Mgonjwa
mmoja mkoani hapa, amethibitika kuugua ugonjwa wa dengue na kulazwa katika
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza ya Sekou Toure.
Hayo
yalibainishwa jana na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Baraka Konisaga katika
mkutano wake na waandishi wa habari, uliofanyika jijini hapa kufuatia kuwepo
kwa taarifa za mgonjwa huyo.
“Napenda
wananchi wa Mkoa wa Mwanza, watambue kuwepo kwa ugonjwa wa dengue na kwamba
hadi sasa mgonjwa mmoja amethibitika kuugua na amelazwa tangu jana (juzi),”
alisema.
Mganga
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Valentine Bangi alisema mgonjwa huyo, ambaye ni
mtumishi wa serikali mstaafu (bila kutaja jina lake) na mkazi wa Kilimahewa,
alifika hospitalini kwa mara ya kwanza Mei 20, mwaka huu.
Alisema
alifanyiwa vipimo, lakini siku iliyofuata alirudi na kusema hali yake sio nzuri
na ndipo walipoamua kuchukua vipimo vya dengue.
Alisema
Mkoa umepokea vipimo 50 vya ugonjwa wa dengue, ambapo 10 wamevisambaza
katika Wilaya ya Kwimba, 10 Wilaya ya Ukerewe na 10 wilayani Sengerema.
Alisema
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii itapeleka vitendanishi vingine kwa sababu
hivyo vilivyopo, walivipokea kabla ya kuwepo kwa ugonjwa huo mkoani hapa.
Ugonjwa
huo huambukizwa na virusi, wanaotokana na mbu aina ya Aedes, baada ya kumng’ata
mtu mwenye ugonjwa huo na kisha kumng'ata mtu mwingine.
Asilimia
90 ya wagonjwa walioambukizwa, huonesha dalili ndani ya siku tatu hadi 14.
Dalili hizo ni homa kali, kichwa kuuma machoni, kichefuchefu, kutapika, kuvimba
tezi, maumivu makali ya viungo na kupatwa na harara.
Hivi
karibuni, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Kebwe S. Kebwe alisema
mabadiliko ya tabianchi na mwingiliano wa safari, vimesababisha kuwepo kwa
ugonjwa wa dengue, ambao ulianzia kwenye nchi za Asia.
No comments:
Post a Comment