Kesi ya
kusambaza dawa bandia za kupunguza makali ya Ukimwi (ARVs), inayomkabili Ofisa
Mtendaji Mkuu wa kiwanda cha Tanzania Pharmacetical Ltd ambaye pia ni
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhan Madabida na wenzake,
imeahirishwa hadi Juni 10 mwaka huu.
Jana kesi hiyo
ilitajwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa ajili ya kuwasomea
washitakiwa maelezo ya awali, lakini Hakimu Mkazi Nyigulila aliahirisha kwasabu
ya kwenda kwenye msiba.
Alidai anaahirisha
kesi hiyo hadi Juni 10 kwa kuwa wanakwenda kwenye mazishi ya daktari bingwa wa
magonjwa ya akili, Gilbert Buberwa aliyefariki kwa ugonjwa wa dengue.
Mbali na
kushitakiwa kwa kusambaza dawa hizo, Madabida na wenzake wanadaiwa kusababisha
hasara ya Sh milioni 148 baada ya kusambaza dawa hizo kupitia kiwanda chake cha
TPL kwa Bohari ya Dawa Tanzania (MSD).
Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ya
uhujumu uchumi ni wafanyakazi wa kiwanda hicho Mkurugenzi Uendeshaji, Seif
Shamte, Meneja Masoko, Simon Msoffe na Mhasibu Msaidizi, Fatma Shango, pamoja
na wafanyakazi wa MSD, Meneja Udhibiti Ubora, Sadick Materu na Ofisa Udhibiti
Ubora, Evans Mwemezi.
Inadaiwa Aprili 5 mwaka 2011, Madabida,
Shamte, Msoffe na Fatma walisambazia MSD makopo 12,252 ya dawa bandia za Antiretroviral,
ikionesha zimetengenezwa Machi 2011 na mwisho wa matumizi Februari mwaka jana
pia walijipatia Sh milioni 148.35 kwa madai ni malipo halali ya dawa hizo.
Materu na Mwemezi wanadaiwa, kati ya
Aprili 5 na 13, 2011, Dar es Salaam, wakiwa waajiriwa wa MSD, kwa nia ya
kutenda kosa la kusambaza dawa hizo, walishindwa kutumia uwezo wao wote kuzuia
kutendeka kwa kosa hilo.
Katika mashitaka mengine, washitakiwa
wote wanadaiwa kati ya Aprili 5 na 30, mwaka 2011, kwa nia ovu au sababu za
kutotekeleza majukumu yao vizuri, walisababishia MSD hasara ya kiasi hicho cha
fedha, kutokana na kuwasambazia dawa bandia.
No comments:
Post a Comment