Viongozi wa kitaifa wameonya kuhusu muelekeo wa
mchakato wa kupata Katiba mpya, kwamba usiachiwe kuvuruga amani, upendo na
mshikamano wa kitaifa, huku Rais Jakaya Kikwete akihadharisha kuwa
isipopatikana, Katiba hiyo, itatafutwa tena miaka ijayo.
Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa,
akikabidhi nyumba 30 za watumishi wa afya wa Mkoa wa Singida, zilizojengwa kwa
ufadhili wa Global Fund Round 9 na kusimamiwa na Taasisi ya Benjamin
Mkapa juzi, aliwataka Watanzania kuhakikisha mchakato wa Katiba mpya
unaoendelea hivi sasa, hauvurugi amani, upendo na utulivu uliopo nchini.
Kwa
upande wake Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, akihutubia katika kilele
cha Siku ya Wafanyakazi Duniani Mei Mosi jana Bwawani Zanzibar, alisema
zipo dalili kuwa baadhi ya wanasiasa wameanza kuutumia mchakato wa Katiba mpya
vibaya, kwa kuanza kujenga uhasama wa kisiasa ambao hatma yake ni nchi kuingia
katika machafuko.
Mkapa
alisema amani na utulivu uliopo nchini kwa miaka mingi havina budi kudumishwa
na kukuzwa, ili kuenzi waasisi wa Taifa letu.
“Vyovyote utakapoishia mchakato huu wa
Katiba…amani, upendo na utulivu lazima vihimili maisha yetu,” alisema Mkapa na
kuongeza: “Tuhitilafianeni lakini bila kupigana.”
Dk
Shein kwa upande wake kutokana na dalili alizozibaini, amewatahadharisha
wananchi na wanasiasa, kwamba mchakato wa kupata Katiba mpya usiwe chanzo cha
kuvuruga amani na utulivu uliopo na kujenga uhasama.
Alisema
kwa muda mrefu sasa Zanzibar imekuwa ikipata mafanikio makubwa, ikiwemo
kuimarika kwa amani na utulivu ambao umewafanya wananchi kuishi vizuri kwa
maelewano na kuzika tofauti za itikadi za kisiasa.
Alifafanua
kwamba mchakato wa Katiba kupitia Bunge Maalumu la Katiba, unatokana na Sheria
ya Mabadiliko ya Katiba na hakuna sababu za kujenga chuki na uhasama kama
inavyoanza kujitokeza.
“Wananchi
wa Zanzibar nawaasa kwamba Bunge Maalumu la Katiba lipo kwa mujibu wa Sheria na
wananchi kamwe wasijenge chuki na uhasama utakaosababisha nchi yetu kurudi
katika siasa za chuki na uhasama,” alisema.
Rais
Kikwete akizungumza katika Sikukuu ya Wafanyakazi Dar es Salaam jana, aliwataka
wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba, kutumia ipasavyo nyongeza ya siku 60
watakayopatiwa kwa kuja na uamuzi wenye manufaa kwa Watanzania, vinginevyo
ikishindikana, Katiba hiyo, itatafutwa tena miaka ijayo.
“Mimi
Rais kazi yangu nimemaliza ya kuteua wajumbe, sasa yanayoendelea mle ndani ni
ya kwao…kwa kweli nasikitishwa na kilichokuwa kikijiri ndani ya Bunge lile na
kuniacha na maswali kuwa hivi tusi ni hoja?” alihoji Kikwete.
Alisema
kuteuliwa kwa wajumbe hao kutoka taasisi, itikadi na maeneo tofauti, ilikuwa ni
moja ya mbinu ya kuibua mijadala mbalimbali ambayo ingewezesha kupatikana kwa
Katiba nzuri yenye manufaa kwa Watanzania.
“Hata
wazungu wanasema acha mawazo 100 yagongane ili kupatikane wazo moja la msingi,
lakini naamini kuwa wajumbe hawa hawataishia pale, watakaa na kutumia likizo
waliyonayo na kuja na mawazo mazuri na kutuletea Katiba mpya,” alisisitiza.
Aliwataka
Watanzania kuwatumia wajumbe wanaowawakilisha katika Bunge hilo, kuwasilisha
mawazo yao badala ya kuwaachia watoe mawazo yao jambo ambalo ni rahisi kwao
kutekwa na mawazo ya wengine.
Naye
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi, Nicholaus Mgaya, alisema
shirikisho hilo, limesikitishwa na mwenendo wa Bunge hilo la Katiba, ambao
umesababisha wananchi kupoteza imani nalo na kushauri wajumbe wote waliohusika
na makosa yaliyojitokeza kujirekebisha katika Bunge lijalo.
Tangu
kuanza kwa mchakato huo baada ya Rasimu ya Katiba mpya kukabidhiwa kwa Rais
Jakaya Kikwete, na wakati wote wa awamu ya kwanza ya Bunge Maalumu la
Katiba, mjadala mkubwa ulihamia katika muundo wa Muungano.
Rasimu
hiyo imependekeza muundo wa Muungano kuwa wa serikali tatu; Serikali ya
Tanganyika, Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Muungano.
Hata
hivyo, hoja mbalimbali zimekuwa zikitolewa kupinga muundo wa serikali tatu
kutokana na kuhusishwa na uvunjifu wa amani, upendo na mshikamano wa
Watanzania, ambao umedumishwa kwa miaka 50 ya Muungano sasa chini ya muundo wa
serikali mbili.
Baadhi
ya hoja hizo zilitolewa na Profesa Bonaventura Rutinwa wa Shule Kuu ya Sheria
ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), ambaye amekuwa akieleza namna muundo wa
Muungano wa serikali tatu utakavyoharibu mshikamano, umoja na upendo wa
Watanzania.
Alisema
kitendo cha Katiba ya Zanzibar kuita eneo hilo la Tanzania kuwa ni nchi na
kutoa haki kwa Wazanzibari, ambazo hazitatolewa kwa wasio Wazanzibari,
kitaharibu umoja na mshikamano uliopo, kama Tanganyika ikianzishwa katika mfumo
unaopendekezwa wa serikali tatu.
“Sasa
kwa kuwa Zanzibar tayari ina Katiba yake, inayotoa na kulinda haki za kisiasa,
kijamii na kiuchumi kwa Wazanzibari, huhitaji nguvu za kinabii kubashiri kuwa
Katiba ya Tanganyika ikija, itatoa na kulinda haki za kiuchumi, kisiasa na
kijamii kwa Watanganyika.
“Hii
ikitokea, itasababisha wananchi kutoka Tanganyika wanaoishi Zanzibar na
Wazanzibari wanaoishi Tanganyika kushindwa kudai haki zao za uraia kisheria,”
alionya Profesa Rutinwa.
Alihitimisha
kuwa katika mazingira hayo, mfumo unaopendekezwa wa serikali tatu, utafifisha
mshikamano wa Watanzania na serikali za nchi washirika, na katika hali mbaya
zaidi utazalisha kero mpya za Muungano zitakazokuwa na nguvu ya kuvunja
Muungano.
No comments:
Post a Comment