Waziri wa Maendeleo
ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba amesema mauaji ya wanawake katika mkoa
wa Mara yanalitia taifa aibu na uvunjaji wa sheria na haki za binadamu.
Alisema hayo
jana wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya Siku
ya Familia yaliyofanyika mjini hapa.
Alisema kwa
mwaka 2014 mauaji ya wanawake mkoani
Mara yanalitia taifa aibu na
kutaka vyombo vya habari kusaidia kuelimisha jamii ili kila mwanajamii aweze
kuishi kwa amani na utulivu.
Pia alisema
maadhimisho ya siku ya familia yanakumbusha kutafakari jinsi ya kutatua changamoto
za malezi ya watoto .
“Siku hizi
wazazi na walezi wanawaacha watoto wao kulelewa na wasaidizi wa kazi majumbani,
marafiki au walimu shuleni bila kufuatilia mienendo yao kwa kisingizio cha kazi
nyingi na hivyo kutokuwa na muda wa kukaa na familia zao,” alisema.
Alisema hata
pale wazazi wanapokaa na watoto wao hawana mbinu stahiki za malezi bora kiasi
cha kusababisha watoto wao kuiga kile wanachokiona au kusikia kutoka kwa
wenzao, shuleni, wanakocheza au wasaidizi majumbani.
Alisema taarifa
ya ukatili dhidi ya watoto uliofanyika hapa nchini kati ya mwaka 2009 hadi 2010
ulionesha kuwa ukatili dhidi ya watoto ni wa aina tatu wa kingono, kimwili na
kihisia na mara nyingine watoto hukabiliwa na aina zote tatu za ukatili.
Aidha utafiti
huo ulionesha kiwango cha ukatili hapa Tanzania ni kikubwa na cha kutisha,
vitendo hivyo vinafanyika katika ngazi ya familia ambapo wazazi, walezi na
ndugu wa karibu pamoja na walimu ndio wahusika wakuu.
Alisema takwimu
zinaonesha asilimia 30 ya wasichana na asilimia 14 ya wavulana walifanyiwa
ukatili wa kingono na ndugu, wakati asilimia 80 ya wasichana na asilimia 65 ya
wavulana walifanyiwa ukatili wa kihisia kabla ya kufikisha umri wa miaka 18.
Simba alisema
familia ni msingi wa Taifa lolote duniani ni vyema mipango imara na ushirikiano
wa kutosha unahitajika miongoni mwa wanafamilia, viongozi na wataalam waliopo
katika ngazi ya jamii ili kulinda maadili na kuelimisha umuhimu wa malezi bora
kwa watoto hasa katika kipindi cha ukuaji.
Aidha akizindua
kampeni ya kupiga vita ukatili wa kingono, alisema pamoja na serikali kufanya
juhudi mbalimbali za kutokomeza ukatili wa kijinsia bado matukio ya ukatili
yanaongezeka.
“Hapa Tanzania
takwimu zinaonesha kuwa theluthi moja ya wanawake walio na umri kati ya miaka
15 hadi 49 wamefanyiwa ukatili wa kijinsia na wenzi wao au ndugu zao,” alisema.
No comments:
Post a Comment