Kampuni
ya Clouds Media International imepatiwa leseni ya kurusha
matangazo katika nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Taarifa
iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo
inayomiliki Clouds Radio na Clouds Tv, Joseph Kusaga ilisema kuwa kwa sasa
Clouds TV International imekuwa ya kimataifa na itakuwa ikishuhudiwa na watu wa
mataifa mbalimbali.
"Clouds
TV kimataifa ni mwendelezo wa televisheni maarufu sana kwa vijana nchini
Tanzania, hata hivyo sehemu kubwa ya maudhui yatakayokuwemo kwenye Clouds
TV kimataifa itakuwa na mpangilio mpana wa vipindi kwa watazamaji
vitakavyorushwa kwa lugha za Kiingereza na Kifaransa,” alisema Kusaga.
Kusaga
aliongeza kuwa "Leo ni siku ya kihistoria na alama ya hatua moja
katika mpango wetu wa kina wa kupeleka maudhui ya Clouds TV kimataifa
kupitia matangazo kwa njia ya mitandao.’’
Alisema
kuwa Clouds TV kimataifa haitatoa tu burudani, lakini pia itakuwa kiunganishi
kwa Waafrika waishio katika Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu pamoja na kuwapa
fursa za kutangaza bidhaa zao na kuimarisha uhusiano baina yao.
Aliongeza
kuwa vituo vya televisheni katika Umoja wa Falme za Kiarabu vipo vingi na
vyenye ushindani mkubwa, lakini Clouds TV kimataifa imebahatika kupata nafasi
ya kurusha matangazo yatakayowafikia walengwa katika chaneli yenye uwezo wa
kuwahudumia zaidi ya watazamaji takribani milioni 3.5 kutoka katika nchi
za Afrika.
“Kwa
sasa hakuna kituo kinachotoa huduma hii na hivyo kuwa fursa muhimu kwa
watazamaji,” alisema Kusaga.
Alifafanua
kuwa Clouds TV kimataifa itarusha vipindi vya burudani, tamthiliya, maigizo,
ucheshi, na muziki, vyote vitakavyo kuwa vimeandaliwa kutoka nchi za Mashariki,
Magharibi na Kusini mwa bara la Afrika na itapatikana kwa watazamaji walio
katika Umoja wa Falme za Kiarabu kupitia huduma ya IPTV inayotolewa na
Etisalat na Du.
No comments:
Post a Comment