Uwepo
wa vyombo mbalimbali vinavyotoa kibali cha kufanya kazi nchini, umetoa mwanya
kwa wageni kuingia nchini na kuajiriwa katika nafasi za kazi, ambazo baadhi
hata Watanzania wana uwezo wa kuzijaza.
Mwishoni
mwa wiki iliyopita wakati wa Sikukuu ya
Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi), Rais Jakaya Kikwete alisema Serikali imebaini
kuwa tatizo hilo la kutolewa kwa vibali kiholela, linatokana na vibali hivyo,
kutolewa na taasisi zaidi ya moja.
Mwandishi
amepata taarifa kutoka Wizara ya Kazi na Ajira, inayoonesha namna wafanyakazi
hao, wanavyopata vibali vya kufanya kazi nchini, jambo lililolalamikiwa na
wafanyakazi kuwa baadhi ya wageni hao, wanapata ajira ambazo Watanzania
wanaweza kuzijaza kwa ufanisi.
Kwa
mujibu wa taarifa hiyo, vibali vya kufanya kazi nchini kwa wageni, vimekuwa
vikitolewa na Wizara ya Kazi na Ajira, kupitia Kamati ya Utatu inayoundwa na
Wizara, Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta) na Chama cha Waajiri nchini (ATE).
Hata
hivyo, baada ya mgeni kukubaliwa kupata kibali na Wizara kupitia utatu huo,
wageni hao hupata kibali kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Idara ya
Uhamiaji ambacho ni kibali Daraja B, kinachoruhusu wageni watakaoajiriwa kwa
masharti ya kudumu tu.
Mbali
na Wizara ya Kazi na Ajira, taarifa hiyo imeeleza kuwa vibali Daraja A na C,
hutolewa moja kwa moja na Idara ya Uhamiaji, bila kupitia Wizara hiyo.
ÒIdara
ya Uhamiaji pia ina mamlaka pia ya kutoa vibali vya muda mfupi bila kupitia
Wizara ya Kazi na Ajira, mfano vibali vya miezi mitatu mpaka sita kwa wageni
ambao wanakuja kufanya kazi kwa muda mfupi,Ó imeeleza taarifa hiyo.
Utaratibu
unaotumiwa na Wizara ya Kazi na Ajira, kutoa kibali kwa mgeni kufanya kazi
nchini, kwa kushirikisha ATE na Tucta, huzingatia mambo mbalimbali.
Kwanza
taarifa hiyo imeeleza kuwa kibali hukubaliwa kwa kuzingatia idadi ya miradi,
ambayo kampuni husika inayo na muda ambao miradi hiyo itakamilika.
Pia,
kabla ya kutoa kibali, mapendekezo ya wizara zenye dhamana ya kupendekeza
waombaji huzingatiwa, mfano Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa upande wa
walimu, Wizara ya Ujenzi kwa wageni katika miradi ya ujenzi na Wizara ya Afya
na Ustawi wa Jamii.
Kwa
mujibu wa taarifa hiyo, sababu nyingine inayozingatiwa wakati wa utoaji kibali
katika Wizara ya Kazi na Ajira, imetajwa kuwa ni cheo cha muombaji, ukubwa wa
kampuni na idadi ya Watanzania, walioajiriwa na kampuni husika.
Mamlaka
nyingine inayohusika kutoa vibali vya ajira kwa wageni ni Kituo cha Uwekezaji
nchini (TIC).
Kwa
mujibu wa taarifa hiyo, Sheria ya Uwekezaji ya 1997 Ibara ya 24 (1) (2),
inaruhusu waombaji watano wa mwanzo katika mradi wa uwekezaji, wapewe vibali
vya kufanya kazi nchini, hata kama sifa zao Watanzania wanazo.
Mbali
na waombaji hao watano wa mwanzo, Sheria hiyo imewaruhusu pia wawekezaji,
kuongeza wageni zaidi ya hao watano katika ajira wanazotoa, kulingana na
umuhimu wa mtu wanayemuombea.
