Wananchi wa Mkoa
wa Dar es Salaam wametakiwa kwenda
katika hospitali za Serikali wanapohisi dalili za ugonjwa wa denge, kwa kuwa
matibabu hutolewa bure wakati Serikali ikijiandaa kusambaza vifaa vya kupimia
ugonjwa katika
wilaya zote nchini.
Makamu wa Rais,
Dk Mohamed Gharib Bilal akifungua Kongamano la Pili la Kisayansi lililoandaliwa
na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (Muhas), alisema Serikali haina mzaha katika kukabiliana na
mlipuko wa
ugonjwa wa
denge.
Alisema Serikali
imeamua kusambaza vipimo hivyo, baada ya kuonekana kuwa ni tishio kwa
maisha ya binadamu hivyo serikali imejipanga kuhakikisha ugonjwa huo
unatokomezwa.
“Kutokana na
ukubwa wa tatizo hili, tayari Serikali imejipanga kipambana na ugonjwa huu, ndio
maana sasa tumeandaa mkakati wa kusambaza vifaa vya vipimo vya ugonjwa huu kwa
kupitia wilaya zote nchini,” alisema Dk
Bilal.
Akizungumzia
masuala ya utafiti nchini, Bilal alisema wanaweka mikakati kuongeza rasilimali
watu hasa vijana katika masuala ya utafiti ikiwemo katika masuala ya afya,
ikiwa ni pamoja na kufanyia kazi tafiti hizo.
Awali Makamu
Mkuu wa Muhas, Profesa Ephata Kaaya, alisema chuo hicho kimeandaa kikosi kazi
maalumu kwa ajili ya kufanya utafiti kuhusu ugonjwa huo, ambacho kitashirikiana
na watafiti wengine.
Profesa Kaaya
alisema lengo la kongamano hilo ni kutafakari na kuangalia malengo waliyojiweka
chuoni hapo hasa katika masuala ya utafiti kama yamefanikiwa katika kufikia
malengo ya maendeleo endelevu na nini kifanyike katika kukamilisha yale
yalisalia.
Naye Mkurugenzi
Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA), Profesa John Mkoma, alisema kwa
sasa Mamlaka yake kupitia Muhas na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii,
wameanza kutumia simu za mkononi kwa ajili ya kufikisha taarifa mbalimbali kwa
wananchi kwa njia ya ujumbe mfupi.
Alisema lengo la
kutumia simu za mkononi, ni kutoa taarifa kwa haraka kwa wananchi juu ya
masuala mbalimbali ya afya yanayotokea, ikiwemo magonjwa ya milipuko kwa nia ya
kupunguza maambukizi kwa haraka.
Naye Mkuu wa Mkoa
wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki, alisema matibabu ya denge yanatolewa bure
na kuwataka wananchi wakijisikia dalili, kwenda katika hospitali za Serikali.
“Tunaomba
wananchi wanapohisi dalili za ugonjwa huo kwenda katika hospitali za Serikali,
ambazo ni Amana, Mwananyamala na Temeke kwa kuwa matibabu yanatolewa bila
malipo,” alisema Sadiki alipokuwa akizungumzia gharama za matibabu ya homa
hiyo.
Mkuu huyo wa
Mkoa alisema kwa sasa wanajenga uwezo ili kila wilaya iwe na vituo vitano
kwa ajili ya matibabu ya ugonjwa huo.
Sadick aliongeza
kuwa Serikali itanyunyuzia dawa ya (Lavacide) sehemu za mikusanyiko kama vile
mashuleni na kwenye madimbwi, lakini maeneo ya hotelini na mabaa
watapaswa kunyunyuzia dawa kwa gharama zao.
“Kwa upande wa
wizara, idara na taasisi za Serikali wanapaswa kunyunyuzia dawa kwa
gharama zao, (yaani matumizi mengineyo),” alisisitiza huku akisema hata kwenye
ofisi yake wamefanya hivyo kwa gharama zao.
Sadiki aliwataka
viongozi wa mitaa na watendaji wengine kuwahimiza wananchi kuhusu usafi wa
mazingira ili kupunguza maambukizi ya ugonjwa huo.
Alisema wananchi
wanapaswa kuhakikisha vifuu vya nazi na visoda kwani maji kidogo
yanayokaa katika vitu husababisha mbu wanaosababisha ugonjwa huo
kuzaliana.
Alisisitiza
hatua ya kwanza kuzuia ugonjwa huo ni usafi wa mazingira na dawa ni hatua ya
mwisho.
Katika
hatua nyingine, Serikali imeshauriwa
kuwapa semina waganga wa tiba
mbadala kuhusu hali halisi ya ugonjwa
huo, ili kuepuka kuibuka kwa wataalamu
watakaodai wanatibu na kuwafanyia majaribio
wagonjwa.
Ushauri
huo ulitolewa jana Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Mandai Herbal Clinic, Dk
Abdallah Mandai, wakati akizungumzia ugonjwa wa denge na kuongeza kuwa umekuwa
ni tatizo la kitaifa linalohitaji hatua stahiki za kukabiliana nalo.
Hivi
karibuni, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Charles Pallangyo,
alisema dalili za ugonjwa huo ni kuumwa kichwa, maumivu ya viungo na uchovu na
dalili hizo huanza kujitokeza kuanzia siku 3 hadi 14 tangu mtu alipoambukizwa
kirusi cha homa ya denge.
“Kwa wakati mwingine dalili za ugonjwa huu
zinaweza kufanana na dalili za malaria, hivyo basi tunawaomba wananchi wakipata
homa kuhakikisha wanapima kama wana malaria au la, ili hatua stahiki
zichukuliwe,” alisema Pallangyo.
Aidha
aliongeza kuwa kuna aina tatu tofauti za ugonjwa huo katika namna
unavyojitokeza, iwapo mtu aking’atwa na mbu mwenye virusi hivyo.
Aina
ya kwanza ndio homa ya denge yenyewe, ambayo huambatana na dalili kuu tatu za
homa kali ya ghafla, kuumwa kichwa na maumivu ya viungo au uchovu. Kwa Tanzania
mpaka sasa zaidi ya asilimia 90 ya wagonjwa wamejitokeza wakiwa na dalili hizo.
Aina
ya pili ni denge ya damu, ambayo huambatana na dalili za magonjwa kutokwa na
damu kwenye fizi au puani na kutokwa na damu chini ya ngozi. Iwapo mgonjwa huyo
ataumia sehemu yoyote, ni rahisi kupoteza damu nyingi kupitia kwenye michubuko.
Aina
ya tatu ni denge ya kupoteza fahamu, ambayo huambatana na mgonjwa kupoteza damu
nyingi ambayo husababisha mgonjwa kupoteza fahamu.
Mpaka
sasa dalili hizo zimeonekana kwa mgonjwa mmoja kati ya wagonjwa 400
waliokwishwathibitika kuwa na ugonjwa hapa nchini.
No comments:
Post a Comment