Makamu
wa Rais Dk Mohamed Gharib Bilal, jana aliongoza mamia ya wananchi wakiwamo
viongozi wa Serikali, mabalozi wa nchi mbalimbali na wanataaluma, kuuaga mwili
wa Balozi wa Malawi nchini, Flossie Chiyaonga.
Mbali
na Makamu wa Rais wengine waliohudhuria misa ya kuagwa kwa balozi huyo ni
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa
Katiba na Sheria, Dk Asha Rose Migiro na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje
na Ushirikiano wa Kimataifa, John haule.
Awali,
mwili wa marehemu uliingizwa katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius
Nyerere (JNICC) na baadae kufuatiwa na misa iliyoendeshwa na Mchungaji Peterson
Muridhi wa Kanisa la St Columbas la Upanga, aliyetokea nchini Kenya.
Akizungumza
katika ukumbi huo, Waziri Membe alisema kifo cha Balozi Chiyaonga kimewagusa
watu wengi kutokana na kuwa cha ghafla bila kutegemewa.
Alisema
alikuwa akitekeleza majukumu yake ipasavyo kwa kusaidia kuboresha uhusiano
baina ya nchi mbili ya Tanzania na Malawi, hivyo kuondoka kwake ni pengo kubwa
kwa nchi zote mbili.
"Alikuwa
mtu mzuri sana, ataishi milele tutamkumbuka daima lakini ataendelea kuwa nasi
daima na siku moja tutakutana. Huu mshituko tumepata wote, tunashirikiana
katika majonzi na maumivu katika kipindi hiki kigumu," alisema Waziri
Membe.
Alisema
mara zote Balozi Chiyaonga alikuwa akimsisitiza kuhakikisha kuwaunganisha watu
wa Tanzania na Malawi kuwa wamoja. Pia kuendeleza mazuri aliyofanya Balozi
Chiyaonga.
Mwakilishi
wa Ubalozi wa Malawi, Kwacha Chisiza alisema kifo cha Balozi huyo ni pigo kubwa
kwa serikali zote na kuishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuonesha umoja wao na
kutoa ndege ya kusafirisha mwili wa
marehemu. Waziri Membe anatarajiwa kuondoka leo pamoja na mwili wa marehemu.
Balozi
Flossie alifariki Ijumaa iliyopita wakati akipelekwa katika Hospitali ya Aga
Khan kwa matibabu, baada ya kuugua akiwa nyumbani kwake.
Jumatatu
iliyopita usiku, Balozi Flossie alijisikia vibaya na kupelekwa Aga Khan, ambako
alipatiwa matibabu na kuwekwa mapumziko kati ya saa sita usiku na saa 12
asubuhi, ambapo alipatiwa dawa za kutumia nyumbani na kuruhusiwa.
Kwa
mujibu wa Haule, hali ilibadilika mchana na kurejeshwa hospitalini lakini alipofikishwa Aga Khan, madaktari
walimfanyia vipimo na kubaini ameshafariki.
Alisema
wakati wa uhai wake, Balozi Flossie alifanya kazi zake kwa kuimarisha
ushirikiano baina ya Tanzania na Malawi na kushirikiana vizuri na mabalozi
wenzake wanaowakilisha nchi zao Tanzania.
No comments:
Post a Comment