MAMEYA, WAKURUGENZI WAKOROFI KUTIMULIWA KAZI



Serikali imesema kuanzia sasa itawaondoa madarakani mameya, wenyeviti wa halmashauri na wakurugenzi katika halmashauri zitakazokumbwa na mgogoro.
Waziri Mkuu Mizengo Pinda, alisema mjini hapa jana kuwa hatua hiyo inalenga kuwafanya viongozi wa halmashauri za wilaya nchini, kutumia muda mwingi katika kutekeleza miradi ya maendeleo, ili kuwaletea maendeleo wananchi.
Pinda aliyekuwa akifungua rasmi Mkutano Mkuu wa 30 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa (ALAT), unaokwenda sambamba na maadhimisho ya miaka 30 ya jumuiya hiyo, alisema tayari amemuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia kuangalia namna ya kuanza kutekeleza agizo hilo.
Alisema kutokana na ubinafsi  wa baadhi ya mameya, halmashauri zimekuwa zikitumbukia kwenye migogoro ya ajabu ajabu isiyo na tija wala maana kwa wananchi, hatua ambayo imekuwa ikisababisha mipango ya maendeleo kuzorota.
Kwa mujibu wa Pinda, kutokana na sababu mbalimbali Serikali imekuwa ikichukua hatua za kuwafukuza kazi wakurugenzi wa halmashauri kama njia ya kukuza nidhamu na uwajibikaji, ambapo alisema tayari wakurugenzi watano wamefukuzwa kazi.
“Ni vizuri sasa kila panapozuka tofauti katika maeneo yenu, mjenge mazoea ya kukaa chini na kujadili tofauti hizo ili kuzimaliza. Katika kila jambo mtakalokaa chini na kulijadili kwa muda mrefu, iwe ni kwa ajili ya kuwasaidia wananchi na si vinginevyo.
“Nchi yetu ina matatizo makubwa,  ipo migogoro ya wakulima na wafugaji na ipo migogoro ya kidini pia. Tumieni muda mwingi kujadili jinsi ya kuondoa matatizo haya, tumieni wazee katika maeneo yenu kuyamaliza haya ili tupate muda mwingi zaidi wa kuwaletea wananchi maendeleo,” alisema Pinda.                                         
Akitolea mfano wa mgogoro unaosababishwa na ubinafsi, Pinda alisema aliyekuwa Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba, Anatory Amani, ameshindwa kuangalia maslahi ya wananchi walio wengi na kung’ang’ania madaraka hayo, hatua inayofanya halmashauri hiyo kushindwa kufanya vikao vya kupitisha bajeti na kupanga mipango ya maendeleo.
“Suala hili la mgogoro wa Bukoba sijalipenda hata kidogo. Mgogoro huu wa Bukoba ni wa kipuuzi. Tulimtuma CAG (Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Ludovick Utouh) akagundua madudu ya ovyo mengi.
“Kwa kuona hali ilivyo tulimshauri Meya  yule ajiuzulu  kwa maana sasa fedha hazisimamiwi, hakuna vikao. Kwanza alikubali na katika kikao akasema ameona ajiuzulu, watu wakashangilia pale na nikaletewa barua ya kujiuzulu kwake na mimi nikaipitisha kukubali.
“Lakini baada ya siku tatu madiwani wanaomuunga mkono, wakakimbilia mahakamani kuzuia kufanyika kwa vikao vyovyote na Hakimu akawakubalia. Sasa kuna mradi wa kuboresha Mji wa Bukoba wa thamani ya Sh bilioni 17, ulikuwa ufanyike lakini nao umekwama na fedha hizo sasa zitarudi zilikotoka.
“Sasa huu ni ubinafsi wa hali ya juu sana, yaani Meya unafikia hatua unaangalia maslahi yako binafsi na si maslahi ya wananchi. Mbele ya maslahi ya umma wewe mtu mmoja si chochote. Suala la kujiuzulu ni suala la baraka kwa  Mungu maana leo wewe mtu mmoja upo na kesho haupo,” alisema.
Awali Mwenyekiti wa ALAT  Taifa, Dk Didas Massaburi, alimueleza Waziri Mkuu mafanikio yaliyofikiwa katika kuboresha maisha ya wananchi katika ngazi  za Serikali za Mitaa, huku akisema mafanikio hayo yameelekezwa katika ugatuaji wa fedha kwenda katika serikali za mitaa, ugatuaji wa rasilimali watu, uboreshaji wa uhusiano baina ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa na pia kuwajengea uwezo madiwani katika kutekeleza majukumu yao.

No comments: