AJALI YA GARI YAUA WATU WATANO MLIMA SEKENKE



Watu watano wamekufa papo hapo na wengine 16 kujeruhiwa baada ya kutokea ajali ya barabarani  iliyolihusisha gari dogo la abiria aina ya Toyota Hiace  eneo la Mlima Sekenke, wilayani Iramba kwenye Barabara Kuu ya Singida -Mwanza.
Mganga wa zamu katika Hospitali ya Wilaya ya Iramba,  Dk Antony Mbulu,  alisema kuwa ajali hiyo ilitokea juzi saa 2:30 usiku wakati abiria  hao  wakienda kwenye sherehe ya Maulid kijiji jirani cha Shelui.
Dk Mbulu aliwataja waliokufa katika ajali hiyo kuwa ni dereva Athuman Adam (34) na Ally Wambura (36), wakazi wa Igunga na Amin Salim (45) mkazi wa mjini Singida. Alisema miili ya watu wawili haijatambuliwa.
Kwa mujibu wa Dk Mbulu, ajali hiyo ilitokea baada ya dereva wa basi hilo lenye namba za usajili T547 ASP kushindwa kulimudu kutokana na mwendo kasi.
Alisema kuwa majeruhi watano kati ya 16 waliolazwa kwenye hospitali hiyo, wamehamishiwa katika Hospitali ya Mkoa wa Singida kwa matibabu zaidi huku hali zao zikielezwa kuwa mbaya.
Baadhi ya majeruhi ambao hawakutaka kutajwa majina yao gazetini, walisema ajali hiyo ilitokana na mwendo kasi na kutokuzingatia sheria za usalama barabarani.
Walidai kuwa ajali ilitokea wakati dereva huyo akipita malori kwa kasi, ndipo akagonga kingo za barabara na kupasua tairi kabla ya kuingia msituni na kupinduka mara nne. Basi hilo dogo lilikuwa limebeba abiria 21 likitokea mjini Singida kwenda Shelui.  

No comments: