KANISA LA TAG LAANDAA IBADA YA UAMSHO MIAKA 75



Kanisa la Tanzania Assemblies of God (Victory Christian Center Terbenacle) Mbezi A jijini Dar es Salaam linaloongozwa na Mchungaji Kiongozi, Dk Huruma Nkone, katika kuelekea maadhimisho ya miaka 75 ya Tag, limeandaa ibada maalumu ya Uamsho.
Ibada hiyo itaongozwa na Mhubiri maarufu duniani, Rais wa SOS Mission International, Mwinjilisti Johannes Amritizer kutoka Sweden na inatarajia kutikisa Jiji la Dar es Salaam na vitongoji vyake, Mei 11, mwaka huu.
Mwinjilisti Amritizer ni miongoni mwa wahubiri wakubwa duniani ambaye Mungu amempa vipawa vya ajabu hususani katika maeneo ya ishara na miujiza kwa watu ambao wana mahitaji mbalimbali kama vile magonjwa na matatizo mengine ambapo pia Mwinjilisti huyu amekuwa akifanya makongamano makubwa sehemu mbalimbali duniani pamoja na kujikita vyema katika kulichambua vyema Neno la Mungu. 
Akizungumza, Dk Nkone alisema hiyo ni  fursa ya kipekee na wanajisikia kuheshimiwa kwa mhubiri mkubwa mwenye ratiba nyingi duniani kukubali kuja Tanzania kuendesha ibada maalumu.
Akieleza zaidi, alisema tayari maandalizi ya ibada hiyo yamekamilika na tayari kanisa limejipanga kuhakikisha maelfu ya wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wanahudhuria ibada hiyo ya kipekee ambayo haijawahi kutokea ambapo mabasi maalumu kutoka Mwenge yameandaliwa kuwabeba washiriki wote.

No comments: