter Msolla (CCM), alitaka masuala ya shule za msingi na
sekondari yabaki katika wizara hiyo na irejeshwe wizara ya kusimamia elimu ya
juu, huku akisisitiza kuwa upangaji madaraja ni angamizo katika elimu nchini.
Naibu
Spika Ndugai naye alipendekeza masuala ya elimu yaondolewe Ofisi ya Waziri Mkuu
tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na kurejeshwa kwa wizara hiyo
ili yasimamiwe vyema.
Kambi
Rasmi ya Upinzani ilisema kuwa malengo na mikakati yote iliyoanishwa ni mizuri,
lakini “tunadhani mikakati hiyo imekuwepo muda mrefu, kilichokosekana ni
utekelezaji na ufuatiliaji wake.”
Msemaji
wake, Susan Lyimo alishauri mikataba ya utendaji kazi katika kila ngazi ya
elimu iwekwe wazi ili atakayeshindwa kutekeleza wajibu wake ijulikane
atawajibika vipi.
No comments:
Post a Comment