Kampuni
ya Ndege ya Tanzania (ATCL) imerejesha safari zake katika anga za Arusha na
Zanzibar na kuahidi kusafiri katika maeneo hayo yenye vivutio bora vya
kiutalii mara sita kwa wiki.
Katika
safari hiyo ya uzinduzi ya kutoka Dar es Salaam kwenda Zanzibar kupitia Arusha,
iliyofanyika jana, kulikuwa na mawaziri wawili wa pande zote za Muungano
. ATCL itakuwa ikitumia ndege yake aina ya Bombardier Dash - 8 yenye
uwezo wa kubeba abiria 50 katika njia hiyo.
Ikitokea
Dar es Salaam kwenda Arusha, alikuwemo Waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro
Nyalandu na wakati wa kutoka Zanzibar kwenda Dar es Salaam, alipanda Waziri wa
Nchi katika Ofisi ya Rais (Utawala Bora) wa Serikali ya Zanzibar, Dk
Mwinyihaji Haji Makame.
Akizungumza
mara baada ya kutua katika uwanja wa ndege wa Arusha, Nyalandu alisema kurejea
kwa ndege za ATCL katika njia ya Arusha na Zanzibar, kutakuza sekta ya utalii
na kurahisisha uunganishwaji wa maeneo hayo muhimu yenye vivutio vikubwa vya
utalii.
“Uzinduzi
wa safari hii unadhihirisha kwamba sasa ushindani wa kweli katika sekta ya
usafiri wa anga umeanza. ATCL inatakiwa kuhakikisha inaendeleza dhamira yake ya
kutoa huduma bora ili iweze kurejesha imani iliyokuwanayo kwa abiria wake walio
wengi,” alisema Nyalandu.
Kaimu
Mkurugenzi wa Biashara wa ATCL, Juma Boma alisema safari ya Dar es Salaam –
Arusha – Zanzibar ni sehemu ya mkakati wa shirika lake kutanua huduma katika
maeneo mengi iwezekanavyo.
“Tunajivunia
kuendelea kutekeleza dhamira yetu ya kuimarisha huduma zetu tukiwa kama
kampuni ya ndege la taifa. Tukilenga kuendelea kutanua wigo wa huduma
zetu ndani ya nchi na kimataifa. Lengo letu kubwa ni kuendelea kutoa huduma
zenye gharama nafuu, vile vile kuongeza uwezo wa abiria kusafiri kwa wakati
wao,” alisema.
Alisema
wameondoa adhabu kwa abiria wanaochelewa kufika uwanja wa ndege au
kushindwa kufika siku ya safari na wanaobadilisha tarehe za safari zao.
Waziri
Makame alisema inatia moyo kuona ATCL ikirejesha safari zake Zanzibar baada ya
kusitisha huduma zake katika kisiwa hicho kwa zaidi ya miaka minne.
Alitaka
ATCL kufuata muda na kuhakikisha wanapunguza adha ya usitishaji wa safari
endapo wanataka kurejesha imani miongoni mwa abiria walio wengi.
Akizungumza
baada ya kupokea safari hiyo ya uzinduzi katika uwanja wa ndege wa Arusha, Mkuu
wa Wilaya ya Arusha, John Mongela alisema kuanza kwa safari katika Makao
Makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki , kumerejesha sifa iliyokuwa nayo ndege
hiyo ya taifa kipindi cha nyuma wakati wa mikutano ya kimataifa jijini
Arusha.
No comments:
Post a Comment