Taarifa
isiyo sahihi ya maambukizi ya homa ya dengue inayoenezwa na mbu aina ya aedes,
imesababisha baadhi ya madereva teksi jijini Dar es Salaam, kujilinda kwa kuvaa
glovu za mikononi, soksi ndefu miguuni na kujifungia muda wote katika magari
yao hata ambayo hayana viyoyozi.
Uchunguzi
wa gazeti hili wiki hii, umebaini madereva hao wamekuwa wakivaa soksi
miguuni hata kama wamevaa kandambili, huku wakiwa na glovu viganjani kwa madai
kuwa wanaogopa kuumwa na mbu mwenye virusi hivyo.
Wakizungumza
na mwandishi, baadhi ya madereva wa kituo cha mtaa wa Mindu Upanga,
walikiri kuvaa mavazi hayo kujikinga na ugonjwa huo ambao hauna tiba.
“Kwa
kweli ugonjwa huu ni hatari kama hauna tiba , unafikiri tutapona kweli, ni heri
tuvae hivi, au tujifungie ndani ya gari wakati tunasubiri wateja,” alisema Juma
Hassan mmoja wa madereva teksi hao.
Hassan
alimruhusu mwandishi kuzungumza naye akiwa amejifungia ndani ya gari huku jasho
likimtoka na kulowanisha shati lake, kwa hofu kwamba akifungua madirisha, mbu
wataingia na kumwambukiza ugonjwa huo.
Baraka
Joseph dereva teksi wa kituo hicho, yeye alikuwa amevaa koti na miguuni amevaa
soksi pamoja na kandambili, na alisema taarifa alizonazo zinaonesha ugonjwa huo
unatisha kwani unaua muda mfupi na hauna tiba, hivyo sio ugonjwa wa kuudharau
hata kidogo.
“Ugonjwa
huu unatisha na tumesikia hapa mjini watu wengi wameupata, sasa kazi yetu hii
tuko vijiweni tangu alfajiri hadi muda huu (saa mbili usiku), ni lazima
tujikinge vinginevyo tutautapa na hatujui kama tutapona,” alisema Joseph.
Hali
kwenye kituo cha kona ya Muhimbili, ambako taksi huwa zinapaki hapo, ilikuwa
tofauti ambapo kulikuwa na dereva mmoja tu, ambaye naye alisema wenzake
wameondoka kwa kuwa maeneo hayo kuna mbu wengi wanahofu ya kuumwa na kupata
homa ya dengue.
“Nimebaki
mimi ,lakini hata hivyo naondoka, nimejipaka dawa ya kuzuia mbu ila bado nina wasiwasi
huenda mbu mwenye virusi hivyo akaniuma nikaupata, sasa itakuwa shida,
kwa kweli ugonjwa huo unatutisha,” alisema Rashid Muhammed, ambaye ni dereva wa
teksi eneo la Kona ya Muhimbili.
Wakati
huo huo, Mkoa wa Shinyanga ulijikuta ukilazimika kukanusha uvumi ulioenea
kuhusu kulipuka kwa ugonjwa wa dengue, baada ya kulazwa kwa mgonjwa mmoja
mwenye viashiria vya ugonjwa huo katika hospitali ya mkoa.
Akizungumza
na gazeti hili ofisini kwake mjini hapa jana Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa
wa Shinyanga, Dk Ntuli Kapologwe, alikanusha kulipuka kwa ugonjwa huo mkoani
hapa, baada ya vipimo vya mgonjwa huyo vilivyopelekwa Dar es Salaam, kubaini
hana ugonjwa huo.
“Ni
kweli mtoto aliyelazwa katika hospitali ya mkoa alikuwa na viashiria vya
kuambukizwa ugonjwa huo vya uchovu, kuishiwa nguvu, kutokwa na damu
puani na homa kali, lakini hakuwa na ugonjwa wa dengue kwa kuwa vipimo vyake
kuonesha anasumbuliwa na ugonjwa mwingine ambao unatibika kwa tiba
sahihi,” alisema Dk Kapologwe.
Uvumi
kuhusu kuibuka kwa ugonjwa huo, ulisababisha mkanganyiko uliowakumba
baadhi ya wagonjwa waliofikia hatua ya kutaka kukimbia wadini ili
kunusuru maisha yao wakihofia kuambukizwa ugonjwa huo.
Dk
Kapologwe alisema, ili kuthibitisha kuwa mgonjwa aliyefika hospitali kupatiwa
matibabu anasumbuliwa na maradhi ya dengue, ni lazima vipimo vyake vipelekwe
kwenye Maabara Kuu jijini Dar es Salaam na majibu ya vipimo yathibitishe kuwa
kweli mgonjwa huyo ameambukizwa ugonjwa huo.
Akizungumzia
kinga ya ugonjwa huo, Dk Kapologwe aliwataka wananchi kuchukua tahadhari kwa
kuchoma na kuangamiza mazingira yanayoweza kuwa chanzo cha mazalia ya mbu ambao
husababisha ugonjwa huo.
No comments:
Post a Comment