Rais
Jakaya Kikwete, amewaahidi wafanyakazi nchini kuwa katika mwaka ujao wa fedha
ambao Mpango wa Bajeti umeonesha kuwa itakuwa ya Sh trilioni 19.7, Serikali
itapandisha mishahara ya wafanyakazi.
Pia
ameonya taasisi za umma na waajiri wote wanaokwepa kuanzisha mabaraza ya kazi
na matawi ya vyama vya wafanyakazi katika maeneo yao ya ajira, kuwa kitendo
hicho ni kinyume cha Sheria na kuiagiza Wizara ya Kazi na Ajira, kufuatilia
suala hilo, na kuwachukulia hatua watakaobainika.
Akizungumza
katika Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani Dar es Salaam jana, Rais
Kikwete alisema suala hilo la mishahara ni kilio cha wafanyakazi cha siku
nyingi, lakini pamoja na uhaba wa fedha unaoikabili Serikali, imekuwa
ikijitahidi kila mwaka, kuongeza mishahara hiyo kulingana na uwezo wake.
“Najua hiki ndio kilio chenu na wote
mnasubiria kwa hamu Serikali inasema nini? Nawaahidi kuwa katika hotuba ya
Bajeti Waziri wa Kazi na Ajira, itabainisha wazi, kiwango cha mshahara ambacho
Serikali imekiongeza katika mishahara ya wafanyakazi,” alisema Rais Kikwete.
Hata
hivyo, alisema Serikali haitoweza kupandisha mishahara hiyo na kufikia ombi la
Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA), kwamba mishahara ya kima cha
chini ipande kutoka Sh 240,000 za sasa na kufikia Sh 750,000, kwa kuwa bado
pato la Serikali liko chini haliwezi kumudu kiasi chote hicho.
“Kwa
sasa pekee Serikali inatumia asilimia 44 ya Bajeti yake na asilimia 10 ya Pato
la Taifa kulipa mishahara ya wafanyakazi, kiwango ambacho ni kikubwa, lakini
kwa kuwa ina dhamira ya kuboresha maslahi ya wafanyakazi wake, imekuwa ikilipa
fedha hizo,” alisisitiza.
Alisema
Serikali kwa muda mrefu imekuwa ikijali wafanyakazi hasa Serikali ya Awamu ya
Nne, ambapo mwaka 2005 kima cha chini cha mishahara ya wafanyakazi kilikuwa Sh
65,000, lakini baada ya kuona ulazima wa kupandishwa kimepanda na kufikia Sh
240,000 ambayo nayo itaongezwa hivi karibuni.
Pamoja
na hayo, Rais Kikwete alionesha kutoridhishwa na namna sehemu kubwa ya sekta
binafsi, isivyozingatia viwango vya mishahara vinavyopangwa na Serikali, hali
inayochangia kuibuka kwa migogoro ya mara kwa mara baina ya waajiri na
waajiriwa.
“Hili
ni tatizo, lakini pia kuna malalamiko mengi tunayapokea serikalini kutoka
kwa wafanyakazi wa sekta binafsi ambayo kwa kweli yanatuumiza, sina budi kukutana
na waajiri ili tuzungumze kiundani na kutafuta ufumbuzi,” alisema Rais Kikwete.
Akizungumzia
suala la Kodi ya Mapato (P.A.Y.E), Rais Kikwete, alisema ombi hilo nalo kama
ilivyo nyongeza ya mishahara ni la muda mrefu, na kuwaahidi wafanyakazi hao
kuwa nalo linafanyiwa kazi ili kupunguza kutoka asilimia 13 inayotozwa kwa sasa
na kufikia tarakimu moja.
Katika
jitihada za kupunguza matatizo ya wafanyakazi, Rais Kikwete alisema
Serikali ina mpango wa kuanzisha Mfuko Maalumu wa Fidia kwa wanaokumbwa na matatizo
wakiwa kazini, kutokana na ukweli kuwa kwa sasa wafanyakazi wengi wanaumia na
kupoteza maisha katika ajira zao bila fidia yoyote.
Alisema
kupitia mpango huo, Serikali itachangia katika mfuko huo kila mwaka asilimia
moja ya mishahara yote, na kwa kuanzia katika mwaka ujao wa fedha tayari
zimetengwa Sh milioni 40 kwa ajili ya mfuko huo, huku waajiri wakitakiwa
kuchangia asilimia 0.5 katika mfuko huo kila mwaka.
Kuhusu
suala la baadhi ya waajiri na taasisi kukwepa kuanzisha mabaraza ya kazi na
matawi ya vyama vya wafanyakazi katika maeneo yao ya kazi, Rais Kikwete alisema
Sheria ya Kazi na Mahusiano Kazini pamoja na Sheria ya Utumishi wa Umma,
zimebainisha wazi umuhimu kila sehemu ya kazi kuwa na mabaraza na matawi hayo.
Alisema
kazi ya mabaraza na matawi hayo, ni kusimamia maslahi na kutetea haki za
wafanyakazi, lakini pia yanatumika kama daraja la mawasiliano baina ya
wafanyakazi na Serikali na kukwepa kuanzisha au kuanzisha na kutofanya
vikao ni kosa kisheria.
“Hawa
wanaokwepa kuanzisha matawi na mabaraza haya watawanyima haki wafanyakazi wao,
lakini pia Serikali tunajua kuwa wapo waajiri wameanzisha mifumo yao iliyo
kinyume na Sheria za nchi kwa kukwepa kuanzisha matawi haya, Wizara ya Kazi na
Ajira tumeni wakaguzi wenu na kuwafichua waajiri hawa,” aliagiza.
Katika
hatua nyingine Rais Kikwete, aliitaka Wizara ya Kazi na Ajira kutoa kipaumbele
kifedha na kutenga mfuko maalum kwa ajili ya kuwezesha Baraza la Usulushi
kutekeleza wajibu wake, kwa kuwa kwa sasa Baraza hilo, linashindwa kuwajibika
ipasavyo kutokana na uhaba huo wa fedha.
Rais
Kikwete pia alisisitiza umuhimu wa kuendelezwa kwa mfumo wa utatu, ambao ni
wafanyakazi, waajiri na Serikali katika kutatua matatizo ya wafanyakazi, ikiwa
ni sehemu ya utekelezaji wa utawala bora.
“Kaulimbiu
ya mwaka huu ya maadhimisho haya imebainisha wazi kuwa Utawala bora, utumike
kutatua kero za wafanyakazi, ni kweli kabisa, migogoro mingi ya wafanyakazi
inatokana na kukiukwa na kutotekelezwa kwa kanuni za utawala bora, hili sote
linatuhusu waajiri, wafanyakazi na Serikali,” alisema.
Aliwahakikishia
Watanzania kuwa Serikali inajitahidi kuhakikisha uchumi wa nchi unakua na
kugusa maisha ya watu, ambapo tayari katika tatizo la mfumuko wa bei,
imejitahidi na sasa hali imetengemaa.
Naye
Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudentia Kabaka, alimpongeza Rais Kikwete kwa
kupatiwa tuzo ya utawala bora Afrika, na kuwataka waajiri nchini kutumia fursa
hiyo kumuenzi kiongozi huyo kwa kuhakikisha wanafuata nyayo na kusimamia
utawala bora, ili kupunguza migogoro ya kazi.
Katibu
Mkuu wa Tucta, Nicholaus Mgaya, akiwasilisha risala ya wafanyakazi katika
maadhimisho hayo, aliiomba Serikali ishughulikie matatizo yanayowakabili
wafanyakazi ya uboreshaji wa mishahara, kupunguzwa kwa kodi ya P.A.Y.E na
kuboreshewa pensheni.
“Utafiti wetu wa mwaka 2006 ulibaini kiwango cha
chini cha mshahara kilichostaafu ni Sh 350,000…utafiti wa mwaka 2013 ulibaini
kiwango cha mshahara kuwa Sh 750,000 kwa mwezi kwa sababu ya kushuka kwa
thamani ya Shilingi pamoja na mfumuko wa bei, tunaomba utusaidie haya
yatekelezwe sasa,” alisisitiza.
No comments:
Post a Comment