POLISI MWANGA WAGOMA KUSAKA WAVUVI HARAMU



Baraza la Madiwani la Hamashauri ya Wilaya ya Mwanga, limeunda kamati ya watu watano ili kumuona Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, kujua sababu za kuwapo mgomo wa vyombo vya dola katika kudhibiti uvuvi haramu katika Bwawa la Nyumba ya Mungu.
Kamati hiyo itaongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uchumi, Ujenzi na Mazingira, Kuria Rajabu na itakuwa na wajumbe Enea Mrutu, Kilavo Mndeme, Mohamed Mgala na Sofia Sharokiwa. Itaanza kazi mara moja  kunusuru kutoweka kwa samaki katika bwawa hilo.
Kamati hiyo itakuwa huru na itakuwa na jukumu la kutafuta chanzo cha mgomo huo waliouita baridi, licha ya Halmashauri  kutenga Sh milioni 100 katika bajeti yake ya mwaka 2013/2014, ambazo hazijatumika hadi sasa.
Akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani la Halmashauri hiyo, Mrutu  ambaye ni Diwani wa Kata ya Shighatini, alisema anashangazwa na kutotumika kwa fedha hizo, licha ya kwamba uvuvi haramu unaendelea kwa kasi.
Hofu ya Baraza iliyosababisha kuundwa kwa kamati hiyo, inatokana na taarifa ya Kamati ya Uchumi, Ujenzi na Mazingira, kuelezea changamoto zinazowakabili, ikiwa ni pamoja na kushindwa kuanza kwa operesheni hiyo baada ya kukosa ushirikiano na Jeshi la Polisi.
Awali,  akiwasilisha taarifa ya Kamati yake, Kuria alisema fedha hizo zilitengwa kwa ajili ya semina na operesheni ya kuzuia uvuvi haramu na kwamba katika operesheni zilizopita, wananchi waliharibu magari ya Polisi.
Hata hivyo akizungumza kwa simu, Mkuu wa Wilaya ya Mwanga, Shaibu Ndemanga, alisema vyombo vya dola havijagoma kushiriki operesheni hiyo, bali kilichotakiwa kufanywa ni ushirikishwaji wa wanajamii wenyewe, badala ya kutanguliza nguvu za polisi.
Alisema maelekezo yaliyotolewa ni kutaka kufahamu mipango ya halmashauri,  baadaye kama itaonekana kuna vurugu,  ndipo Polisi itatumika kuhakikisha usalama unakuwepo, badala ya kuwatumia sasa, ambapo inaweza kuonekana mabavu zaidi yanatumika.
Alisema iwapo polisi watahitajika kulingana na hali halisi, watakwenda katika operesheni hiyo na kuongeza kuwa siku za nyuma kulitokea uvumi, uliosababisha magari ya Polisi kuvunjwa vioo na wananchi wanaojiita wenye hasira.
Kutokana na taarifa hiyo, Mrutu alilieleza baraza hilo kuwa huenda matokeo ya operesheni zilizopita, ndiyo sababu zilizosababisha polisi kususia kushiriki operesheni nyingine za halmashauri hiyo, ingawa alisema kamati iliyoundwa, itatoa jibu kamili.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo,Theresia Msuya alithibitisha kuwapo kwa mgomo huo,  aliosema aliuthibitisha kupitia taarifa aliyopewa na Mkuu wa Wilaya ya Mwanga, kuwa Polisi inataka wanajamii wenyewe washiriki operesheni hiyo.
Alisema mgomo huo, umeifanya Wilaya ya Mwanga kuomba msaada wa Polisi kutoka Mkoa wa Tanga, ambao hata hivyo hawajaupata, kwa madai bado Polisi mkoani Kilimanjaro, haijatoa kibali kwa Polisi Mkoa wa Tanga kutoa msaada, kama zilivyo taratibu za jeshi

No comments: