Chama
Cha Mapinduzi (CCM) kimemtaka Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Seif
Sharif Hamad, kama kweli hataki Muungano wa serikali mbili, amuandikie
barua Rais wa Zanzibar, Dk Mohamed Shein
na kujiuzulu wadhifa wake wa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.
Tamko
hilo lilitolewa jana na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, wakati
akihutubia mkutano mkubwa wa hadhara, uliofanyika kwenye viwanja vya
Kibandamaiti mjini Unguja.
Kinana
alisema anachokifanya Seif ni sawa na kuwaramba vichogo wanasiasa wenzake wa
upinzani, wakati yeye akipata mshahara na marupurupu mengine, yanayomwendeshea
maisha yake chini ya serikali ya CCM.
Alisema
kama kweli Maalim Seif anajigamba ni jasiri, achukue uamuzi sahihi wa kujiuzulu
wadhifa wake, ili apate nafasi ya kutosha kuwatumikia wananchi nje ya Serikali.
Kinana
alieleza kuwa kutembea nchi nzima kwa Seif, si kitendo cha uungwana kufanywa na
kiongozi mwenye wadhifa wa Makamu wa Kwanza wa Rais, akiwa ndani ya Serikali
inayomlipa mshahara na huduma nyingine muhimu, akaamua kuwachochea wenzake,
ambao wako nje ya Serikali kuleta chokochoko dhidi ya Serikali anayoitumikia.
Maalim
Seif ameshatuhumiwa kuwa kigeugeu katika maisha yake ya kisiasa, ambapo hivi
karibuni Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, Mohammed Seif Khatib, alielezea
namna kiongozi huyo wa CUF, alivyowahi kuwa mtetezi wa serikali mbili alipokuwa
kiongozi katika Serikali ya CCM, ambako alitumia nguvu kubwa kupinga vuguvugu
la kudai serikali tatu mwaka 1984.
Khatibu
alinukuu kauli ya Maalim Seif alipokuwa akipambana na watu, waliokuwa wakitaka
serikali tatu, akiwepo Rais wa Zanzibar wa wakati huo, Aboud Jumbe.
"Msimamo
wa Jumbe umetufadhaisha sisi sote, tunataka maelezo yake kwa kuwa ni dhahiri
hoja ya serikali tatu haikuanzishwa na watu wadogo, imechangiwa pia na baadhi
ya viongozi wa Baraza la Mapinduzi na Aboud Jumbe ni chanzo cha hayo,"
alinukuliwa Maalim Seif akisema mwaka 1984.
Viongozi
ambao Maalim Seif alikuwa akisema wanataka serikali tatu na kwa kufanya hivyo
wamemfadhaisha na wanastahili adhabu pamoja na Jumbe ni Jamal Faki, Abuu Salim na Wolfgang Dourado,
ambaye alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Kwanza wa Zanzibar.
"Tuangalie
viongozi wanaobadilika badilikaĆmwaka 1984 Maalim Seif alitaka serikali mbili,
mwaka 1992 akiwa CUF msimamo wake ukawa serikali tatu, juzi serikali ya
mkataba, huyu ni kiongozi wa aina gani? Ni wa kuongopea watu tu," alisema
Khatibu.
Kinana
katika mkutano wa jana aliendelea kusema: "Maalim Seif aache kuwababaisha
wananchi, atulie kwa sababu ameamua kutumikia serikali za CCM na hana uwezo
wowote wa kuvuruga amani ya Taifa kama anavyojigamba kwenye majukwaa ya
kisiasa."
Aliongeza
kuwa Katibu Mkuu huyo wa CUF, anaposimama na kutaka muundo wa Muungano wa
serikali tatu, hiyo ni danganya toto, lakini kila mwenye macho na masikio,
anatambua nia ya kiongozi huyo ni kutaka kuusambaratisha Muungano wa Tanganyika
na Zanzibar kwa maslahi yake na rafiki zake.
Kinana
alisema Tanganyika kukosa Serikali wakati Zanzibar ikiwa na mamlaka ya ndani si
kioja, kwani hata Uingereza yenye Muungano wa nchi za Wales, Scotland, Ireland
ya Kaskazini na England, ina kiti kimoja Umoja wa Mataifa. Pia, alisema England
ambako anatoka Malkia Elizabeth II, haina Serikali.
Kwa
upande wake, Mnadhimu wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Salmin Awadh Salmin,
alisema wawakilishi wa CCM wanatazamia kuwasilisha hoja binafsi kwenye Baraza
la Wawakilishi Zanzibar, ili wananchi waulizwe kama wanaafiki mfumo wa Serikali
ya Umoja wa Kitaifa visiwani humo au la.
Salmin
alisema dhamira na madhumuni ya kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa,
imefutika na haileti tena matumaini kwa wananchi, kwa kuwa pande mbili za
kisiasa, zinazounda ushirika huo, zina itikadi zinazotofautiana.
"Tutawasilisha
hoja binafsi Baraza la Wawakilishi, ili wananchi wapige kura ya maoni kama
wanaafiki muundo huo au hawautaki, CCM haitakubali kufanya kazi na watu wenye
itikadi, mitazamo na misimamo tofauti, wenzetu ni adui wa Muungano na Mapinduzi
Zanzibar," alisema Salmin.
Mjumbe
wa Kamati Kuu ya CCM, Dk Emmanuel Nchimbi, aliwaeleza wananchi kwamba hakuna
mahali ambapo Rais Jakaya Kikwete, alisema majeshi yatachukua nchi, kama
inavyoenezwa kwa uongo na wapinzani kwa makusudi.
Dk
Nchimbi alifafanua kuwa Rais Kikwete alisema kukiwa na Muungano wa serikali
tatu na ile ya Muungano ikiwa haina vyanzo vya uhakika vya mapato, kuna hatari
ya Jeshi kuchukua madaraka ikiwa wanajeshi watashindwa kulipwa mishahara yao
kwa wakati na kwa uhakika.
"Kinachofanywa
na wapinzani ni kutapatapa kwa kukosa hoja, wasimlishe maneno Rais ambayo
hajayasema, waseme alivyosema na kama wana hoja wajibu kwa nguvu ya hoja na si
hoja dhaifu na upotoshaji unaoendelea," alisema Dk Nchimbi.
Akizungumzia
kuhusu Muungano, alitoa mfano wa Taifa la Marekani, lenye Muungano wa nchi
zaidi ya 50, ambapo katika miaka 47 ya Muungano, taifa hilo lilipata
misukosuko, lakini halikuyumba na mpaka sasa limebaki kuwa taifa moja lenye
kiti kimoja katika Umoja wa Mataifa.
Alisema
nchi nyingine zote katika Taifa hilo, zina mamlaka ya ndani na hakuna Mmarekani
hata mmoja, anayefikiria au kutamani kusambaratika kwa Taifa hilo lenye nguvu zaidi
kiuchumi duniani.
Katika
hatua nyingine, Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), wamehadharishwa na tabia
ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar,
Maalim Seif, kwa kuwa ni mwanasiasa
kigeugeu, anayeweza kuwasaliti na kuwatosa wakati wowote.
Katibu
wa Idara ya Oganaizesheni ya CCM, Seif Khatib, alisema hayo wakati akihutubia
mkutano wa hadhara katika uwanja wa Kibandamaiti mjini Unguja, Zanzibar.
Khatib
alisema Umoja huo, hautafika mahali popote, kwani mmoja kati ya wanachama wa
umoja huo, ambaye ni Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif, atawatosa kama
alivyomtosa aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Aboud Jumbe.
Alitaja
viongozi wengine waliowahi kutoswa na Maalim Seif mwaka 1984 kuwa ni Waziri Kiongozi wa zamani,
Ramadhan Haji Faki na aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Wolfang Dourado.
Alisema
anawashangaa viongozi wa vyama vya
Chadema, NCCR-Mageuzi, DP na NLD kukubali kushirikiana na kiongozi huyo, mwenye
sifa na historia ya kusaliti wanasiasa wenziwe na viongozi wa kiserikali katika
maisha yake.
"Alimsaliti
Jumbe mwaka 1984, akamtosa James Mapalala mwaka 1994, akachongea kina Naila
Jidawi na Shaibu Akwilombe na mwisho amemzamisha Hamad Rashid Mohamed, Ukawa
iko siku watajuta kumsikiliza kiongozi huyo," alisema Khatib.
Aidha,
Mwanasiasa huyo mkongwe na Waziri wa zamani wa Muungano, aliwaeleza wananchi
kwamba kitendo cha kiongozi huyo, kuwashinikiza wajumbe wa Bunge la Katiba,
wasusie vikao vya Bunge Maalum wakati yeye akiwa Makamo wa Kwanza wa Rais, ni
aina ya usaliti wa kisiasa.
Kwa
upande mwingine, Mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde, aliwaasa wananchi wa
Zanzibar, kumpuuza Maalim Seif na badala yake waendelee kudumisha amani,
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kuyalinda Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka
1964.
"Nje
ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Mapinduzi ya Zanzibar yatapotea, amani,
umoja wa kitaifa na mshikamano vitapotea, ni jukumu la kila mmoja kukataa
uchochezi wa aina yoyote, unaoenezwa na wapinzani nchini," alisema Khatib.
No comments:
Post a Comment