Serikali
imetangaza na kusisitiza mpango wake wa kupunguza bei ya umeme kwa wananchi,
utakaoanza mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara
mpaka Dar es Salaam.
Naibu
Waziri wa Nishati na Madini, Stephen Masele, alisema hayo jana bungeni,
alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Martha Mlata
(CCM).
Martha
katika swali lake Mlata aliitaka Serikali kupunguza bei ya umeme, ili wananchi
wa kawaida watumie nishati hiyo kupikia
na kupunguza matumizi ya mkaa yanayochangia kuharibu mazingira nchini.
Akifafanua
zaidi, Masele aliwataka Watanzania kuvuta subira kwa kuwa ujenzi wa bomba hilo
kwa sasa umefikia kati ya asilimia 80 na 90 kukamilika na ukikamilika,
utawezesha kupungua kwa bei ya umeme.
Kwa
mujibu wa Masele, kwa sasa Shirika la Umeme (Tanesco), linanunua umeme kutoka
katika kampuni za ufuaji umeme wa mafuta kwa senti 38 na 55 za dola za Marekani
kwa uniti moja, ili kuwauzia Watanzania.
Wakati
kampuni hizo zikiuza umeme kwa bei hiyo, takwimu za Tanesco zinaonesha kuwa
shirika hilo linalazimika kuuza umeme huo kwa kati ya senti 10 mpaka senti 19
za dola za Marekani kwa uniti moja kwa wananchi.
Takwimu
hizo zinaonesha kuwa wateja wa majumbani uniti moja ya umeme wanauziwa kwa
senti 19 za dola za Marekani, wateja wa biashara senti 13, viwanda vya kati na
vikubwa senti 10 na taa za barabarani senti 19.
Kwa
takwimu hizo na kwa bei hizo, Tanesco katika kila uniti moja ya umeme inayouza
imekuwa ikipata hasara ya senti 28 mpaka 36 za dola za Marekani.
Katika
mpango wa Serikali, Masele alisema bomba hilo likianza kufanya kazi, umeme
utaanza kununuliwa na Tanesco kutoka kwa wafanyabiashara kwa kati ya senti nane
hadi tisa za dola za Marekani tofauti na sasa ambapo umeme unanunuliwa kwa kati
ya Dola 38 na 55.
Alifafanua
kwamba baada ya kuanza kununua umeme kwa bei nafuu, Serikali inapanga kupunguza
bei ya umeme katika muda usiozidi miezi 12.
Masele
alitangaza hayo bungeni huku kukiwa na taarifa kuwa wafanyabiashara wanaouzia
umeme Tanesco, wamekuwa wakipambana bei hiyo isishuke.
Wafanyabiashara
hao wenye mitambo ya kufua umeme wa mafuta na waagizaji wa mafuta, wanafanya
jitihada kuhakikisha lengo hilo halifikiwi, kwa kuwa watapoteza karibu Sh
bilioni nne wanazopata kila siku kutoka Tanesco.
Waziri
Mkuu Mizengo Pinda, alipokuwa mkoani Mtwara kukagua ujenzi wa bomba la gesi
hivi karibuni alisema kuwa wafanyabiashara hao wako katika mapambano kutaka
malengo ya kushusha bei ya umeme yasifikiwe.
“Sisi
tunaona kuwa suluhu ya kuondokana na gharama hizi (za umeme) ni gesi, lakini
kuna watu wanajua watanyang’anywa tonge mdomoni, vita hii tunaijua; lakini sisi
hatuwezi kurudi nyuma katika hili ni lazima tuendelee mbele,” alisema Pinda.
Pinda
alisema mapambano hayo yalianza tangu wakati wa jaribio la kuzuia gesi isifike
Dar es Salaam, kwa kuwa wafanyabiashara hao wanahofia kuwa mwisho wa biashara
yao ya kuuzia Tanesco umeme kwa bei ya juu, umefika.
Alisisitiza
kuwa Serikali imedhamiria kuachana na umeme huo wa mafuta na kama
wafanyabiashara hao wanataka kuendelea na biashara hiyo, ni vyema wabadilishe
mitambo yao iwe ya gesi na sio ya mafuta kama ilivyo sasa hivi.
No comments:
Post a Comment