Polisi
mkoani Morogoro, inaendelea na uchunguzi wa kilichotokea mpaka mtoto
mmoja mkoani hapa (jina limehifadhiwa), akateswa na mzazi mlezi kwa kuwekwa
katika boksi tangu akiwa na miezi tisa, mpaka alipotimiza miaka minne.
Jana
kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Leonard Paul, Baba mzazi wa
mtoto huyo, Rashid Mvungi ambaye ni mtumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya
Morogoro alitakiwa kuja kutoa maelezo yake kituoni leolakini hakutokea.
Kamanda
Paul alisema walijaribu kumtafuta mzazi huyo kwa simu ili kumkumbusha umuhimu
wa kufika Polisi kutoa maelezo, lakini simu zake zilikuwa zimezimwa.
Mwandishi
alifika kwa mwajiri wake katika Ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro,
ambako hakuwepo kwa kuwa aliaga kwamba amekwenda katika Kituo cha Ustawi wa
Jamii, alikodai kuwa aliitwa.
Hata
hivyo, mwandishi alipofika katika ofisi hiyo, lilihakikishiwa Ofisa Ustawi wa
Jamii, Oswin Ngungamtitu, kuwa Mvungi hakuwa amefika katika eneo hilo, wala
hakukuwa na mwito wa yeye kufika katika ofisi hiyo.
Katika
tukio lingine la kutia shaka, mwandishi alipohojiana na Mvungi katika nyakati
tofauti juzi, alitoa taarifa mbili tofauti, kuhusu sababu za kumuacha mwanaye
kwa mama mkubwa wake, Mariam Said, aliyemuweka katika boksi kwa zaidi ya
miaka mitatu.
Katika
mahojiano ya awali, Mvungi alidai baada ya mzazi mwenzake, Mwasiti Ramadhan
kufariki dunia, alishindwa kumchukua mtoto wake kwa sababu tayari alishakuwa na
mke.
Alidai
kwa kuwa alikuwa ameoa, alikubaliana na upande wa pili wa familia ya marehemu,
kuwa mwanaye huyo alelewe na mama yake mkubwa, Mariamu.
Katika
mahijiano na mwandishi mwingine juzi hiyo hiyo, Rashid alidai mwanae huyo
alichukuliwa na Mama yake mkubwa ili kumlea akiwa na umri ndogo na mara
zote alikuwa akipeleka fedha za matumizi.
Alidai
kwa mara ya mwisho alimwona mwanae huyo miezi miwili iliyopita akiwa na afya ya
kuridhisha, wakati taarifa zilizotolewa na Mariam, zilidai kuwa mtoto huyo
hajaogeshwa tangu Julai mwaka jana.
“
Kila nikienda kumwona nyumbani kwao sikubahatika kumwona , nilikuwa nikiambiwa
amelala ama ametoka na watoto wezake...isipo kuwa miezi miwili iliyopita,” alidai
Rashid kauli inayoonesha kuwa mtoto huyo alikuwa akitoka na wenzake wakati
majirani walitoa ushahidi kuwa hawakuwahi kufahamu uwepo wa mtoto katika nyumba
hiyo.
Taarifa
kutoka katika Hospitali ya Rufaa mkoani Morogoro, zimeeleza kuwa baada ya
uchunguzi wa awali wa afya ya mtoto huyo, alibainika kuwa na niumonia, ulegevu
wa viungo ikiwa ni pamoja na baadhi ya mifupa katika mwili wake
kuvunjika.
Daktari
Mshauri wa watoto, Hores Msaky alipozungumza na gazeti hili jana, alisema
walimpokea mtoto huyo juzi alikuwa katika hali ya uchafu usio wa kawaida.
Msaky
alisema waliamua kumfanyia vipimo vya awali pamoja na picha za X ray,
wakagundua kuwa mifupa yake si ya kawaida, inaonekana
imevunjika ingawa hawajajua nini kimemvunja.
“Tunachokifanya
hivi sasa ni kujaribu kujua tatizo hilo limetokana na nini,”
alisema daktari huyo
Hata
hivyo Msaky alisema kuwa hospitali hiyo haina vifaa vingi vya kupimia mifupa,
hivyo imeshauriwa apelekwe Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, jijini Dar es
Salaam kwa ajili ya uchunguzi
zaidi
.
Muandishi
wa habari hizi alifanikiwa kuingia wodi aliyolazwa mtoto huyo na kumkuta akiwa
amechangamka, na alipoulizwa anaendeleaje alisema anasikia maumivu katika
sehemu
ya
kifua .
Mtoto
huyo alikuwa akidhulumiwa haki yake ya utu na kuteswa kwa zaidi ya miaka
mitatu, kwa kufungiwa ndani ya boksi kama mnyama, ili asiamumbukize mama mlezi
virusi vinavyosababisha Ukimwi.
Unyama
huo wa kusikitisha, ulikuwa ukifanyika muda wote huo kwa mtoto huyo Morogoro
mjini katika mtaa wa Azimio bila kuripotiwa popote, huku wakazi na majirani wa
nyumba hiyo wakisikia akikohoa na kulia usiku, na baba yake mzazi akiendelea na
maisha kwa kumuogopa mkewe.
Wakizungumza
na mwandishi juzi majirani hao walidai Mariam alihamia katika nyumba hiyo mwaka
2010, lakini hawakuwahi kumuona akiwa na mtoto.
Hata
hivyo majirani hao walikiri kwamba walikuwa wakisikia mtoto akikohoa na kulia
hasa nyakati za usiku, lakini walikuwa na wasiwasi kuwa huenda mtuhumiwa
alikuwa mshirikina anayefuga watu waliouawa kishirikina au kwa jina linguine
misukule.
Hatimaye
juzi mateso ya mtoto huyo yalipungua, baada ya msamaria mmoja kupata taarifa
sahihi, kwamba ndani ya nyumba hiyo kuna kiumbe asiye na hatia aliye katika
mateso na kutoa taarifa kwa Ofisa Mtendaji wa Kata ya Kiwanja cha Ndege, Dia
Zongo.
Zongo
akiwa katika kazi za kawaida katika mtaa huo, alipata taarifa kutoka kwa
majirani kuwa kuna mwanamke, Mariamu Said, amemficha mtoto ndani ya boksi na
hamfanyii usafi wala kumtoa nje.
Baada
ya kupata taarifa hizo, Zongo alimtafuta mwenyeji wake, Mwenyekiti wa mtaa huo,
Tatu Mgagalana na kuongozana naye hadi kwenye nyumba hiyo ambapo
walimkuta mtuhumiwa, Mariamu na kuanza kumuhoji kuhusu tuhuma hizo.
Kwa
mujibu wa Zongo, wakati mtuhumiwa akijibu maswali aliyoulizwa huku akibabaika,
ghafla mtoto huyo alipiga chafya na kuanza kukohoa hali iliyowapa wasiwasi na
kuamua kuingia chumbani kwa Mariamu kwa nguvu, hatua iliyomuokoa mtoto huyo
kutoka katika mateso ya zaidi ya miaka mitatu.
Ofisa
huyo na mwenyeji wake walimkuta mtoto huyo ametapakaa uchafu uliotokana na
kinyesi na mkojo, kwa kuwa boksi hilo lilikuwa chumba chake cha kulala, meza
yake ya chakula na maji na choo kwa ajili ya haja ndogo na kubwa.
No comments:
Post a Comment