Nafasi
zao, watokako
Kwa
mujibu wa taarifa hiyo, uchambuzi uliofanyika wizarani, umeonesha wageni wengi
wanaokuja kufanya kazi nchini, hupendelea nafasi za umeneja, ambazo ndizo zenye
malipo mazuri.
"Uchambuzi
unaonesha mameneja (uendeshaji, masoko, fedha na kadhalika), ndio wanaoongoza
kwa idadi ya wageni wanaokuja kufanya kazi nchini," taarifa hiyo imeeleza.
Wengine
ni wataalamu, ambao hawako katika mchanganuo wa kisekta, wakiwemo mafundi
mchundo katika sekta ya ujenzi, walimu, wasimamizi, mameneja wakuu na
wakurugenzi, wafanyakazi katika viwanda vya chuma, wahandisi na wanasayansi.
Nchi
zinazoongoza kwa kuwa na wingi wa wageni wanaofanya kazi nchini, kwa mujibu wa
taarifa hiyo, ni India ikifuatiwa na China, Kenya, Afrika Kusini, Pakistani na
Uingereza.
Taarifa
hiyo imekiri kuwa kumekuwa na udanganyifu mkubwa kwa wanaopewa vibali hivyo,
ambapo baadhi ya wawekezaji wanapata vibali na kufanya kazi, ambazo hazipo katika vibali vyao.
"Wafanyabiashara
ndogo hasa maduka, hawapendekezwi kupewa vibali isipokuwa kumekuwa kukifanyika
udanganyifu mkubwa, mfano wanaingia nchini kama wawekezaji na nyaraka zote
muhimu wanapata na wakipewa hawafanyi lengo lililowaleta.
"Wizara
ya Viwanda na Biashara, Msajili wa
Makampuni (Brela) na TIC kubaini mbinu zote na kuchukua hatua kwa kuwa ili mtu
afanye biashara hapa nchini, taasisi mbalimbali zinahusika," ilieleza
taarifa hiyo.
Akizungumza
mwishoni mwa wiki katika sherehe za Mei Mosi, zilizofanyika kitaifa jijini Dar
es Salaam, Rais Kikwete alisema kutokana na kukithiri kwa malalamiko ya
Watanzania, kuhusu kutolewa holela kwa vibali vya kazi kwa wageni, Serikali
inafikiria kurekebisha Sheria ya Vibali vya Ajira kwa Wageni, ili kudhibiti
ipasavyo utolewaji wa vibali hivyo.
Alisema
Serikali imebaini kuwa tatizo hilo la kutolewa kwa vibali kiholela, linatokana
na vibali hivyo kutolewa na taasisi zaidi ya moja.
"Hali
hii inatoa fursa kwa watumishi wasio waaminifu kutumia mwanya huo wa taasisi
nyingi kuidhinisha vibali hivi na kuvitoa hata kwa watu wasiostahili kwa
kujinufaisha, hili hatuwezi kulinyamazia," alisema Rais Kikwete.
Alisema
kutokana na kukithiri kwa tatizo hilo, Serikali imekuwa ikipokea malalamiko
mengi kutoka kwa wananchi, juu ya kujaa kwa wageni nchini, wanaofanyakazi hata
zile zinazoweza kufanywa na wananchi wa kawaida, jambo linalowanyima ajira
wananchi wengi.
Aliwaahidi
Watanzania kuwa Serikali imeliona tatizo hilo na iko kwenye mchakato wa
kulifanyia kazi kwa kuipitia upya Sheria hiyo na kuandaa muswada wa marekebisho
katika kipengele cha vibali vya ajira kwa wageni.
Alisema
moja ya mapendekezo, yanayofanyiwa kazi kwa ajili ya kurekebishwa katika sheria
hiyo, ni pamoja na eneo la taasisi zinazohusika kutoa vibali hivyo, ambapo
katika marekebisho hayo, itapendekezwa iwe taasisi moja pekee.
"Tutarekebisha
na kutoa fursa ya kutoa vibali hivyo kwa taasisi moja pekee na kuiongezea
udhibiti, ili endapo kutatokea wafanyakazi wasio waaminifu iwe rahisi kuwabaini
na kuwadhibiti," alisisitiza.
No comments:
Post a Comment